Habari za Punde

Kizimkazi Mkunguni wapongezwa kwa jitihada za kujitafutia maendeleo

 

MKUU wa Wilaya ya Kusini Rajab Yussuf Mkasaba amewapongeza wananchi wa kijiji cha Kizimkazi Mkunguni  kwa jitihada zao za  kujitafutia maendeleo na kukuza kipato chao kupitia sekta ya uvuvi.

 Mkuu huyo wa Wilaya ametoa pongezi hizo huko Kizimkazi Mkunguni wakati alipokuwa akizungumza na wananchi wa kijiji hicho  katika hafla ya uzinduzi wa uvunaji wa pweza ambapo wananchi hao walirimbika kwa muda wa miezi mitatu.

 Alisema kuwa kusimamia urimbikaji wa pweza unahitaji ujasiri  mkubwa kwani kuna baadhi ya  wasio waaminifu  huharibu kwa makusudi  taratibu zinazowekwa  na kuingia baharini  kuiba pweza waliorimbikwa.

Hivyo, alitumia fursa hiyo kuwapongeza na kuwashukuru wananchi wa kijiji cha kizimkazi Mkunguni kwa ustahamilivu wao mkubwa kwa kipindi chote hicho cha miezi mitatu kufanya zoezi hilo bila ya kujitokeza ukorofi wa aina yoyote juu urimbikaji huo.

 Alieleza kwamba mashirikiano hayo ndiyo yanayohitajika miongoni mwa jamii kwani ndio sababu kuu ya kuendeleza umoja na mshikamano sambamba na kudumisha amani na usalama katika jamii.

 Aliongeza kuwa pale panapojitokeza wananchi wakorofi na kutofuata matakwa ya makubaliano juu ya zoezi hilo wakati mwengine hupelekea kujitokea viashiria vya uvunjaji wa amani jambo ambalo halipewi nafasi katika Wilaya hiyo.

 Kutokana na mafanikio hayo, Mkasaba aliwaeleza wananchi hao kwamba Ofisi ya Wilaya hiyo imeamua kwa makusudi kwamba hivi sasa suala zima la urimbikaji wa pweza katika ukanda huo lisimamiwe na Wilaya kwa lengo la kufuata taratibu na miongozo inayotolewa na vijiji husika kupitia Kamati zao juu ya urimbikaji sambamba na uvunaji wa pweza.

 Alieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kuondoa migogoro inayotokea kati ya kijiji na kijiji katika zoezi zima la kurimbika na kurimbua pweza.

 Kwa upande wake Diwani wa Wadi ya Muyuni  Mustafa Haji  amesema kuwa mashirikiano mazuri  kati ya wananchi na Kamati ya uvuvi ya kijiji hicho ndio iliyopelekea kufanikisha zoezi hilo na kwa kiasi kikubwa  imeonesha kufanikiwa kuwafunga pweza na hatimae kuwavuna kwa wingi na wananchi kujiingizia kipato ili kuweza kujikimu kimaisha.

 Nao wananchi wa kijiji hicho cha Kizimkazi Mkunguni kwa upande wao walitoa shukurani na pongezi kwa Mkuu huyo wa Wilaya kwa mashirikiano mazuri anayowapa kwani amekuwa mstari wa mbele kushirikiana nao katika jitihada zao za kujiletea maendeleo endelevu katika kijiji chao.

 Wananchi hao waliahidi kuendelea kumuunga mkono Mkuu wa Wilaya huyo pamoja na uongozi wote wa Wilaya hiyo huku wakiwataka wananchi wa kijiji hicho kuendeleza umoja na mshikamano walionao katika shughuli zao mbali mbali za maendeleo zikiwemo hatua hizo za kuimarisha uchumi wa buluu.

 

Imetayarishwa na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kusini,

Mkoa wa Kusini Unguja.

26.10.2022.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.