Habari za Punde

Risala ya Wafanyakazi Maadhimisho ya May Day



Mh. Mgeni rasmi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa baraza la Mapinduzi
Dr. Ali Mohammed Shein

Nd. Mwenyekiti wa ZATUC
Nd. Zahran Muhammed Nassor

Nd. Waziri wa Kazi, Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi na Ushirika
Nd. Haroun Ali Suleiman

Mkurugenzi wa Jumuiya ya Waajiri ZANEMA

Nd. Salahi Salim Salahi

Mwakilishi wa ILO Zanzibar

Bibi. Fatma Mohammed Rashid

Viongozi wa vyama vya wafanyakazi

Viongozi mbali mbali wa Serikali

Viongozi wa taasisi binafsi

Nd. Wafanyakazi

Nd. Wananchi

Mabibi na mabwana

Asalaam alaykum

 IFUATAYO NI RISALA YA WAFANYAKAZI WA ZANZIBAR KUPITIA SHIRIKISHO LA VYAMA VYA WAFANYAKAZI ZANZIBAR KATIKA KUADHIMISHA SIKU YA WAFANYAKAZI DUNIANI TAREHE 01- 05 – 2012

Mhe. Mgeni Rasmi, ndugu viongozi na ndugu wafanyakazi
Kwanza kabisa nichukue fursa hii kumshukuru M/ Mungu mwingi wa rehema kwa kutujaalia kufika hapa tukiwa wazima wa afya zetu na usalama wa nchi yetu
Pili, tunapenda kukushukuru wewe Mh. Rais kwa kukubali kwako kuwa Mgeni Rasmi katika siku hii adhimu inayoadhimishwa kila mwaka na Wafanyakazi Duniani
Tatu, tunawashukuru wageni wetu waalikwa, viongozi wafanyakazi na wananchi wote kwa kuhudhuria kwenu kwa wingi katika hadhara hii


Mhe. Mgeni Rasmi, ndugu viongozi na ndugu wafanyakazi
Siku ya wafanyakazi duniani (Mai Dei) ni miongoni mwa kumbukumbu muhimu duniani kote ambayo haitasahaulika kwani inaashiria historia iliyotokea siku ya tarehe 1 Mei, 1889 ambapo wafanyakazi huko CHICAGO Marekani waliandamana kwa amani kwa madhumuni ya kupinga madhila waliyokuwa wakifanyiwa katika sehemu zao za kazi na kudai haki zao, maslahi yao na hali bora za usalama katika sehemu za kazi zao,
Baadhi ya madhila ambayo waliyapinga wafanyakazi hao ni
·      Kufanyishwa kazi kwa masaa mengi bila mapumziko wala malipo ya ziada
·      Kulipwa mishahara duni isiyokidhi hali zao za maisha
·      Kafanyakazi katika mazingira yasiyo na usalama kiafya nay a hatari
·      Kubaguliwa katika sehemu zao za kazi hasa ubaguzi wa rangi
·      Kudhalilishwa katika sehemu za kazi

Lakini badala ya kusikilizwa na waajiri na Serikali ya wakati huo huko Marekani, mabavu yalitumika na kuwatawanya kwa mitutu ya bunduki na kwa masikitiko makubwa maelfu ya wafanyakazi wasio na hatia waliuwawa.

Pamoja na kwamba ni miaka 123 imepita tangu tukio hilo litokee wafanyakazi wote Duniani wanaendelea kuliadhimisha kila ifikapo tarehe kama ya leo

Vile vile tukio hilo limekuwa kichocheo kinachopelekea wafanyakazi kote Duniani kuendelea kudai haki, maslahi zaidi na mazingira bora ya kazi zao na kuhakikisha wanatambuliwa kuwa ni wadau muhimu katika maendeleo ya nchi na jamii zao. Hasa kwa vile bado baadhi ya nchi duniani hali haiko tofauti sana na ile ya wafanyakazi wa Chicago ya Mwaka 1889

Siku hii pia hutumika kuhimiza ajira zenye staha katika nchi zote duniani, yaani zenye maslahi bora na heshima kwa lengo la kuondowa migogoro, migongano na kutoaminiana baina ya Wafanyakazi, Waajiri na Serikali zao.

