Habari za Punde

Wadau wa Utalii watakiwa kutangaza maeneo mapya yaliuoibuliwa

Na Abdi Shamnah

WAZIRI wa Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo Zanzibar, Mhe. Rashid Ali Juma, amawataka wadau wa Utalii wanaolenga kuitangaza Zanzibar katika maeneo mbali mbali ya dunia, kuelekeza nguvu katika maeneo mapya yalioibuliwa.

Alisema kuna umuhimu wa wadau hao kuelekeza nguvu zao katika kutangaza vivutio vipya vya utalii, hususan vinavyogusa utamaduni wa Wazanzibari.

Changamoto hiyo ameitoa ofisini kwake Kikwajuni, alipokuwa na mazungumzo na Mkurugenzi wa Makampuni ya Naif Company Limited na Naif Engineering Company, Bi.Khadija Naif, alipofika nchini kwa lengo la kuangalia vivutio vya utalii vilivyopo pamoja kuwashajisha wajasiriamali wa Zanzibar kutangaza biashara zao katika nchi za Ghuba.

Alisema kwa kipindi kirefu kumekuwa na juhudi za kuutangaza Utalii wa Zanzibar, kupitia vivutio mbali mbali, ikiwemo historia, inayohusisha utawala wa kisultani, fukwe, magofu na makumbusho.

Alisema wakati umefika kwa wadau wa utalii nchini, kuutangaza utalii wa Zanzibar katika nyanja za kiutamaduni na kubainisha kuwepo maeneo mengi, vikiwemo vyakula vya asili vinavyoliwa na wenyeji.

Aidha alisema eneo jengine ni kuhusiana na mavazi ya Wazanzibari, ambayo kimsingi yanafanana na yale yanayovaliwa na wananchi wa nchi za Ghuba, sambamba na urembo wa asili, ukiwemo ule utokanao na miti na rasilimali zake.

Aidha alisema hatua ya UNESCO kuizawadia Zanzibar kuwa kituo cha Hifadhi ya kimataifa, kutokana na uhifadhi wa  kimaumbile wa misitu yake pamoja na wanyama walio na tabia tofauti duniani, ni vyema wadau hao wakachukua jukumu la kuitangaza.

‘UNESCO imetuzawadia kwa kuwa na misitu ya kimaumbile, lakini pia tuna wanyama walio tofauti na wengine wote duniani, tunao wanyama wenye uwezo kwa siku kula miti mia moja ya aina tofauti, bila kuathirika, jambo ambalo sio la kawaida na inapotokea kutaka kuathirika hutafuta makaa kama tiba’’, alisema.

Vile vile Waziri huyo alisema kuanza kwa safari za mashirika tofauti ya ndege hapa Zanzibar, ni ishara tosha kuwa utalii wa Zanzibar unaendelea kuimarika kadri siku zinavyosonga.

Alisema kutokana na juhudi mbali mbali zinazochukuliwa na wadau, asasi zisizo za kiserikali na taasisi za Serikali, kuna mwelekeo mzuri wa kufikia malengo ya kupokea hadi watalii 360,000 ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.

Waziri Rashid alimpongeza  Mkurugenzi huyo, kwa uzalendo anaonesha katika kuutangaza utalii wa Zanzibar, na kuthibitisha hoja kuwa utalii utaimarishwa na wadau wa sekta hiyo na sio taasisi za Serikali.

Nae, Mkurugenzi Naif, alisema amefarijika mno kufika hapa Zanzibar, na kupata fursa ya kutembelea maeneo mbali mbali pamoja na kuangalia vivutio vya utalii.

Alisema ametumia fursa hiyo  kuwahamasisha wajasiriamali wadogo wadogo wa Zanzibar kuandaa mazingira ya kutangaza bidhaa zao katika nchi za ghuba.

Alisema akiwa wakala wa utalii kutoka Saud Arabia atafanya kila juhudi kuhakikisha anautangaza vyema utalii wa Zanzibar, pamoja na kuwaunganisha wajasiriamali wa Zanzibar ili waweze kutumia fursa zilizopo nchini humo kwa kuuza bidhaa zao.

Aidha alisema anakusudia kuwaunganishi kati ya wafanyabaishara wa Saud Arabia na wajasiriamali wa Zanzibar ili waweze kutumia fursa za kupata bidhaa kutoka huko, kwa makubaliano ya Kibenki, ili kujiendeleza kimaisha.

Katika ziara hiyo Mkurugenzi huyo, alipata fursa ya kuzungumza na Mkurugenzi wa Jumuiya ya wafanyabaishara, Wenye viwanda na wakulima,Bi. Munira Houmud na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mwenyekiti wa Baraza la Mpinduzi,Mhe. Issa Haji Ussi.    

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.