Habari za Punde

Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale atoa mwongozo kwa wageni na watalii wanaoingia nchini

 Na Khadija Khamis -Maelezo Zanzibar 14/02/2021

Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar Lela Muhamed Mussa ametoa muongozo kwa wageni na watalii wanaoingia nchini  kufuata maadili yanayohusiana na mavazi ili kwenda sambamba na mila silka maadili na utamaduni wa kizanzibari .

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari alisema hivi karibuni kumejitokeza  ukiukwaji wa maadili  hususani katika suala la mavazi kwa baadhi ya wageni na watalii wanaotembelea  nchini.

Alifahamisha kuwa wageni na watalii wanatakiwa kufuata maadili ya nchi kwa kuvaa nguo za stara wanapokuwa katika  sehemu  za umma  ili kuepusha kero na maudhi kwa wananchi.

Alieleza  kuwa kushindwa kuifuatilia na kuisoma miongozo ya maadili ambayo imekuwa ikitolewa na taasisi zinazosimamia utalii nchini ni miongoni mwa sababu zinazopelekea utaratibu mbaya wa mavazi kwa wageni hao.

Waziri  Lela alisema hali hii haitoi sura nzuri na inaashiria kutokuwepo uwajibikaji wa pamoja na mashirikiano kwa baadhi ya wananchi au taasisi ambazo zinashindwa kusimamia suala la maadili kwa wageni na watalii wanaoingia nchini.

Alisema serikali haipendezeshwi na hali ya kivazi kwa wageni na watalii ikiamini kwamba pamoja na kuhitaji utalii kwa maslahi ya wananchi na serikali kwa ujumla lakini inaheshimu suala la maadili ya jamii.

Alieleza kuwa  kutokana na kutoridhishwa na hali hiyo Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale imeona ipo haja ya kusisitiza umuhimu wa kusimamia maadili kwa watalii kwa vile mila, silka,  na utamaduni wa Zanzibar ni urithi na ni miongoni mwa vivutio  vya utalii .

 Waziri huyo alizitaka jumuiya zenye kuandaa misafara ya kitalii nchini (tour operators )ambazo zimabeba jukumu la kuleta wageni kuzingatia kanuni za mwaka 2015 kifungu cha 51 (b)inayozipa jukumu la kuhakikisha watalii wanaowasimamia wanafuata sheria pamoja na kuwapatia kanuni za maadili kwa watalii kabla ya kuwafikisha nchini pamoja na kuwasimamia kufuata maadili hayo wanapoingia nchini.

Hata hiyo  alisema kwa upande wa wenye Mahoteli na mikahawa ya kitalii kuwa  na wajibu wa kutoa taarifa kuhusiana na miongozo ya maadili kwa watalii na wageni na ni marufuku kwa wenye kuendesha biashara ya hoteli kuwavisha nguo zisizo na stara wafanyakazi wao .  

Wizara inaviomba vyombo vya ulinzi na usalama nchini kushirikiana pamoja na wadau wengine wa utalii katika kukabiliana na kadhia hiyo.

Alifahamisha Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale imeshawasiliana na ofisi za kibalozi za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  katika nchi mbali mbali duniani na kuwapatia maadili ya utalii wa Zanzibar.







No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.