Ajira zenye Staha ni tamko la kimataifa la shirika la kazi duniani linaloelekeza nchi zote duniani kuhakikisha mambo yafuatayo

1.  Fursa za kuajiriwa au kujiajiri kwa wananchi zinaimarishwa
2.  Haki za msingi za wafanyakazi zinalindwa katika nchi
3.  Majadiliano ya pamoja na ufungwaji wa mikataba kwa wafanyakazi na ushirikishwaji katika mambo ya ajira kwenye ngazi zote.
4.  Hifadhi ya jamii kwa wafanyakazi na familia zao zinakuwepo

Mhe. Mgeni Rasmi, ndugu viongozi na ndugu wafanyakazi

Miongoni mwa haki za msingi za wafanyakazi duniani ambazo kwa bahati nchi yetu imeridhia ni inastahiki kuzilinda ni kama zifuatazo

1.  Haki wa kujiunga pamoja na kufanya shughuli za vyama vya wafanyakazi bila kuingiliwa
2.  Haki ya kujadiliana na muwajiri juu ya masula na mazingira ya kazi na kufungiana mikataba ya hali bora za kazi
3.  Haki ya kutofanyisha kazi za shuruti na kazi za utotoni
4.  Haki za utokubaguliwa au kudhalilishwa katika sehemu ya kazi yako
5.  Haki ya kulidwa kwa watoto na vijana na kazi za hatari
6.  Hati ya kupata mafao sawa kwa kazi zinazofanana

Mhe. Mgeni Rasmi, ndugu viongozi na ndugu wafanyakazi

Wafanyakazi wa Zanzibar tunamshukuru M/Mungu kwa kupata fursa ya kushirikiana nawe katika maadhimisho haya adhimu, kama ulivyoshuhudia tumeandamana kwa amani ilikuonyesha furaha yetu kwako na hisia zetu kwa Serikali yako na waajiri.  Fursa hii vile vile inatupa hamu ya kuelezea wazi wazi mafanikio yaliyofikiwa na Serikali unayoiongoza chini ya muundo wa Umoja wa Kitaifa unayoiongoza katika kipindi kifupi cha kuwa madarakani,

Miongoni mwa mafanikio hayo ni

1.  Kuendeleza hali ya amani na utulivu hapa nchini kitendo kilichowafanya wafanyakazi na wananchi kuendelea na kazi zao bila wasiwasi wowote.
2.  Kutoa fursa kwa vyama vya wafanyakazi kutekeleza shughuli zao bila kuingiliwa au kubughudhiwa na mtu au chombo chochote humu nchini.
3.  Jitihada zako za kushirikiana na vyama vya wafanyakazi katika kutatua kero zao na kutoa huduma bora kwa wananchi
4.  Juhudi unazozifanya katika kuimarisha Maslahi ya wafanyakazi wake. mfano
·      Kuunda wizara maalum inayoshughulikia maslahi ya wafanyakazi
·      Kurejesha utaratibu wa kupandisha ngazi watumishi
·      Kurejesha utaratibu wa nyongeza za mwaka
·      Kuzingatia taaluma katika kupanga mishahara ya wafanyakazi
·      Kuzipa vipaumbele taaluma adimu
·      Kupambana na tatizo la wafanyakazi hewa na malipo hewa

5.  Kuimarishwa kwa kitengo cha kutatua migogoro
6.  Kuundwa kwa kamati ya kitaifa ya afya na usalama katika sehenu za kazi
7.  Bodi ya ushauri wa mambo ya kazi sasa inakutana kwa mujibu wa sheria.
8.  Kukutana kwa bodi ya ushauri wa kima cha chini cha mshahara na kupitia mishahara ya sekta binafsi.
9.  Kuwashirikisha wafanyakazi katika michakato ya kitaifa
10.       Kuanzisha mchakato wa kutungwa kwa sera ya hifadhi ya jamii

Mhe. Mgeni Rasmi, ndugu viongozi na ndugu wafanyakazi

Pamoja na hatua tulizoziainisha na tulizokuwa hatukupata muda wa kuzieleza bado wafanyakazi wale wa Serikalini, sekta binafsi na sekta isiyo rasmi kwa Mwaka mmoja uliyopita haukuwa mzuri sana, hali hii ilisababishwa na mambo mengi yalijitokeza katika kipindi hicho yakiwemo yafuatayo

1.     Kuendelea kuwepo kwa matatizo makubwa katika utaratibu wa nyongeza za mishahara ulifanywa na serikali mwaka jana. mfano
·   Vyama vya wafanyakazi kutoshirikishwa kabisa katika mapendekezo ya nyongeza za mishahara ya serikali kama sheria ya ajira inavyoeleza.
·   Serikali kushindwa kutoa malimbikizo ya mishahara kwa wale waliochelewa kufanyiwa marekebisho kama utaratibu unavyotakiwa
·   Serikali haikuwa makini katika utekelezaji nyongeza za mishahara kiasi kwamba lilileta usumbufu kwa baadhi ya wafanyakazi.
2.     Kuchelewa kutekelezwa kwa masuala ya kisheria juu ya masuala ya maslahi ya wafanyakazi
a)      Uundwaji wa kanuni za sheria za kazi.
b)    Uundwaji wa Idara ya fidia
c)     Mahakama ya kazi ya Zanzibar kukosa jengo na kanuni
3.     Kutokuwajibika kwa baadhi ya watendaji katika kusimamia sheria za kazi
·         Kutokusimamia ipasavyo ufungaji wa Mikataba ya kazi sehemu za kazi hasa katika sekta binafsi jambo linalopelekea wafanyakazi kukosa haki zao.
·         Kutokuwasilishwa kwa Mikataba ya Kimataifa katika Baraza La Wawakilishi la Zanzibar
·         Bodi ya ushauri wa mishahara kutokutumiwa katika kupendekeza mishahara Serikalini kama sheria inavyolekeza.
4.     Upungufu wa vitendea katika baadhi ya sehemu za ambavyo vilidumaza uwezo wa utendaji wa kazi katika sehemu zao za kazi.
5.     Kutokuwepo kwa chombo cha Kitaifa cha majadiliano katika masuala ya kazi
6.     Ushirikishwaji mdogo wa wafanyakazi katika masuala yanayowahusu kwa mujibu wa sheria (Kamati za uongozi).
7.     Madeni ya serikali juu ya haki za wafanyakazi kama vile likizo, overtime na fidia.
8.     Baadhi ya waajiri kutokutoa ushirikiano wa  kutosha juu ya utekelezaji wa tamko la kupandishwa kima cha chini cha mshahara wa sekta binafsi
9.     Baadhi ya viongozi wa Serikali na taasisi za binafsi kuwa na mtazamo hasi juu ya kuwepo na kufanyakazi kwa vyama katika sehemu zao za kazi na Kitaifa.
10.                      Wafanyakazi wa mashirika ya umma kuchelewa kufanyiwa marekebisho ya mishahara yao kila ambapo wafanyakazi wengine wa serikali wanaporekebishiwa mishahara

Mhe. Mgeni Rasmi, ndugu viongozi na ndugu wafanyakazi

Wafanyakazi wa Zanzibar wanaendelea kukosa usingizi juu ya hali inavyoendelea nchini mwetu kwa maoni mwa mambo yanayo wapa taabu sana ambayo viongozi wa serikali iliyopo madarakani ni lazima wayashughulikie ni

