Habari za Punde

Wanafunzi 284 wenye mazingira magumu wapatiwa sare za skuli Bambi

Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Rashid Hadid Rashid akimkabidhi sare ya Skuli miongoni mwa mwanafunzi ikiwa ni sadaka  kutoka kwa kamisheni ya wakfu na Mali ya Amana

Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Rashid Hadid Rashid akimkabidhi sare ya Skuli mwanafunzi Mwanaisha Saidi ikiwa ni sadaka  kutoka kwa kamisheni ya wakfu na Mali ya Amana.

 

Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Rashid Hadid Rashid,Mkuu wa Wilaya ya Kati Marina Tomas wakiwa katika picha ya pamoja wanafunzi wa Skuli ya Bambi baada ya makabidhiano ya Sare za Skuli kwa wanafunzi wanaoishi katika mazingira magumu.

Msanii wa Tungo za  Mashairi Kassim yussuf (ziro kasorobo) akighani utenzi katika hafla ya ugavi wa sare za skuli kwa wanafunzi wanaoishi katika mazingira magumu huko Bambi Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja. 
Katibu Mtendaji Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana Alhaaj Abdalla Talib akizungumza machache na kumkaribisha mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Rashid hadid Rashid kuendesha zoezi la ugawaji wa Sare Kwa wanafunzi wanaoishi katika mazingira magumu huko  Skuli ya Bambi Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja.
 

Mwalimu Mkuuu Skuli ya Msingi Bambi Muhammed Ramadhan Mapuri akitoa neno la shukrani kwa niaba ya wazazi na wanafunzi wa Skuli hiyo kufuatia msaada wa Sare za Skuli uliotolewa na  kamisheni ya wakfu na Mali ya Amana.

 

Na Fauzia Mussa,    Maelezo

Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Rashid Hadid Rashid amewataka wazazi kuunga mkono juhudi zinazochukuliwa  katika kuimarisha upatikanaji wa elimu na kuhakikisha wanafunzi wanakuwa na mazingira bora ya kujisomea.

 

Akizungumza wakati wa ugawaji wa Sare za Skuli kwa wanafunzi wanaoishi katika  mazingira magumu huko Bambi Wilaya ya Kati Mkoa wa kusini Unguja, Mkuu huyo amesema kufanya hivyo kutasaidia  wanafunzi kutimiza ndoto zao walizozitarajia.

 

Alisema  hatua iliyochukuliwa na Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana ya kuekeza katika sekta ya elimu ni yakupongezwa kwani kutasaidia kuwaweka wanafunzi katika mazingira rafiki ya kujisomea .

“ Kuna baadhi ya wanafunzi wanawacha kwenda skuli kutokana na  kukosa mazingira rafiki ya kujisomea ikiwemo kuchanika kwa sare zao  hivyo sadaka hiyo itaendea kutimiza ndoto za wanafunzi  hao”,alieleza Mkuu huyo.

 

Mkuu wa Mkoa aliwataka wazazi na walezi  kuzitunza na kuzitumia vizuri sare hizo ili kufikia lengo lililokusudiwa  pamoja na kuwaomba  wadau na wahisani kuwekeza katika sekta ya  elimu kwani  elimu ni sadaka inayoendelea.

 

“Sio mnachukua sare mnaenda kuchungia kwa sababu tu ni za msaada ni wajibu  kuthamini juhudi hizi zinazochukuliwa na wenzetu za kuhakikisha watoto wetu wanasoma katika mazingira rafiki”, alisistiza Mkuu huyo.

 

Mapema Mkuu wa Wilaya ya Kati Marina Tomas  aliwataka wazazi kuacha kuwapa wanafunzi majukumu yasiowahusu na badala yake kuwapatia muda wa ziada kuweza kupitia masomo yao.

 

Aliwasisitiza  walimu kujitahidi kuwasimamia na kuwasomesha vizuri  wanafunzi ili kuhakikisha ongezeko la ufaulu linakuwa katika  Wilaya hiyo na kutimiza ndoto zao walizotarajia.

 

Kwa upande wake Katibu Mtendaji Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana Alhaj Abdalla Talib  Abdalla amesema Kamisheni ina jukumu la kusimamia haki pamoja  na ugawaji wa sadaka na zaka kwa wanaostahi hivyo imeamua kutoa sadaka ya sare za skuli kwa wanafunzi wanaoishi katika mazingira magumu ili wapate kufarijika na kusoma vizuri kama wanafunzi wengine.

 

Hata hivyo aliwaomba  wananchi kutoa sehemu katika  mali zao na kuwapa wanaostahiki kwa kutaraji malipo kutoka kwa Allah.

 

Akitoa neno la shukurani Mwalimu Mkuuu Skuli ya Msingi Bambi Muhammed Ramadhan Mapuri amesema sare ni nyenzo muhimu miongoni mwa nyenzo za kujifuniza hivyo sadaka hiyo ni faraja kubwa  kwa wanafunzi na itapelekea kujiamini katika masomo yao.

 

Hata hivyo aliwataka wadau wa elimu na wenye uwezo kujitokeza kusaidia wanafunzi hao katika mambo mbalimbali ya kuwajengea mazingira rafiki ya kujisomea ikiwemo kufanyiwa  ukarabati wa skuli  pamoja  na  kupatiwa vikalio.

 

Jumla ya wanafunzi 284  wenye mazingira magumu wa msingi na Sekondari katika Skuli ya Bambi wamepatiwa sare za skuli kutoka kwa Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana Zanzibar .

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.