Habari za Punde

Rais Dk Shein Awataka Watumiaji wa Mitandao Kuwa Makini na Kulinda Hali ya Amani Nchini Kuepusha Matatizo.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                            10.2.2016
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  amewataka  watumiaji wote wa mitandao ya kijamii na wale wenye dhamana ya kusimamia na  kufanya tahariri wawe makini zaidi ili kulinda hali ya amani ya nchi na kujiepusha na matatizo yanayoweza kuwakumba kwa uvunjaji wa sheria.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika maadhimisho ya Siku ya Sheria Zanzibar zilizofanyika katika viwanja vya Victoria Garden, Mjini Zanzibar na kuhudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Idd, Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mohamed Chande Othman na wengineo.

Katika hotuba yake hiyo Dk. Shein alisema kuwa inasikitisha kuona kwamba baadhi ya viongozi na wahariri wa mitandao hiyo wanaishi hapa Zanzibar na wanausahau utu wao pamoja na utu wa wenzao kwani heshima ya wananchi wa Zanzibar inayoambatana na utamaduni na desturi zao zinajulikana vizuri sana.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ina imani kwamba kuwepo kwa mitandao ya kijamii iliyobora na inayotumainiwa na kuongozwa kwa kuzingatia sheria ni jambo la lazima kwa maendeleo na kuimarisha uhuru wa wananchi wa kutoa maoni kama ilivyoelezwa na Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 katika Ibara ya 18.

Dk. Shein alisema Serikali inaendelea kuhakikisha kuwa uhuru wa wananchi wa kuwa na maoni yao pamoja na uwezo na kutafuta na kutoa taarifa unatumiwa vizuri na kwa kuzingatia sheria, ili kulinda haki za wananchi na maslahi ya nchi.

“Kwa upande mwengine, ni wajibu wa kila mwananchi kuelewa kwamba Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 inatulinda na inatuhakikishia kuwa katika utumiaji wa taarifa na utoaji wa maoni, utu wa mtu unaheshimika na hakuna aliye na haki kisheria ya kuweza kumdhalilisha mwenzake”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa Sheria ya Mitandao ya mwaka 2015, iliyopitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inazidi kulinda heshima, hifadhi na faragha za wananchi katika suala zima la mawasiliano kupitia mitandao na simu kama ilivyokusudiwa na sheria hiyo.

Dk. Shein alisema kuwa ipo baadhi ya mitandao ya kijamii ambayo inatumiwa kurusha habari za uchoshezi na habari za uongo dhidi ya Serikali ambapo baadhi ya wakati mitandao hiyo inaruhusu wanachama kutumia taarifa huku wakificha majina yao.

Katika hotuba yake hiyo Dk. Shein alisema kuwa ni wazi kwamba kauli mbiu ya mwa ka huu isemayo ‘ Matumizi Mabaya ya Mitandao ya Kijamii Yanaweza kuwa Chanzo cha Uvunjaji wa Sheria na Amani ya Nchi” imekuja wakati mzuri ambapo matumizi ya simu na mitandao yameongezeka na kukua kwa kiasi kikubwa hapa Zanzibar.

Alisema kuwa hivi sasa mwananchi  wa Zanzibar, takriban popote alipo katika kisiwa cha Unguja na Pemba anaweza kupata huduma za inteneti na kujiunga na mitandao ya kijamii yote muhimu duniani kwa haraka na wepesi kwa kupitia mashirik mbali mbali ya simu yaliopo Zanzibar.

“Mitandao yote hii sasa imekuwa ni nyenzo muhimu ya kurahisisha utoaji wa huduma na ya kupeana taarifa mbali mbali zikiwemo zile zinazoitwa ‘dripu’...ni taarifa zinazotolewa kwa lengo la kutiana moyo juu ya jambo fulani japo kuwa taarifa hizo baadhi ya wakati huwa hazina ukweli wala mantiki yoyote”,alisema Dk. Shein.

