STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 27.12.2016
![---](file:///C:/Users/user/AppData/Local/Temp/msohtmlclip1/01/clip_image004.gif)
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein ameipongeza Serikali ya Oman na Serikali ya Cuba kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar
katika kuendeleza miradi ya maendeleo sambamba na kuimarisha uhusiano na
ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na nchi hizo.
Akizungumza kwa
nyakati tofauti wakati alipokutana na Mabalozi wa nchi hizo Ikulu mjini
Zanzibar hivi leo, Dk. Shein alizipongeza nchi hizo kwa kuendeleza uhusiano na
ushirikiano wa kihistoria ambao umekuwa chachu katika kuimarisha juhudi za
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kujileta maendeleo.
Akizungumza na Balozi
wa Cuba katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anaemaliza muda wake wa kazi hapa
nchini, Jorge Luis Lopez Tormo, Ikulu mjini Zanzibar, viongozi hao walisisitiza
haja ya kuendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya pande mbili hizo.
Katika Mazungumzo hayo,
Dk. Shein alisema kuwa Cuba ina historia kubwa katika juhudi za kuiunga mkono
Zanzibar kwenye sekta za maendeleo hasa sekta ya afya kwani tokea mwaka 1964
nchi hiyo imekuwa ikileta madaktari wake kuja kufanya kazi hapa Zanzibar.
Alieleza kuwa mbali ya
madaktari hao kuja kufanya kazi kwa kutoa huduma ya afya kwa jamii hapa nchini,
Cuba imekuza uhusiano wake kupitia sekta hiyo kwa kushirikiana na Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar kuanzisha chuo cha Udaktari ambacho tayari kimeshaanza
kuza matunda kwa kutoa Madaktari Wazalendo.
Aidha, alisema kuwa
mbali ya ushirikiano wa sekta ya afya alieleza haja ya kuanzishwa ushirikiano
katika sekta ya utalii kutokana na Cuba kupiga hatua kubwa katika sekta hiyo.
Dk. Shein alisema kuwa
Zanzibar ina mengi ya kujifunza kutoka kwa ndugu zao wa Cuba kutokana na nchi
hiyo kujiimarisha kwenye sekta ya utalii sambamba na vyanzo vyake vya utalii yakiwemo
maeneo ya kitalii likiwemo eneo maarufu la ukanda wa kitalii la ‘Varadero’.
Sambamba na hayo, Dk.
Shein alisema kuwa ushirikiano huo pia, utahusisha mji Mkongwe wa Zanzibar na
ule mji Mkongwe wa Havana ambao yote kwa pamoja ina historia kubwa pamoja na
vivutio kadhaa vya kitalii ndani yake.
Pia, Dk. Shein
alitumia fursa hiyo kwa mara nyengine tena kutoa mkono wa pole kwa kifo cha
kiongozi shupavu na mpigania haki za wanyonge marehemu Fidel Castro, na
kumtumia salamu Rais Raul Castro za kumtakia afya njema yeye na wananchi wa
Cuba ili waendelee kulijenga taifa hilo.
Dk. Shein alisisitiza
haja kwa nchi hiyo kuunga mkono azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya
kuwasomesha madaktari wazalendo katika vyuo vikuu vya afya nchini humo kupitia
kada maalum za udaktari kwa kiwango cha elimu ya juu kwa ufadhili wa SMZ.
Nae Balozi Jorge Luis
Lopez Tormo alimuhakikikishia Dk. Shein kuwa Cuba inathamini sana uhusiano na
ushririkiano wa kihistoria kati yake na Zanzibar na kuahidi kuendelea
kuudumisha.
Balozi huyo wa Cuba kuwa
miradi yote ya maendeleo inayoishirikisha nchi yake itaendelezwa kwa juhudi
kubwa huku akimueleza Dk. Shein kuwa nchi yake itafarajika kwa kuwepo
ushirikiano katika sekta ya utalii.
BaloziTormo alisema
kuwa kwa mwaka huu pekee, Cuba imeweza
kupokea watalii wapatao milioni tatu na nusu na kukiri kuwa mfanano wa miji
mikongwe ya Zanzibar na Havana unaweza kuwa chachu katika kukuza utalii kwa
pande zote mbili.
Mapema, Dk. Shein
alifanya mazungumzo na Balozi Mdogo mpya wa Oman, Ahmed Bin Humoud Al Habsi, ambapo
alitumia fursa hiyo kuipongeza Oman kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika
harakati zake za kukuza uchumi na kuimarisha maendeleo.
Dk. Shein alieleza
kuwa miongoni mwa juhudi zilizochukuliwa na Oman katika kuisaidia Zanzibar ni
pamoja na ujenzi wa Chuo cha Afya kilichopo Mbweni pamoja na fedha taslim kwa
ajili ya ununuzi wa vifaa vya Kiwanda cha Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali, msaada
wa gari kwa ajili ya viongozi wa Serikali na misaada mengine ambayo nchi hiyo
imeshawi kuitoa.
Aidha, Dk. Shein
alitumia fursa hiyo kumpongeza Sultan Qabous Bin Said Al Said na Serikali yake kwa
kuendelea kuiunga mkono Zanzibar na alimtaka
Balozi huyo wa Oman amfikishie salamu zake kwa kiongozi huyo.
Nae Balozi Ahmed Bin
Humoud Al Habsi, ambaye amechukua nafasi ya Balozi Mdogo wa Oman aliemaliza
muda wake wa kazi hapa Zanzibar, Ali Abdulla Al Rashdi alieleza kuwa Oman
itaendeleza uhusiano na ushirikiano wake kati yake na Zanzibar na kupongeza
hatua za maendeleo zilizofikiwa hapa nchini.
Aidha, Bin Mahmoud alisema
kuwa Serikali ya Oman inatambua juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein za kujiletea maendeleo hivyo, Oman
itaendelea kuziunga mkono juhudi hizo ili Zanzibar izidi kupata mafanikio.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment