Na Salmin Juma , Pemba
Naibu Waziri wa ujenzi na mawasiliano Zanzibar, Mh Mohammed Ahmada Salum amesema wizara imepanga kuzifanyia ukarabati barabara za ndani katika jimbo la Mkoani ili ziweze kupitika.
Amesema lengo la Serekali ni kuona wananchi wake wanaondokana na usumbufu wanaoupata wakati wa kusafiri na kusafirisha bidhaa zao.
Mh Mohammed ameeleza hayo kwa nyakati tofauti alipozitembelea barabara za ndani zilizomo katika jimbo la Mkoani pamoja na jimbo la Chambani na kuona hali halisi za barabara hizo.
Amesema ni vyema kwa wananchi kuwa wastahamilivu wakati serekali ikijiandaa kuziboresha barabara hizo ambazo ni kiunganishi kikubwa cha uchumi.
Nae mwakilishi wa Jimbo la Mkoani, Mmanga Mjengo Mjawiri ameiomba Wizara kuziangalia vyema barabara hizo ili kuwarahisishia wananchi kuyafikia masoko na mahitaji yao mengine ya kijami.
Mapema wananchi wa jimbo la Mkoani na Chambani wameiomba serekali kuharakisha kuziboresha barabara hizo ili ziweze kupitika kwa urahisi zaidi.
No comments:
Post a Comment