Habari za Punde

Uzinduzi wa filamu ya Ndonga

Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Vijana , Utamaduni na Michezo Fatma Hamadi Rajab akizungumza na Wasanii wa Tanzania bara na Zanzibar( hawapo pichani) kuhusu kuigiza Maigizo katika Utamaduzi wa Mtanzania katika Uzinduzi wa Filam ya Ndonga huko  Ukumbi wa Sanaa Raha leo Mjini Zanzibar.
Msaidizi Mratibu Maeneo ya Hifadhi za Bahari Zanzibar kutoka  Idara ya Maendeleo ya Uvuvi Omar Hakim Foum akiwasisitiza Wasanii (hawapo pichani) kutunga Maigizo ya kuhamasisha Uchumi wa Bluu  katika Uzinduzi wa Filam ya Ndonga Ukumbi wa Sanaa Raha leo Zanzibar.
Mkurugenzi wa Kikundi cha Allan Culture Mwahija Mungi akisoma Risala ya Filamu ya Ndonga katika Uzinduzi wa Filam hiyo Ukumbi wa Sanaa Raha leo Mjini Zanzibar.
Mvuvi wa Chaza Khusuu Juma Said akizungumza kuhusu kupewa kipao mbele katika Uvuvi huo katika Uzinduzi wa Filamu ya Ndonga Ukumbi wa Sanaa Raha leo  Zanzibar.

Baadhi ya Wasanii kutoka Bara na Zanzibar waliohudhuria Uzinduzi wa Filam ya Ndonga Ukumbi wa Sanaa Raha leo Mjini Zanzibar.

Picha Na Bahati Habibu -  Maelezo Zanzibar


MARYAM KIDIKO MAELEZO ZANZIBAR  13/ 2/2021

Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Vijana , Utamadni na Michezo Fatma Hamad Rajab amewataka wasanii nchini kufanya kazi zao kwa kuzingatia mila, tamaduni na desturi za Kitanzania ili ziweze kudumu na kurithisha vizazi vijavyo.

Akizungumza katika uzinduzi wa Filamu ya Ndonga ilioandaliwa na kikundi cha Allan Culture kutoka Dar es Salaam  huko ukumbi wa Sanaa Rahaleo amesema utamaduni ni lulu ambayo inahitaji kuenziwa, hivyo Sanaa zitumike vizuri katika kuutangaza utamaduni wa Mtanzania ndani na  nje ya nchi.

Amesema watu wengi wamepata maendeleo kupitia Sanaa hivyo amewataka vijana kujifunza Sanaa ili waweze kuzalisha Sanaa yenye viwango inayokubalika na jamii hatua ambayo itaibuwa fursa nyingi za ajira na kuwaingizia kipato.

Akizungumzia kuhusiana na Filamu ya Ndonga bi. Fatma ameeleza kuwa filamu hiyo iliyobeba maudhui ya kuielimisha jamii juu ya kulinda mazingira ya bahari na madhara yatokanayo na uvuvi haramu, itasadia kuipa mwanga jamii katika kufikia azma ya serikali ya kufikia maendeleo ya uchumi wa buluu.

Aidha amewasisitiza wasanii kujisajili katika vyombo husika ili waweze kutambulika na kupata haki zao za msingi kupitia kazi zao.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dk. Khamis Abdallah Said amesema filamu ya Ndonga itumike kutoa elimu kwa jamii ili mazingira ya bahari yawe salama na kuweza kuliingizia mapato taifa.

Kwaupande wake Mkurugenzi wa kikundi cha Allan Culture Mwahija Mungi amesema Sanaa ni kazi kama kazi nyengine hivyo ameiomba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Habari, Vijana Utamaduni na Michezo kuionesha filamu ya donga kupitia vyombo vya habari vilivyopo Zanzibar ili maudhui ya filamu hiyo ifike katika jamii ya wazanzibari kwa haraka.


 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.