1.  Wasi wasi wa wafanyakazi kuhusu kuendelea kupanuka kwa pengo baina ya watumishi wa kawaida na wale wa ngazi za juu (wateuliwa wa Rais)
2.  Mazingira ya kazi kiafya na usalama yanahitaji kuboreshwa
3.  Wasi wasi wa wafanyakazi juu ya miswada ya sheria inayopelekwa katika Baraza la Wawakilishi bila kuzingatia mahitaji na haki za msingi ya wafanyakazi
4.  Tatizo la ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana linatishia usalama wa nchi wakati wo wote kuanzia sasa.
5.  Masula ya msingi ya kazi kama vile hifadhi ya jamii na fidia kwa wafanyakazi kutokuwepo chini ya wizara ya kazi jambo linalosababisha ushiriki wa vyama vya wafanyakazi kuwa mdogo.
6.  Kujitokeza kwa vikundi vinavyo hatarisha amani kwa kukashifu wananchi wenzao na viongozi kwa visingizio vya dini
7.  Hali za baadhi ya viongozi kutokuzielewa sheria za kazi na kufikia hadi kuwabughudhi wanachama wa vyama vya wafanyakazi

Mhe. Mgeni Rasmi, ndugu viongozi na ndugu wafanyakazi

Wafanyakazi tunamatarajio makubwa kwamba viongozi mliomadarakani mtajitahidi kufuata sheria, kutandika miongozo mizuri ya utawala bora na kutimiza ahadi zenu mlizozitoa wakati wa uchaguzi wa 2010 zikiwezo

Ø Kushirikana na vyama vya wafanyakazi katika kuimarisha mashali ya wafanyakazi
Ø Kutatua kero zinazowakabili wafanyakazi humu nchini ikiwemo mishahara midogo
Ø Kukuza fursa za ajira kwa vijana wetu
Ø Kuwashirikisha wafanyakazi katika mambo yanayowahusu kwa mujibu wa sheria.
Ø  Kutekeleza sheria za kazi kama zilivyo pitishwa
Ø  Kutekeleza sera ya ajira ya Zanzibar kwa lengo la kukuza ajira, ufanisi pamoja na kuimarisha sekta ya viwanda.
Ø  Kutekeleza mpango wa utekelezaji wa kuondoa ajira za watoto Zanzibar

Haya yote tunayakumbusha ili yawe vipaumbele serikali na waajiri kwa malengo yafuatayo

1.  Kuimarisha maisha ya wafanyakazi, familia zao na jamii kwa ujumla.
2.  Kuwepo kwa ajira zenye staha (desent work) na huduma bora kwa umma (quality public sevices delivery)
3.  Kuwepo kwa utekelezaji makini wa sheria za kazi na mikataba ya kimataifa.
4.  Kuwepo kwa mashirikiano bora kwa wadau wote katika kuleta tija, ufanisi na maendeleo ya nchi kijamii na kiuchumi

Mhe. Mgeni Rasmi, ndugu viongozi na ndugu wafanyakazi

Kauli mbiu ya mwaka huu ya maadhimisho ya Mei Mosi hapa Zanzibar ni

MFUMKO WA BEI KODI KUBWA NI MISHAHARA DUNI, NI PIGO KWA WAFANYAKAZI

Wafanyakazi wa Zanzibar wameamua kuchagua ujumbe huu kwa kuzingatia kuwa masuala hayo matatu ni miongoni mwa matatizo makubwa ya wafanyakazi wa yanayowakabili kwa sasa.  
Pamoja na jitihada zinazofanywa na viongozi wa juu, wizara na Serikali kwa ujumla kuhakikisha mfumko wa bei upungue hapa nchini bado wafanyabishara na watoa huduma hawaonekani kusikia au kujali hatua hizo za serikali na wanaendelea na kuuza bidha au kutoa huduma kwa bei za juu

