Habari za Punde

Vifaa vya Ujenzi wa Barabara vya Kampuni ya CCECC Vyawasili

Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi Zanzibar Dk. Khalid Salum Mohamed, akiwa na Viongozi wa Kampuni ya Ujenzi ya CCECC, akikagua vifaa vya kampuni hiyo katika bandari ya Malindi Zanzibar,wakati wa ushushaji wa vifaa hivyo vya Ujenzi wa barabara za mjini kupitia Kampuni ya CCECC.

Na.Kassim Abdil -WUMU.

Wizara ya Ujenzi,Mawasiliano na Uchukuzi itahakikisha inasimamia kwa karibu na kutoa ushirikiano kwa Kampuni zilizopewa kazi ya Ujenzi wa barabara wanakamilisha kazi hiyo kwa wakati uliopangwa.

Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi Zanzibar Dk. Khalid Salum Mohamed ameeleza hayo leo wakati akikagua zoezi la ushushaji wa vifaa vya Ujenzi wa barabara za mjini kupitia Kampuni ya CCECC.

 

Waziri Dk. Khalid ameshuhudia zoezi hilo katika Bandari ya Malindi ambapo meli iliobeba vifaa hivyo imewasili Zanzibar na imepata nafasi ya kufunga nanga kwa ajili ya kazi ya ushishaji wa vifaa.

 

Mhe. Waziri akiwa pamoja na viongozi wengine wamepata fursa ya kuvikagua vifaa vya ujenzi vilivyowasili ikiwemo magari makubwa Ishirini, rola nane, skaveta pamoja na vifaa vyengine kwa ajili ya ujenzi wa barabara za mjini zenye urefu wa 100.9 km.

 

Waziri Dk. Khalid amesema kutokana na uharaka wa kazi ya ujenzi wa barabara Wizara itahakikisha vifaa hivyo vinashushwa kwa haraka hadi wakati wa usiku.

 

Amesema kazi ya ujenzi wa barabara za Mjini tayari imeanza na jumla ya barabara kadhaa zimeanza kujengwa ikiwemo barabara ya Uwanja wa Ndege- Mnazi mmoja, Barabara ya Chukwani - Buyu, na Barabara za Mwanakwerewke.

 

Amesema kuwasili kwa vifaa hivyo kutaiwezasha kampuni hiyo ya CCECC kujenga barabara nane kwa wakati mmoja.

 

Pia, Mhe. Waziri amesema Wizara imepanga mpango maalum wa kuhakikisha barabara za ndani zenye urefu wa Km 275.9 zinaendelea kujenga Ungaja na Pemba ambapo wameitaka kampuni iliopewa kazi hiyo kujigawa katika makundi matatu.

 

"Katika kuhakikisha kazi ya ujenzi wa Barabara inakwenda kwa haraka tumeigaiza Kampuni ya ARIS ASER kujigawa katika makundi matatu ambpo moja litakua kaskazini Unguja, Kundi la Pili litakua Kusini Unguja na kundi jengine liendelee na kazi kwa upande wa Pemba.

 

Waziri Dk. Khalid ameeleza kuwa, kazi ya Ujenzi wa Barabara kwa upande wa Pemba imekwisha anza ambapo Kampuni hiyo inaendelea na kazi ya kusafisha eneo la barabara ya Finya-Kicha.

 

Mhe. Waziri amesema mbali na vifaa hivyo lakini meli nyengine ipo njiani na kukamilisha jumla ya vifaa Mia moja na nne (104) kwa ajili ya ujenzi wa barabara za Mjini.

 

…………………………

Kassim Abdi.

Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi Zanzibar.

28/05/2023.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.