Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk.Hussein Mwinyi Amejumuika na Wananchi wa Mbweni Katika Ibada ya Sala ya Ijumaa Masjid Quba Mbweni Zanzibar

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk.Hussein Ali Mwinyi akisalimiana na Viongozi wa Masjid Quba Mbweni Wilaya ya Magharibi “B” Unguja Jijini Zanzibar, alipowasili katika viwanja vya msikiti huo kwa ajili ya Ibada ya Sala ya Ijumaa iliyofanyika leo 10-5-2024.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na kuwasalimia Wananchi baada ya kumalizika kwa Ibada ya Sala ya Ijumaa iliyofanyika leo 10-5-2024, katika ,Masjid Quba Mbweni Wilaya ya Magharibi “B” Unguja Jijini Zanzibar.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk.Hussein Ali Mwinyi akijumuika na Waumini wa Kiislam katika kuitikia dua ikisomwa na Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh.Saleh Omar Kabi, baada ya kumalizika kwa Ibada ya Sala ya Ijumaa iliyofanyika katika Masjid Quba Mbweni Wilaya ya Magharibi “B” Unguja Jijini Zanzibar leo 10-5-2024.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi ameahidi kuchangia nguvu za uendeshaji wa Masjid Quba ili kuongeza ari na hamasa kwa viongozi na waumini wanaoutumia msikiti huo.

Alhaji Rais Dk. Mwinyi amesifu uongozi wa msikiti huo kwa weledi wao wa kutoa taaluma bure kwa vijana na waumini wa dini ya kiislamu na kuwaahidi kuwaongezea nguvu za mahitaji ya msikiti huo.

Al hajj Dk. Mwinyi alitoa ahadi hiyo mara baada ya ibada ya sala ya Ijumaa msikitini hapo, Mbweni Mkoa wa Mjini Magharibi.

“Maadam na mimi mmenieleza haya mnayoyafanya basi na mimi nitakuchangieni ili tuzidi kuliendesha gurudumu hili” Aliahidi  Al hajj Dk. Mwinyi.

Akizungumzia suala la kuwaombea dua viongozi wa Serikali, Al hajj Dk. Mwinyi amewasihi waumini na viongozi wa msikiti huo wasichoke kuwaombea dua viongozi wa nchi ili Mwenyezi Mungu azidi kuwapa wepesi wa kutekeleza na kuzikamilisha ahadi walizoziahidi kwa wananchi.

Al hajj Dk. Mwinyi alisema, ahadi nyingi tayari zimetekelezwa na kukamilishwa kwa wakati lakini bado zipo nyingi pia zinahitaji kukamilishwa kwa mafanikio makubwa na kueleza maombi mema kutoka kwa wananchi kwenda kwa viongozi wao, bado yanahitajika katika kufika malengo ya nchi iliyojiwekea na kufanyakazi kwa uadilifu.

Mapema, akizungumza kwenye ibada hiyo ya sala ya Ijumaa msikitini hapo, Katibu Mtendaji kutoka Ofisi ya Mufti Zanzibar, Sheikh Khalid Ali Mfaume alisifu juhudi za Alhaj Dk. Mwinyi kwa uweledi wake wa kushirikiana na wananchi na waumini wa dini ya kiislamu kwenye ibada ya sala ya Ijumaa kwa maeneo mbalimbali nchini kutokana na dhamira na nia yake njema kwa watu wa Zanzibar.

Alisema, uongozi wa Al hajj Dk. Mwinyi ni juhudi zake za kuwafikia wa watu wote pamoja na hudumia kwani ni kiongozi wa wote.

Akitoa hutba kabla ya sala ya Ijumaa, Khatib wa sala hiyo Sheikh, Ali Masoud amewasihi waumini wa dini ya Kiislam kuwaombea mema na kuwatii viongozi wa nchi, kwani kufanya hivyo ni kulitakia heri na baraka taifa na watu wake.

Mara baada ya ibada ya Sala hiyo ya Ijumaa, Al hajj Dk. Mwinyi aliwatembelea wazee, akiwemo Mbunge wa zamani wa Chama Cha  Mapinduzi (CCM), jimbo la Amani, Mzee Hassan Rajab, nyumbani kwake Kisauni “Wilaya ya Magharibi B” na Mjumbe wa Baraza la Wazee kupitia Chama Cha CCM Kisiwandui, bibi Maryam Hengwa nyumbani kwake Kwa Mchina, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Al hajj Dk. Mwinyi amekua na utaratibu wa jukumuika pamoja na wananchi na waumini wa dini ya Kiislam kwenye ibada ya sala ya Ijumaa kwa maeneo mbalimbali ya visiwa vya Zanzibar  kwa kufanikiwa kusali zaidi ya misikiti 170 ndani ya kipindi cha miaka mitatu ya uongozi wake, pia Alhajj Dk. Mwinyi amefungua misikiti mipya zaidi ya 30 kwa maeneo mbalimbali ya Unguja na Pemba pamoja na kuwatembelea wananchi, wazee na wagonjwa hospitalini.

IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.