Kupitia ujumbe huu tunaiomba serikali yetu kuchukua juhudi, hatua za dharura na kuandaa mipango madhubuti kupambana na watu kamahao wanaojitakia manufaa na utajiri migongoni mwa wananchi ambao maisha yao ni ya masghaka
.
Aidha, wafanyakazi wa Zanzibar ni miongoni mwa walipa kodi wakuu na wa uhakika vile vile ndio kundi pekee lenye uhakika wa kulipa aina zote kodi bila kukwepa. Isisahaulike kuwa wafanyakazi pia ndilo kundi linalolipa kodi mara nyingi, yaani moja kwa moja na kupitia huduma na bidhaa

Cha kusikitisha ni kwamba kila ukicha kodi zinapanda na nyingine zinaanzishwa, hivyo anaeumia zaidi ni mfanyakazi na familia yake
Kwa kupitia ujumbe huu tuaiomba serikali kupitia upya taratibu za kodi anazomgusa mfanyakazi na kuzipunguza ili kumpunguzia mzigo ambao tayari umemlemea

Suala la mishahara midogo na mafao mengine ni kilio kikubwa kwa wafanyakazi wa Zanzibar la kusikitisha zaidi ni kwamba pamoja na serikali kufanya jitihada ya kuongeza mishahara suala hili linakwazwa na kupanda kwa gharama za maisha
Kwa upande mwengine Serikali kwa kushirikiana na wadau wake kukubaliana kuongeza kiwango cha mishahara cha sekta binafsi lakini bado kuna baadhi ya waajiri wanapinga kutoa mishahara hiyo kwa visingizio mbali mbali na wengine ni jeuri tu

Hivyo basi kutitia ujumbe huu tunaiomba serikali ilisimamie suala hili kinyume chake linaweza kuleta mtafaruku katika sekta ya ajira na uhatarisha amani iliopo

Wafanyakazi wa Zanzibar ni wavumilivu sana lakini uvumilivu unamipaka nasi hatumbeni tufike kuko ndio maaana tunakumbushana hapa hadharani

Mhe. Mgeni Rasmi, ndugu viongozi na ndugu wafanyakazi

Kwa kumalizia tungalipenda kutoa nasaha zetu au w itokwa wafanyakazi wenzetu mliohudhuria hapa na wafanyakazi wote wa Zanzibar kupitia kwenu:-
1.  Kuelewa nafasi yetu katika maendeleo ya nchi yetu kwa kufanya kazi kwa bidii katika kujenga uchumi wetu ilituweze kuhalalisha madai yetu mbele ya waajiri na serikali kwani penye tija maslahi huongezeka au HAKI NA WAJIBU NI WATOTO PACHA.
·Tunawaomba  wafanyakazi kuutumia muda wa kazi kwa kuzajisha mali au kutoa huduma zilizobora kwa wananchi
·Kufika na kuondoka kazini kwa wakati
·Kujiepusha na uzembe, udokozi, rushwa ,upendeleo na ubaguzi
2.  Kuendeleza amani na utulivu katika sehemu zetu za kazi na nchi yetu na kufanya kazi kwa bidii, maarifa, nidhamu na ubunifu katika kuongeza tija na kuimarisha huduma bora kwa wananchi
3.  Tunatoa ushauri kwa viongozi wa kisiasa, vikundi vya kiraia , vikundi vya kidini, wafanyakazi wote na wananchi wote wa Zanzibar kuchukua kila tahadhari ili kuepukana na vurugu, mfarakano, utengano, ubaguzi, ugomvi, fitna na choyo katika kutekeleza majukumu yao na kushiriki katika michakato mbali mbali ya kitaifa yanayojitokeza hapa nchini, mfano ni wa mchakato wa mabadiliko ya katiba. Kwani ushahidi unaonyesha kwamba kuna baadhi ya taasisi kama hizo tayari wameichukuwa hoja ya katiba kuwagawa wananchi
4.  Tunawaomba wafanyakazi na wananchi wote wa Zanzibar kuchukua kila tahadhari ili kuepukana na maambukizo ya Ukimwi, kutokaribia Madawa ya kulevya, uharibifu wa mazingira, kuchukia rushwa, ufisadi na wizi wa mali za umma, mambo ambayo huzorotesha maendeleo ya nchi yoyote.
5.  Tunawatahadharisha viongozi tuliowachaguwa na kuteuliwa kwamba wamepewa jukumu la kutuongoza na si kututawala hivyo ushirikishwaji wa wafanyakazi na wananchi ni kitu cha lazima. Kwani ushahidi unaonyesha kwamba kuna baadhi ya viongozi waliochaguliwa na hasa waliteuliwa kuongoza taasisi za serikali na mashirika wanatumia nafasihizo vibaya kwa kutokuzingatia haki za wafanyakazi
6.  Tunawashauri wafanyakazi wote kujiunga na kuviunga mkono vyama vya wafanyakazi kama njia ya kuimarisha umoja wetu na mshikamano wetu na kupata nguvu za kuwasilisha madai yetu mbele ya waajiri na Serikali. Hatuna wasiwasi kuwa Serikali yetu ni sikivu na iko tayari kutekeleza maombi yetu.
Sisi wafanyakazi wa Zanzibar tunakuhakikishia Mh. Rais na Serikali unayoiongoza na wananchi kuwa tumekuwa na tuko tayari kushirikiana nanyi katika juhudi za kukuza na kuimarisha uchumi wetu kwa faida yetu sote

