Na Khadija Khamis –Maelezo Zanzibar 26/02/2023/
Ugonjwa la Kisukari ni miongoni mwa Magonjwa yanayoathiri jamii kwa kiwango kikubwa na yamekuwa yakiongezeka kwa kasi hapa nchini na hupelekea vifo na ulemavu wa viungo
Akifungua Mkutano Mkuu wa Jumuiya ya Watu Wanaishi na Kisukari Zanzibar huko katika ukumbi wa Skuli ya Ben-Bella Katibu Mkuu Wizara ya Maji Nishati na Madini Joseph Kilangi kwa Niaba ya Naibu Wazara wa Maji Nishati na Madini Shaaban Ali Othman amesema
mwaka 2019 watu milioni kumi na tisa Barani Afrika wanaishi na ugonjwa wa kisukari kati ya umri wa miaka 20 hadi 70 ambapo kwa hapa Zanzibar ripoti inaonyesha kuwa watu 4 kati ya watu mia 100 huugua ugonjwa huo .
Amesema ongezeko hilo linaendelea kukuwa siku hadi siku jambo ambalo huko nyuma halikuwepo na limekuwa ni changamoto katika taifa kutokana na kuutwika mzigo mkubwa Seriikali.
Aidha amefahamisha kuwa kundi la watu wanaishi na kisukari liko katika hatari zaidi kwa kushambuliwa na maradhi mengine hivyo ameitaka jamii kuzingatia lishe bora, kufanya mazoezi kuachana na tabia za matumizi ya pombe ya kupitiliza na sigara pamoja na kujiepusha na msongo wa mawazo ambayo hupelekea kupata ugonjwa huo.
Alifahamisha kuwa elimu bado inahitajika kwa jamii ya kupambana na vichocheo vya maradhi hayo pamoja na kuwa na utamaduni wa kupima afya mara kwa mara ili kuipunguzia mzigo mkubwa serikali kutibu ugonjwa huo kwa kutumia fedha nyingi kwa matibabu fedha ambazo zingelitumika kwa mambo mengine
Nao Katibu wa Jumuia ya Watu Wanaishi na Kisukari Zanzibar (DAZ) Omar Abdalla Ali na Mjumbe wa Bodi ya Watu Wanaishi na Kisukari Dk Faiza Kassim wamesema Serikali ni vyema kuzidi kupambana na suala la dawa na shindano kwa wanaoishi na kisukari.
Aidha wamesema kuwa ni vyema kwa jamii kujikinga na visababishi vya maradhi hayo na kuwataka kufanya uchunguzi wa mara kwa mara ili kuweza kujigundua mapema na kupata huduma stahiki
Mapema akisoma Risala ya Jumuiya wa Watu Wanaishi na Kisukari Zanzibar(DAZ) ambae ni Mwenyekiti wa Vijana wa Jumuia ya Watu Wanaishi na Kisukari Bi Nunuu Kheir Saleh amesema ugonjwa wa kisukari unawapata hasa watu wazima, wajawazito na watoto ambapo kisukari cha utotoni imeonekana kuongezeka na kushika kasi na husababisha madhara na mzigo mkubwa kiuchumi kwa serikali na watu binafsi.
amesema miongoni mwa dalili kubwa za ungonjwa huo ni kunywa maji mengi kuliko kawaida na kusikia kiu kila wakati, kwenda haja ndogo mara kwa mara, kusikia njaa kila wakati, kupata ganzi hasa sehemu ya miguu viganja vya mikono na vidole, pamoja na vidonda vya miguu vinavochelewa kupona.
Nae Mwanachama Omar Ahmada Ali ameiyomba Jumuiya hiyo kuwapa msaada wa mahitaji ya lazima kwa wale wanachama mwenye hali ngumu za maisha
Akitoa neno la shukrani Mrajis wa Jumuiya zisizo za kiserikali Bw Ahmed Gharib Abdalla ameipongeza jumuia hiyo kwa kufanya kazi za kupambana na ugonjwa wa kisukari pamoja na kutoa elimu kwa jamii .
Amesema kuwa ni vyema kwa Jumuiya zinazoanzishwa ziwe na malengo ya kuisaidia serikali ili kuipunguzia mzigo na lengo liweze kufanikiwa
No comments:
Post a Comment