Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Temeke (TRRH), Dkt.Joseph Kimaro, ameeleza kuwa hospitali inaendelea kuboresha huduma zake na kusema uanzishwaji wa huduma ya usafishaji damu (dialysis) hospitalini hapo, ni huduma muhimu sana kwa eneo la Temeke. amefafanua kuwa hospitali hiyo inahudumia wilaya tatu: Kigamboni, Temeke, na Mkuranga, na ni hospitali pekee ya serikali katika eneo hilo inayotoa huduma ya usafishaji damu.
Dkt. Kimaro pia ameeleza kuwa katika kipindi cha mwaka mmoja na nusu, hospitali hiyo imefanikisha upatikanaji wa dawa kwa asilimia 98 kwa bidhaa 500. Mafanikio haya yanatokana na jitihada kubwa za timu ya uendeshaji wa huduma za afya(RRHMT) hospitalini hapo, ambapo asilimia 80 ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba unafanywa na fedha za uchangiaji wa huduma.
Dkt. Kimaro ametoa shukrani zake kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa uliofanywa katika hospitali za Tanzania, hususan Temeke, kupitia vifaa tiba vya kisasa na wataalamu wa mionzi. Pia amemshukuru Waziri wa Afya, Mhe. Ummy Mwalimu kwa kusimamia wizara na watumishi wake, na kuhakikisha miongozo na sera za wizara zinafuatwa ipasavyo.
No comments:
Post a Comment