Habari za Punde

Akinamama wapigwa msasa kuhusu Udhalilishaji waaswa kutokuwa na muhali


 Bahati  habibu                        Maelezo  Zanzibar 

 

Wazazi  na walezi  wametakiwa kutokuwa na muhali kwa watu wanaowafanya  vitendo vya udhalilishaji kwa watoto na wanawake  ili kufikia lengo la Serekali la kuondosha udhalilishaji nchini. 


Hayo yameelezwa na  afisa wa dawati jinsia wanawake na watoto  Mkoa wa Kusini Unguja Najat Saleh  Abdulkadir wakati akiwasilisha mada ya udhalilishaji katika kikao cha  Baraza la UWT Jimbo la Tunguu huko Tunguu.


Amesema kesi nyingi za udhalilishaji zinashindwa kufikia hukumu kutokana na wazazi au walezi na wahanga wa udhalilishaji  kukataa kwenda mahakamani kutoa ushahidi Mahakamani kwa kuhofia muhali utakao jitokeza baada ya hukumu.


Akielezea  Wilaya ya Kati amesema kwa sasa vitendo vya udhalilishaji vinavyoripotiwa  kwa wingi ni  kwa watoto wa kike wa miaka 14 hadi 17 kubakwa na kuingiliwa kinyume na maumbile  au kupewa ujauzito.


Akizitaja sababu zinazopelekea kuongezeka kwa vitendo vya udhalilishaji ni pamoja na  talaka ,watoto kushirikishwa katika mambo ya kikubwa , ubinafsi na watu kuenda kinyume na mafundisho ya dini zao.


Nae  mwenyekiti wa UWT Mkoa wa kusini Unguja Shemsa Abdallah Ali amewhimiza wazazi na walezi kurejesha malezi ya zamani kwa kuwalea watoto kwa mashirikiano kitu kitakachosaidia kuondosha vitendo hivi.


Wakati huo huo mgeni rasmi wa baraza hilo Semeni Khamis Vuai akifungua mkutano wa Baraza hilo amewataka wanachama wa  UWT wa jimbo la Tunguu kulipa ada ili waweze kuwa wanachama hai  na kufanikisha malengo ya Chama Cha Mapinduzi ya kupata ushindi katika chaguzi zijazo.


Aidha katibu wa Chama cha Mapinduzi  wa Jmbo hilo Sharifa  Maabadi  amewataka wanachama hao kujitokeza kwa wingi katika kuomba nafasi mbali mbali za uongozi kwa chaguzi za ndani zinazo tarajiwa kuanza ifikapo mwaka 2022.

Nao wajumbe wa Baraza hilo wameushukuru uongozi wa Jimbo hilo kwa kuwapatia elimu inayohusu vitendo vya udhalilishaji na kusema kuwa wapo tayari kumunga mkono Rais wa Zanzibar  Dkt Husein Ali Mwinyi katika harakati za kuondosha vitendo vya udhalilishaji hapa nchini.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.