Mhe. Mgeni Rasmi, ndugu viongozi na ndugu wafanyakazi
Mwisho kabisa tungelipenda kuchukuwa fursa hii kwa mara nyengine tena kukupongeza sana kwa kufika kwako katika maadhimisho yetu haya na kwa msaada mkubwa na nasaha unazoendelea kutupa wakati wote na hasa katika kipindi cha maadhimisho kama haya.
Wafanyakazi wa Zanzibar tunakuahidi kukuunga mkono katika jitihada zako na Serikali za kuwaletea maendeleo Wazanzibari na watanzania na tuko bega kwa bega katika kujenga umoja, amani na uchumi wa taifa.Tunakutakia kila la kheri na tunakuombea kwa M/Mungu akupe afya ili ukitumikie kipindi chako cha uongozi salama, akupe umri mrefu wenye neema na familia yako. Tunakuahidi kuendelea kutumia ushauri na busara zako unazotupa na utakazotupa kwani mchango wako kwa vyama vya wafanyakazi vya Zanzibar wauwezi kuepukika.
Vile vile shukurani zetu dhati kwa Mh. Waziri wetu wa Kazi, Uwezeshaji wananchi kiuchumi na Ushirika, nd. Haroun Ali Suleiman pamoja na watendaji wake wote wanaoongozwa na Bibi: Asha Ali Abdulla kwa mashirikiano yao mema na jumuiya yetu,
Aidha pongezi na shukrani za pekee kwa mh. Waziri wa utumishi wa umma na utawala bora Mh. Haji Omar Kheir kwa ushirikiano usiokifani na ZATUC, kusema kweli mh. Kama mawaziri wengine wangaliiga mfano wa mh. Haji tusingalikuwa hapa katika maendeleo ya nchi. Anajali ushauri wetu , anashirikiana nasi katika raha na shida, hana mafuta ya ukubwa . Tumpongezeni sana na wasaidizi wake wakiongozwa na Bw. Joseph Meza
Shukurani kwa viongozi wote wa serikali, Jumuiya ya waajiri, Shirika la kazi duniani kwa mashirikiano yao kwetu

Asanteni kwa kunisikiliza

SOLIDARITY FOR EVER

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.