Habari za Punde

Kamati ya Bunge Yapokea Taarifa ya Ofisi ya Makamu wa Rais

 

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis akifafanua jambo wakati wa kikao cha kuwasilisha na kupokea taarifa ya utekelezaji wa Mpango-kazi wa Taifa wa kupunguza matumizi ya Zebaki kwa wachimbaji wadogo wa dhahabu (2020 - 2025) mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira jijini Dodoma 

Watalaamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais wakiwa katika kikao cha kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango-kazi wa Taifa wa kupunguza matumizi ya Zebaki kwa wachimbaji wadogo wa dhahabu (2020 - 2025) mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira jijini Dodoma leo Septemba 08, 2022.

                                     (PICHA NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS)

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis amesema Serikali imeendelea kutekeleza mradi wa kufanya utafiti kuhusu teknolojia mbadala wa Zebaki.

Amesema hayo leo Septemba 08, 2022 wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango-kazi wa Taifa wa kupunguza matumizi ya Zebaki kwa wachimbaji wadogo wa dhahabu (2020 - 2025) mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira jijini Dodoma.

Mhe. Khamis mradi huo unatekelezwa kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais, Baraza la Taifa la Hifadhi la Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na Wizara ya Madini na Tume ya Madini.

Alisema kazi zilizofanyika ni kufanya tathmini ya teknolojia zilizopo ambazo zinatumika katika shughuli za wachimbaji wadogo wa dhahabu na kubaini teknolojia mbadala zilizopo ambazo hazijafanyiwa utafiti kuhusu ufanisi kulingana na maeneo ya kijiolojia, gharama zake na uwezo wa kukamatisha dhahabu kulingana na miamba ya eneo husika.

Akijibu hoja za wabunge alisema Serikali itaendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu Zebaki ili kukabiliana na changamoto za kemikali hiyo ili kulinda mazingira na afya za wananchi.

Naibu Waziri Khamis aliongeza kuwa Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na wadau inaendelea kuhamasisha matumizi ya teknolojia mbadala zisizotumia zebaki zinazoendelea kufanyiwa utafiti hapa nchini.

“Ni kweli Zebaki ina athari kubwa hasa inapochanganyika na maji na watu wanakwenda kuyatumia na nikuahidi mheshimiwa mwenyekiti hili tutalifanyia utafiti zaidi lakini pia tunaendelea kutoa elimu kuhusu teknolojia mbadala wa zebaki za gharama nafuu, rahisi kutumiwa, zinazoweza kutengenezwa hapa nchini na zenye ubora,” alisema.

Pia, naibu waziri huyo alisema utekelezaji wa Mpango-Kazi huu utachangia katika juhudi za taifa za kufikia malengo ya maendeleo endelevu hususan kupunguza umaskini, hifadhi ya mazingira na kulinda afya ya binadamu.

Alitoa wito kwa wadau wote muhimu hususan wizara za kisekta, taasisi, sekta binafsi, washirika wa maendeleo, asasi zisizo za kiserikali, vikundi vya wachimbaji wadogo na wanahabari kushiriki kikamilifu katika kutekeleza Mpango-Kazi huu.

Hata hivyo, alisema ongezeko la idadi ya wachimbaji wadogo wa dhahabu na uzalishaji wa dhahabu vinaashiria ongezeko la matumizi ya zebaki nchini hivyo, kutokana na hali hiyo, Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali ambayo ina jukumu la kusimamia uingizaji na matumizi ya zebaki nchini iliendesha zoezi la kufuatilia na kupata taarifa za awali juu ya uingizaji, usambazaji na matumizi ya zebaki nchini.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.