RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi
Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akiwa na Mkewe Mama Mariam Mwinyi akifungua mlango
kuashiria ufunguzi wa Kongamano la Wanawake Zanzibar na Mwenyekiti wa Bodi ya
Wakurugenzi wa Benki ya Biashara Tanzania Bw. Edmund Mndolwa (kushoto)
kongamano hilo lililofanyika katika ukumbi wa Golden Tulip Kiembesamaki Jijini
Zanzibar lililoandaliwa na Benki ya Biashara Tanzania (TCB).(Picha na Ikulu)
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Hussein Ali Mwinyi ameeleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea
kutoa ushirikiano unaohitajika na kujenga mazingira mazuri ili Benki ya
Biashara ya Tanzania (TCB) iendelee kutoa huduma kwa wananchi wa Zanzibar.
Rais Dk. Mwinyi
aliyasema hayo leo wakati akizindua Kongamano la Wanawake kuhusu Nafasi ya
Mwanamke katika Kukuza Uchumi wa Buluu, hafla iliyofanyika katika ukumbi wa
Hoteli ya Golden Tulip, iliyopo uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani
Karume, Zanzibar ambapo Mama Mariam Mwinyi nae alihudhuria.
Katika maelezo
yake Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa uwamuzi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania wa kuunganisha benki ndogo ndogo zilizokuwepo awali kwa lengo la
kuunda Benki ya TCB umelenga kuyanufaisha makundi mbali mbali ya
wafanyabiashara, wawekezaji, wajasiriamali na wananchi kwa jumla.
Hivyo Rais Dk.
Mwinyi aliihimiza Benki hiyo kufanya kazi kwa bidii na uzalendo ili malengo ya
Serikali ya kuianzisha na kuiimarisha benki hiyo yaweze kufikiwa kwa maslahi
mapana ya nchi.
Aliitaka benki
hiyo kuongeza juhudi za kuwa wabunifu ili Taasisi hiyo isiyumbe, iendelee kuwa
imara na yenye uwezo na nyenzo za kuhimili ushindani mkubwa uliopo ndani na nje
ya nchi katika sekta ya huduma ya fedha. “Kuweni mstari wa mbele katika mageuzi
ya kiuchumi yaliyopangwa na Serikali zetu katika pande mbili za Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania”,alisema Dk. Mwinyi.
Rais Dk. Mwinyi
alitoa wito kwa wananchi kushirikiana na taasisi za fedha pamoja na wawekezaji
wa ndani na nje katika juhudi za kuendeleza uchumi wa buluu na kuhimiza
kuzitumia kikamilifu fursa zinazotolewa na benki za hapa nchini.
Aidha, Rais Dk.
Mwinyi, alizihimiza Benki za hapa nchini kuendelea kushirikiana na
wajasiriamali kwa kuwapatia mikopo yenye unafuu wa riba na kuendela kuzisogeza
huduma za fedha karibu na maeneo yao ya kazi,kuwapatia mafunzo pamoja na
kuwapatia masoko.
Alieleza kuwa
uwamuzi wa benki hiyo wa kutoa elimu na kuhamasisha wanawake kushiriki katika
kutekeleza mipango inayohusu uchumi wa buluu ni muhimu ikizingatiwa kwamba
uchumi wa buluu umejumuisha sekta kadhaa zikiwemo uvuvi, utalii, usafiri wa
bahari, ujenzi wa bandari za kisasa, kilimo cha mwani, uchimbaji wa mafuta na
gesi na matumizi mengineyo ya rasiliamali za bahari kwa kuzingatia uhifadhi wa
mazingira.
Alisema kuwa Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini juhudi za kina mama katika kuendeleza zao
la mwani ambalo ni sehemu ya uchumi wa buluu, hivyo kupitia kongamano hilo
anaamini kwamba mipango na mikakati ya kuliendeleza zao hilo kwa matumizi ya
mbegu bora pamoja na mbinu za kuliongezea thamani na utafutaji wa masoko
itajadiliwa.
Aliongeza kuwa
Serikali itaendelea na jitihada za kuwapatia mitaji, vifaa na masoko
wazalishaji wa mwani wa Unguja na Pemba kwani imeweka mkazo maalum wa kuyapatia
mikopo makundi mbali mbali ya wanawake wanaojishughulisha na uzalishaji mwani
na shughuli nyengine za biashara.
Rais Dk. Mwinyi
alieleza kuvutiwa kwake na uwamuzi na utaratibu wa Benki ya Biashara Tanzania
wa kuweka mkakati maalum wa kuandaa na kuendesha makongamano malaum ya wanawake
kwa ajili ya kujadili masuala muhimu yanayohusu maendeleo ya wanawake kwa lengo
la kustawisha ustawi wa wanawake nchini.
Nae Waziri wa Afya,
Ustawi wa Jamii, Wazee, Jinsia na Watoto Nassor Ahmed Mazrui alitoa pongezi
zake kwa Rais Dk. Mwinyi kwa juhudi zake za kuwakomboa wananchi kiuchumi na
kusisitiza kwamba hatua zake hizo zitaendelea kuungwa mkono kwani ana nia njema
ya kuwasaidia wananchi wake.
Mwenyekiti wa
Bodi ya Benki hiyo Dk. Edmund Mndolwa alieleza kwamba licha ya changamoto
kadhaa inazozipata Benki hiyo lakini hata hivyo imeweza kupata mafanikio
makubwa na kueleza matumaini yake kwamba benki hiyo ndani ya miaka mitano
itakuwa ni beni ya mfano hapa nchini.
Mkurugenzi Mkuu
wa Benki ya Biashara Tanzania (TCB),
Sabasaba Moshingi alieleza matumaini yake makubwa ya maendeleo
yatakayofikiwa na Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk. Mwinyi.
Alisema kuwa
Benki hiyo ya Biashara (TCB) ni Benki kongwe ambayo ina miaka 97 tokea
kuanzishwa kwake na ambayo inamilikiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania kwa asilimia 83, Shirika la Posta Tanzania asilimi 8, Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar asilimia 3, Posta na Simu asilimia 3 na Mfuko wa Hifadhi
wa Jamii kwa watumishi wa Umma asilimia 2.
Katika hafla
hiyo Rais Dk. Mwinyi alitoa zawadi mbali mbali kwa wateja wa benki hiyo
vikiwemo vikundi vya wajasiriamali, Taasisi ya Maisha Bora ‘Zanzibar Maisha Bora Foundation’ pamoja na
kukabidhiwa kadi yake ya uwanachama wa benki hiyo.
Mapema Rais Dk.
Mwinyi alipata fursa ya kukagua bidhaa mbali mbali za Wajasiriamali waliokuwepo
hotelini hapo katika hafla hiyo.
Imetayarishwa na Kitengo cha Habari
Ikulu Zanzibar.
No comments:
Post a Comment