Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe.Othman Masoud Othman akisalimiana na Viongozi wa ACT wazalendo Wiya ya Kaskazini B Unguja waliojitokeza kaika ziara iliyoandaliwa na chama cha ACT wazalendo kwa ajili ya kuwatembelea wagonjwa na kuwafariji Visiwani Zanzibar.
Na.Talib Ussi -Zanzibar.
Makamo wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe.Othman Masoud Othman amesema Zanzibar inahitaji kuendelea na Umoja ili iwe rahisi kuleta maendeleo kwa wananchi wake. Kauli hiyo amaeitoa mara baada ya kukamilisha ziara ya kichama ilioandaliwa na Chama cha ACT- Wazalendo kwa ajili ya kutembelea wagonjwa katika Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Makamu wa Kwanza wa Rais Mhe.Othman Masoud alisema hakuna njia nyengine itakayoweza kuleta maendeleo bila kuwepo mashirikiano, upendo na umoja miongoni mwa Wazanzibar.
Alieleza kuwa yupo tayari kutoa mchango wake kwa kuwatumikia wananchi kwani anaamini nao wapo tayari kuendeleza upendo na amani juu ya nchi yao.
“Na mimi naweka ahadi ya kuwatumikia wazanzibar kwa wakati wowote ili kuendeleza yale yaliyoanzishwa na kuweza kuleta tija katika muendelezo wa kuyaimarisha zaidi” alisema Othamn.
Alisema anayoimani kwamba anaweza kutoa mchango wake katika kutumikia watu na kufanyakazi kwa moyo na wananchi kwa malengo ya uwepo Umoja wa kitaifa uweze kufikiwa.
“Ili tupendane basi tuwe wamoja kwani umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu” alisema othaman.
Alifahamisha kuwa umoja na upendo ndio silaha pekee ya uwepo wa amani kudumu katika taifa loloote lile duniani.
Alisema upendo na umoja huo unapendeza zaidi watu wakitembeleana na kusaidiana kwa wale wanaohitaji msaada.
Kutokana na kauli hiyo aliwaomba wananchi wote kuwa na utamaduni wa kutembeleana kuazia familia, majirani pamoja na marafiki kwa lengo la kujenga upendo miongoni mwao.
Alisema mgonjwa yeyote akiona anatembelewa na jamaa zake au majirani, marafiki basi hujisikia faraja kupunguza maumivu ya maradhi.
Sambamba na hilo aliwashauri wananchi wa Zanzibar hasa mwezi huu mtukufu wa Ramadhani kuftari kwa umoja ili kuwa karibu zaidi na kuwastiri wale waliokuwa hawana uwezo.
Alisema kuna watu wengi hawana Ftari lakini kama utamaduni wa kuftari kwa pamoja ndugu na majirani utaendelea basi utaleta faida kubwa miongoni mwao.
Katika Ziara hiyo ya kuangalia na kuwafariji wagonjwa katika vijiji vya Mkoa wa Kaskazini Makamu wa Kwanza alitembelea wagonjwa katika Vijiji vya Chaani, Matemwe ,Nungwi, Kendwa, Kilimani Tazari, Mahonda ,Bumbwini Mafufuni, na Kiomba Mvua.
No comments:
Post a Comment