Habari za Punde

Balozi wa Tanzania nchini Kuwait afanya mazungumzo na Mwenyekiti wa Makampuni ya Fouad Alghanim

Balozi wa Tanzaznia nchini Kuwait, Dkt. Mahadhi J. Maalim, akiwa katika picha ya pamoja na Bw. Fouad Alghanim, Mwenyekiti wa Umoja wa Makampuni ya Fouad Alghanim. Kushoto kwa Mhe. Dkt. Mahadhi ni Bw. Sami M. Al-Farhan, Makamu Wa Rais wa Umoja huo wa Makampuni ya Fouad Alghani anayeshughulikia masuala ya uwekezaji wa Kimataifa na mwanzo upande wa kulia ni Bw. Iman Njalikai, Mkuu wa Masuala ya Utawala katika Ubalozi wa Tanzania Kuwait.
Mhe. Dkt. Mahadhi Juma Maalim, Balozi wa Tanzania nchini Kuwait akiwa katika mazungumzo na Bw. Fouad Alghanim, Mwenyekiti wa Umoja wa Makampuni ya Fouad Alghanim.

Balozi wa Tanzania nchini Kuwait Mhe. Dkt. Mahadhi Juma Maalim, , amemtembelea Mwenyekiti wa Umoja wa Makampuni ya Fouad Alghanim, Bw. Fouad M. T. Alghanim ofisini kwake tarehe 1 Septemba 2016.

Umoja wa Makampuni ya Fouad Alghanim, unajumuisha zaidi ya Makampuni ishirini ambayo yanajihusisha na masuala mbalimbali ikiwemo uwekezaji, nishati, mafuta na gesi, usafirishaji, miundombinu, biashara ya magari, masuala ya anga na ndege, mawasiliano, ujenzi wa makazi ya kisasa, masuala ya ulinzi, utalii na afya.

Katika mazungumzo hayo, Mwenyekiti huyo alieleza matarajio yake juu ya ziara atakayofanya hivi karibuni kutembelea Tanzania ili kujionea fursa mbalimbali za uwekezaji zinazopatikana. Mwenyekiti huyo alimfahamisha mheshimiwa Balozi kuwa licha ya kutokuwa na shughuli za kiuchumi nchini Tanzania, Umoja huo unatekelezaji miradi mbalimbali katika nchi za jirani za Uganda, Rwanda na kwingineko. Aliongeza kuwa, Umoja huo una nia ya kuwekeza katika sekta mbalimbali Tanzania hususan miundombinu.

Kwa upande wake, Mhe. Dkt. Maalim, alimshukuru Mwenyekiti huyo kwa kuonesha nia ya kutembelea Tanzania na kuona fursa mbalimbali za uwekezaji. Vilevile, alimshauri kuangalia namna ambavyo Umoja huo unaweza kushirikiana na Serikali pamoja na Sekta binafsi hususan katika suala la ujenzi wa makazi ya kisasa katika Makao Makuu mapya ya Serikali mjini Dodoma.

Aidha, Mhe. Dkt. Maalim, alipongeza kitendo cha Mwenyekiti huyo kuamua kufanya ziara Tanzania na kumuahidi kuwa Ubalozi wa Tanzania Kuwait upo tayari kutoa ushirikiano utakaohitajika ikiwepo kuwapatia taarifa muhimu kuhusu uwekezaji nchini Tanzania, pamoja kuwakutanisha na wadau muhimu katoka sekta binafsi na ile ya umma.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.