Habari za Punde

Zanzibar inajuvunia uhusiano wake na Norway

Na Mwandishi wetu,
ZANZIBAR inajivunia uhusiano wa muda mrefu uliopo baina ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya watu wa Norway katika kusaidia maendeleo ya wananchi wa Zanzibaar.
Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Makaazi Maji na Nishati, Ali Khalil Mirza ameyazungumza hayo wakati wa mkutano wa pamoja baina ya ujumbe wa Kamati ya Nishati na Mazingira kutoka nchi ya Norway ulipofika ofisini kwake Forodhani kuangalia utekelezaji wa miradi inayosimamiwa na nchi hiyo.
Katibu Mkuu amesema kuwa uhusiano wa muda mrefu uliopo wa kuwapa mafunzo watendaji mbali mbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na uwekezaji katika sekta ya Nishati ya umeme ni jambo la kupigiwa mfano.
Ujumbe huo wa kamati ya Nishati na Mazingira kutoka Bunge la Serikali ya Norway ukiongozwa na Mwenyekiti wa kamati hiyo Bwana Ola Elvestuen umefika Zanzibar kuangalia utekelezaji wa miradi mbali mbali inayofadhiliwa kupitia Shirika la Maendeleo la nchi ya Norway (NORAD).

Mbali na ujumbe huo kufanya mazungumzo na watendaji wa ofisi mbali mbali ulipata fursa ya kutembelea kazi mbali mbali za ujasiriamali huko vijijini zinazoendeshwa kwa kutumia nishati ya umeme.
Meneja Mkuu wa Shirika la Umeme Zanzibar, Mhandisi: Hassan Ali Mbarouk akiukaribisha ujumbe huo kuzungumza na wananchi wa shehia sita (6) za Mkoa wa Kaskazini hapo Chuo cha Amali Mkokotoni amesema kuwa Shirika la Umeme linajivunia mafanikio makubwa ya utekelezaji wa mradi huo wa usambazaji umeme vijijini ulitekelezwa kwa awamu nne (4) tofauti zenye mafanikio makubwa tokea mashirikiano hayo yalipoanza mnamo miaka ya 1980s.
Amefahamisha kuwa mradi wa usambazaji umeme vijijini umepelekea upatikanaji wa umeme katika maeneo mengi ya Unguja na Pemba ikiwemo uwekaji na ulazaji waya wa umeme baharini kutoka Tanga hadi Pemba, uwekaji na ulazaji waya wa umeme bahirini kutoka Mkokotoni hadi Tumbatu, uimarishaji wa miundo mbinu ya umeme na usambazaji umeme vijijini.
Ujumbe huo ulitembelea na kuangalia kazi mbali mbali za mikono kama vile kiwanda cha mbao na kusaga nafaka kilichopo Mkwajuni na kuangalia kazi mbali mbali zinazofanywa na Chuo cha Amali Mkokotoni zikiwemo ushoni na ufundi wa umeme.
Aidha, ujumbe huo ulihitimisha ziara yake kwa upande wa Unguja kwa kufanya mkutano na kuzungumza na wananchi wa shehia sita (6) za Mkoa wa Kaskazini Unguja ikiwemo shehia ya Mkokotoni, Pita na Zako, Mto wa Pwani, Kibeni, Pale na Mkwajuni.
Wananchi hao wametoa shukrani zao kwa Serikali ya Norway juu ya miradi ya usambazaji umeme katika mkoa huo na kusema kuwa imewakomboa kiuchumi hususan katika shughuli zao za uvuvi na kuuomba ujumbe huo kuweka nguvu zao zaidi kuwasaidia katika sekta ya kilimo hususan kilimo cha umwagiliaji maji.
Wakiwa ni wafadhili wa karibu wa huduma ya umeme kupitia Shirika la Umeme ZECO na ushirikiano uliopo tokea miaka ya 1980s Serikali ya Norway kupitia Shirika lake la Maendeleo (NORAD) wameweza kusaidia sekta ya umeme nchini kwa awamu nne tofauti zenye mafanikio ikiwa Shirika la Umeme (ZECO) kwa sasa linajiandaa na mpango mwengine wa utekelezaji wa mradi huo unaofadhiliwa na NORAD.
Naye Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya Nishati na Mazingira kutoka Norway Bwana Ola Elvestuen kwa niaba ya Serikali ya Norway wamewashukuru wananchi hao kwa mwitikio wao na kuzungumzia changamoto mbali mbali zinazowakabili na kuahidi kuzifikisha sehemu husika ili kuweza kufanyiwa kazi.
Ujumbe huo utaendelea na ziara yake wiki hii kisiwani Pemba.

 

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.