Habari za Punde

Waziri Mhe Mhagama Afurahishwa Makubaliano Kati ya Kampuni ya ORYX na TUICO

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu)  Mhe. Jenista Mhagama akizungumza wakati wa hafla ya uwekaji saini mkataba wa hiari wa Hali bora baina ya Menejimenti ya Makampuni ya ORYX energies na Chama cha Wafanyakazi wa Viwandani, biashara, Taasisi za fedha, huduma na ushauri (TUICO) jijini Dar es Salaam.

NA. MWANDISHI WETU

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama amepongea hatua iliyochukuliwa na Kampuni ya ORYX Enegies na Chama cha Wafanyakazi wa Viwanda, Biashara, Taasisi za Fedha, Huduma na Ushauri (TUICO) ya kusaini Mkataba wa Hiari wa Hali Bora ili kuendelea kuboresha mazingira ya wafanyakazi ili kuleta tija katika nafasi zao.

 

Hafla hiyo iliyofanyika mwishoni mwa wiki na kuhudhuriwa na Katibu Mkuu wa TUICO Bw. Boniphace Nkakatisi, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Gesi ya ORYX,Benoit Aramari na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mafuta ya ORYX, Kalpesh Mehta na Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Waajiri (ATE), Dkt. Aggrey Mulimuka pamoja na wafanyakazi wa kampuni hizo Jijini Dar es Salaam.

Waziri alieleza kufurahishwa na makubaliano hayo kwa kubainisha faida zitakazopatikana kwa wafanyakazi ikiwemo kuongeza hali bora za wafanyakazi na kuongeza tija kwao.

“Ninafarijika sana kushuhudia waajiri wa Makampuni ya ORYX mnavyowajali wafanyakazi na kuchukua hatua kama hii ya utiaji saini wa mkataba wa hali bora bila ya kusukumwa na mtu yeyote hakika ninawapongeza sana,”alisema Waziri. 

Waziri alisema kuwa Makubaliano ya Mkataba wa Hali bora waliofikia ni hatua nzuri ya utekelezaji wa Sheria za kazi hususani Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini Na. 6 ya mwaka 2004 na Kanuni zake za mwaka 2007 (the Employment and Labour Relations Act No.6 of 2004 and the Code of Good Practice) Rule, 2007 (GN No. 42 ya tarehe 16TH Feb, 2007). Sheria hii na Kanuni zake zinaweka muongozo wa utaratibu na njia za kufuatwa na masuala muhimu ya kuzingatiwa katika kufanya majadiliano mahala pa kazi.

Aidha aliwaasa wafanyakazi kuendelea kutumia fursa hiyo kwa kufanya kazi kwa juhudi na ubunifu mkubwa ili kuwa na matokeo chanya katika kampuni hiyo.

“Wafanyakazi mtapata ziada ya vitu vingi msibweteke badala yake muwe na bidii na ushirikiano wa karibu ili tuendelee mbele badala ya kurudi nyuma,”alisisitiza

Naye Katibu Mkuu wa TUICO Bw. Boniphace Nkakatisi alieleza furaha yake kwa hatua hiyo na kuwaasa waajiri wengine kuona umuhimu wa kuwa na mikataba hii ili kuboresha utendaji kazi kwa wafanyakazi

“Tunapoingia mikataba kama hii inasaidia kuboresha vipengele mbalimbali vya kisheria na vinavyotokana na mazingira ya kazi na kuleta afya na ustawi kwa masuala haya,”alisema Nkakatisi

Aliongezea kuwa, makubaliano haya yanaleta hali ya kuaminiana, kupunguza manung’uniko kazini, kupunguza migogoro na kuendeleza umoja na mshikamano baina ya menejimenti na wafanyakazi.

Kwa Upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni za ORXY Bw. Benoit Aramari alishukuru Serikali kujali mazingira ya wawekezaji nchini na kuitumia nafasi hiyo kuendelea kuipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu yenye dhamana na masuala ya Kazi na Ajira nchini kwa kuona umuhimu wa kushuhudia makubaliano hayo na kuahidi kuendelea kushirikiana na kufanya kazi katika misingi na sheria za kazi zilizopo.

Akitoa neno la shukran Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) Dkt.Aggrey Mulimuka alipongeza Waziri kuona umuhimu na kushuhudia zoezi hilo kwa kuzingatia wingi wa majukumu aliyonayo.Alipongeza Menejimenti na Wafanyakazi kwa kutambua uwepo wa Chama cha Wafanyakazi na kuweka makubaliano haya yanayoashiria uhai wa kampuni na kusema hatua hiyo inafaa kuigwa na wengine.

Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) Dkt. Aggrey Mlimuka akizungumza wakati wa hafla uwekaji saini mkataba wa hiari wa Hali bora baina ya Menejimenti ya Makampuni ya ORYX energies na Chama cha Wafanyakazi wa Viwandani, biashara, Taasisi za fedha, huduma na ushauri (TUICO).
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama akikabidhi hati za makubaliano kwa uongozi wa makapuni ya ORYX Tanzania mara baada ya kusaini mkataba wa hiari wa Hali bora baina ya Menejimenti ya Makampuni ya ORYX enegies na Chama cha Wafanyakazi wa Viwandani, biashara, Taasisi za fedha, huduma na ushauri (TUICO).
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama pamoja Mkurugenzi wa ATE Dkt. Aggrey Mlimuka wakikabidhi hati za makubaliano kwa Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Viwandani, biashara, Taasisi za fedha, huduma na ushauri (TUICO) Bw. Boniphace Nkakatisi mara baada ya zoezi hilo.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) Dkt. Aggrey Mlimuka (kulia kwake), wakishuhudia hati za makubaliano hayo mara baada ya zoezi la uwekeji saini kukamilika wa kwanza kulia ni Katibu Mkuu wa TUICO, Boniphace Nkakatisi na wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi wa kampuni ya mafuta, Kalpesh Mehta na Mkurugenzi wa makampuni ya ORYX Tanzania Bw. Benoit Aramari (wa pili kutoka kushoto).
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama akiteta jambo na Mkurugenzi Mtendaji wa makampuni ya ORYX Bw. Benoit Aramaei wakati wa hafla hiyo.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama (katika) akiwa katika P9picha ya pamoja na wafanyakazi wa kampuni ya ORYX mara baada zoezi la kusaini hati za makubaliano kati yao na TUICO.

 (PICHA ZOTE NA OFISI YA WAZIRI MKUU)

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.