Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein
Ali Mwinyi amempongeza Profesa Abdulrazak Gurnah, Mshindi wa Tuzo ya Nobel ya
Fasihi ya mwaka 2021 kwa kuipa heshima
kubwa Zanzibar Kimataifa.
Rais Dk.
Mwinyi aliyasema hayo leo wakati alipofanya mazungumzo na Profesa Abdulrazak
Gurnah, Mshindi wa Tuzo ya Nobel ya Fasihi ya mwaka 2021 ambae alifika Ikulu Zanzibar,
kufuatia mwaliko wa Rais Dk. Mwinyi.
Katika maelezo
yake, Rais Dk. Mwinyi alimueleza mshindi huyo wa Tuzo ya Nobel ya Fasihi ya
mwaka 2021 kwamba Zanzibar inajivunia na kuona fakhari kutoa mtu aliyefanikiwa
kwa kupata Tuzo hiyo ambayo ni kubwa duniani.
Aidha, Rais
Dk. Mwinyi alimpongeza Profesa Gurnah kwa utayari wake wa kufanya kazi na
kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika mambo mbali mbali ya
kimaendeleo ikiwemo maonesho ya vitabu.
Rais Dk.
Mwinyi pia, alitumia fursa hiyo kumkaribisha nyumbani Mshindi huyo wa Tuzo ya
Nobel ya Fasihi ya mwaka 2021 na kumpongeza kwa mafanikio hayo aliyoyapata
ambayo yameitangaza Zanzibar.
Pamoja na
hayo, Rais Dk. Mwinyi alisisitiza kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko
tayari kufanya kazi na mtu yeyote mwenye azma ya kuitangaza Zanzibar.
Rais Dk.
Mwinyi pia, alieleza kwamba kwa vile Zanzibar ni nchi ya Kitalii na kwa vile nchi
nyingi hivi sasa zimekuwa zikiyatumia matamasha katika kujitangaza hivyo, ipo
fursa ya kujifunza kutokana na matamasha hayo na kueleza kwamba tamasha la
vitabu ambalo Mshindi huyo ameahidi kuliunga mkono, litasaidia zaidi kuitangaza
Zanzibar.
Mapema Profesa
Abdulrazak Gurnah, Mshindi wa Tuzo ya Nobel ya Fasihi ya mwaka 2021alimpongeza
Rais Dk. Mwinyi kwa kumpa mwaliko huo wa kuja kumuona ambapo mwaliko huo
aliutoa Rais Dk. Mwinyi siku aliyompongeza Mshindi huyo kwa kumpigia simu mara
tu baada ya kutangazwa kupewa Tuzo hiyo.
Hivyo, katika
mazungumzo hayo, Profesa Abdulrazak Gurnah, Mshindi wa Tuzo ya Nobel ya Fasihi
2021 alimuhakikishia Rais Dk. Mwinyi utayari wake wa kushirikiana na Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar katika mambo mbali mbali ya kimaendeleo.
Alitumia fursa
hiyo kutoa shukurani kwa ukaribisho alioupata kutoka kwa Serikali, ndugu, jamaa
na marafiki pamoja na makaribisho aliyoyapata kutoka kwa uongozi ZATO na FESTAC
Africa 2022, Tamasha la Sanaa na Utamaduni wa Muafrika linalofanyika hapa Zanzibar
katika Hoteli ya Verde iliyopo Mtoni.
Aidha, Profesa
Abdulrazak Gurnah, Mshindi wa Tuzo ya Nobel ya Fasihi ya mwaka 2021 alieleza
nia yake kwa Rais Dk. Mwinyi ya kushirikiana na watu wengine hapa nchini katika
Tuzo mbali mbali ambazo zitakuwa zikitolewa kila baada ya muda ikiwa ni pamoja
na kushirikiana na Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).
Nao uongozi wa
Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale, ulieleza kufarajika kwa ujio wa Mshindi huyo
pamoja na ahadi zake mbali mbali alizoahidi katika kuutangaza utalii wa
Zanzibar ikwia ni pamoja na kuyatumia makumbushi ya Zanzibar kwa ajili ya
kuweka vitu na nakala zake mbali mbali.
Profesa
Abdulrazak Gurnah, Mshindi wa Tuzo ya Nobel ya Fasihi ya mwaka 2021 alizaliwa
mnamo mwaka 1948 na kukulia Zanzibar na hatimae kuelekea Uingereza akiwa kijana
kwa ajili ya masomo mwishoni mwa miaka ya 1960, Mwandishi huyu wa Tunzo hiyo ya
Nobel ya Fasihi alikuwa Profesa wa Kiingereza katika Fasihi kwenye Chuo Kikuu
cha Kent huko Ceterburry nchini Uingereza hadi alivyostaafu hivi karibuni.
Mnamo Alhamis
ya tarehe 07 Oktoba mwaka 2021 kituo kinachotoa tuzo kilimtangaza Profesa
Abdulrazak Gurnah kuwa mshindi wa Tuzo ya Nobel ya Fasihi na kumpongeza kwa
kuangazia suala la ukoloni na athari zake katika utunzi wake.
Tuzo hiyo
inayotolewa na kituo hicho cha Sweden ina thamani ya corona milioni kumi za
taifa hilo sawa na dola za Kimarekani milioni 1.4.
Mwandishi huyu
wa riwaya, kazi yake ya kwanza aliandika akiwa na umri wa miaka 21 huko nchini Uingereza
ambapo ndie mwandishi wa kwanza Mtanzania kushinda Tuzo ya Nobel ya Fasihi na
wa pili barani Afrika baada ya mwandishi wa vitabu Wole Soyinka kutoa nchini
Nigeria.
Tunzo za Nobel
ambazo zimetunzwa tangu mwaka 1901, zinatambua ufanisi katika fasihi sayansi,
amani na uchumi ambapo washindi wa awali wamekuwa wakiwashirikisha waandishi wa
Riyawa kama vile Emest Hemingway, Gabriel Garcia Marquez na Toni Morrison,
washairi kama vile Pablo Neruda, Joseph Brodsky na Rabindranath Tagore na
waandishi wa michezo ya kuigiza akiwemo Harold Pinter na Eugene O’Neill.
Imetayarishwa na Idara ya Mawasiliano,
Ikulu Zanzibar.
OF
RESPONSIBILITY
No comments:
Post a Comment