RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akiwa na mgeni
wake Waziri Mkuu Mstaafu wa Uingereza Mhe Tony Blair, wakizungumza na kuagana
baada ya kumaliza mazungumzo yao yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar.(Picha
na Ikulu)
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amempongeza Waziri Mkuu Mstaafu wa Uingereza
Tony Blair kwa kutekekeleza kwa vitendo ahadi zake za kuendelea kuiunga mkono
Zanzibar hasa katika mipango na mikakati ya upangaji wa vipaumbele kwa
watendaji wa Serikali.
Rais Dk. Mwinyi aliyasema hayo wakati alipofanya mazungumzo na Waziri Mkuu Mstaafu wa Uingereza Tony Blair Ikulu Zanzibar ambaye yupo Zanzibar kwa ziara maalum.
Katika maelezo yake Rais Dk. Mwinyi alisema
kuwa Waziri Mkuu Mstaafu Tony Blair kupitia taasisi yake ya (Tony Blair
Institute for Global Change), imeweza kuunga mkono jitihada za Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar ya kutoa mafunzo kwa watendaji wakuu juu ya upangaji wa
vipaumbele hatua ambayo ina umuhumu mkubwa katika mipango ya Serikali.
Alisema kuwa mafunzo hayo ambayo Taasisi hiyo
iliyatoa kwa watendaji wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yana mchango mkubwa katika mipango ya Serikali na utekelezaji
wake.
Aidha, Rais Dk, Mwinyi alimuhakikishia
kiongozi huyo kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuthamini michango
ya taasisi ya (Tony Blair Institute for Global Change), kwani imeonesha nia na
dhamira kubwa ya kuiunga mkono Zanzibar ili mipango yake ya maendeleo iweze
kufanikiwa ipasavyo.
Nae Waziri Mkuu Mstaafu wa Uingereza Tony
Blair Ikulu Zanzibar alimueleza Rais Dk. Mwinyi hatua zinazoendelea kuchukuliwa
na taasisi yake katika kuhakikisha malengo na mikakati ya kuiunga mkono
Zanzibar yanatekelezeka na kuzaa matunda.
Tony Blair alitumia fursa hiyo kumpongeza Rais
Dk. Mwinyi kwa juhudi zake anazozichukua katika kuhakikisha Zanzibar inapata
maendeleo endelevu huku akimuahidi kuwa taasisi yake itaendelea kumuunga mkono.
Sambamba na hayo, Waziri Mkuu huyo mstaafu
alimueleza Rais Dk. Mwinyi kwamba tayari taasisi yake imeshaweka mipango
kabambe katika kuhakikisha inatoa mchango mkubwa katika kuhakikisha mipango
iliyopangwa na Serikali anayoiongoza Rais Dk. Mwinyi inatekelezeka.
Tayari taasisi ya Waziri Mkuu Mstaafu wa
Uingereza Tony Blair (Tony Blair Institute for Global Change) imeshatoa mafunzo ya Upangaji wa Viapaumbele
kwa watendaji wakuu wa Serikali ya Mapiduzi ya Zanzibar wakiwemo Makatibu
Wakuu, Wakurugenzi, Maafisa Wadhamini
pamoja na watendaji wengine, mafunzo yaliyofanyika mnamo mwezi wa
Febuari mwaka huu huko katika ukumbi wa Chuo Cha Utalii Maruhubi, Zanzibar.
Imetayarishwa na Kitengo cha Habari,
Ikulu Zanzibar.
No comments:
Post a Comment