Dk. Shein alisema kuwa faida zinazopatikana kwa kuwepo na kuimarika kwa huduma za intaneti, mitandao ya kijamii na huduma za simu zimegusa sekta zote za kiuchumi na kijamii kwani teknolojia ya habari imerahisisha sana maisha na kufungua fursa nyingi ambazo zinahitaji kulindwa kwa sehria ili faida zinazopatikana ziwe endelevu.
Hata hivyo Dk. Shein alieleza kuwa iko haja kuanza kufikiria namna bora itakayowezesha kutumia simu na mitandao wakati wa kazi bila ya kuathiri utekelezaji wa majukumu, hasa katika taasisi zinazotoa huduma kwa wananchi.

Pia, alisisitiza umakini katika kuhakikisha kuwa matumizi ya simu makazini hayaathiri utekelezaji wa majukumu yaliopangwa.

Wakati huo huo, Dk. Shein ameeleza azma ya Serikali katika bajeti ijayo ya kujenga jengo jipya la Mahakama Kuu huko Tunguu pamoja na kupokea ombi la kuongezwa kwa Majaji na kusisitiza kuwa Serikali itatekeleza wajibu wake.

Aidha, ameueleza uongozi wa Mahakama kuu kuwa fedha zilizoombombwa hivi karibuni Tsh, milioni 30 kwa ajili ya kumalizia jengo la Mahakama ya Watoto huko Mahonda atawapa kwa lengo la kumazizia ujenzi huo pamoja na kulengwa vizuri Bajeti yao ya mwaka huu wa fedha. Pia, Dk. Shein alizindua kitabu cha mwaka cha Sheria.

Mapema Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar Othman Makungu alisema kuwa katika kipindi cha mwaka mmoja wamesogeza karibu zaidi huduma za kimahkama kwa wananchi baada ya kuanzishwa kwa Mahakama ya Mwanzo Kitulia Wete Pemba pamoja na  kuanzishwa kwa Mahakama ya Biashara.

Jaji Makungu alisema kuwa duniani kote watu wanawasiliana kwa njia ya mtandao ambao umerahisisha mawasiliano yakiwemo ya kibiashara, kiuchumi, kielimu na kihabari.

Aliongeza kuwa simu za mkononi zimekuwa ni kero shuleni, kazini, nyumbani na hata katika nyumba za ibada ambapo baadhi ya ndoa zimevunjika kutokana na meseji mbaya zilizoonekana katika simu ya mmoja wa wanandoa.

Pia, katika nchi zinazoendelea intaneti imekuwa ni kero, imeathiri maendeleo mazuri ya wanafunzi kimasomo na pia, imeathiri maendeleo mazuri ya wanafunzi kimasomo na pia, imeathiri maisha ya vijana, watoto na  hata watu wazima kutokana na kuangalia picha chafu na kutumia muda mwingi kuchati na marafiki.

Hata hivyo Jaji Makungu alisema kuwa mtandao umekuwa na changamoto kubwa kwa Tume za Uchaguzi duniani, ikiwemo zile za Tanzania na Zanzibar ambapo matokeo ya uchaguzi yamerushwa kwenye mitandao kabla ya kutangwaza na Tume husika.

Nae Mwanasheria Mkuu wa Serikali  ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Said Hassan Said alisema kuwa  pamoja na kuwepo kwa faida katika matumizi sahihi ya mitandao pia, kumekuwepo na changamoto kubwa ya matumizi mabaya ya mitandao katika jamii.

Ili kudhibiti matumizi mabaya ya mitandao Mwanasheria Mkuu alitoa wito wa kuheshimu Katiba na Sheria za nchi katika matumizi ya mitandao ya kijamii, kutumia mitandao ya kijamii kwa usahihi zaidi katika kujiletea maendeleo ya kiuchumi na kijamii, kuongeza uwezo wa kitaaluma waataalamu wa kiusalama katika usimamizi wa matumizi ya mitandao, kupiga vita hali hiyo na kutoa mashirikiano kwa vyombo vinavyosimamia sheria ili kuthibiti hali hiyo.

Viongozi mbali mbali walihudhiiria hafla hiyo akiwemo pia, Jaji Kiongozi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Shaaban Ali Lila, Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Mhe. Jaji Damian Lubuva, Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi Ali Abdalla, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Ikulu na Utawala Bora Mhe. Mwinyihaji Makame Mwadini, Mkurugenzi wa Mshtaka, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Mahakimu, Makadhi na viongozi wa dini pamoja na wananchi.

Rajab Mkasaba, Ikulu

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.