STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 25.04.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amesema kuwa michezo ni sehemu ya maisha ya mwanaadamu na ina
umuhimu mkubwa hasa kwa vijana na ndipo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
imeamua kwa makusudi kuiimarisha michezo na utamaduni maskulini.
Hayo aliyasema leo
huko katika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi katika hafla ya kukabidhi vifaa vya michezo
kwa skuli za Mikoa ya Unguja na Pemba vilivyotolewa na Mwakilishi wa Jimbo la
Uzini, Mohammed Raza Dharamsi kwa ajili ya mashindano maalum ya ‘UMOJA CUP’ chini ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya
Amali.
Katika maelezo yake,
Dk. Shein alisema kuwa Serikali inatambua kuwa katika maisha ya mwanaadamu
yoyote michezo ina umuhimu, kwani huleta
mshikamano, kujuana, huburudisha na husaidia katika kujenga afya ya akili na
kiwiliwili kwa vijana na watu wazima.
Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kueleza historia ya michezo hapa nchini ikiwa ni pamoja na michezo katika
skuli ambapo hata yeye mwenyewe binafsi alishiriki kikamilifu wakati huo huku
akisisitiza kuwa michezo hudumisha umoja, udugu na kukuza ujasiri ambapo kwa
hivi karibuni, michezo imekuwa ni chanzo kikubwa cha ajira.
Aliongeza kuwa pamoja
na juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuendeleza michezo na
utamaduni katika Skuli lakini katika miaka michache iliyopita hamasa ya michezo
katika skuli ilionekana kushuka.
Hivyo, baada ya kuona
hivyo alichukua juhudi za makusudi kutokana na ukereketwa wake wa michezo
alichukua hatua kadhaa ikiwemo kuwaita wanamichezo mahiri wa zamani na wenye uzoefu
mkubwa na kufanya nao mazungumzo kwa lengo la kurejesha na kuinua sekta ya
michezo hapa nchini.
Alieleza kuwa miongoni
mwa hatua za awali alizozichukua ni kuanzisha kwa Idara ya Michezo na Utamaduni
katika Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, kuazisha mashindano ya riadha ya
Wilaya, kugawa vifaa pamoja na mambo mengineyo.
Aidha, Dk. Shein
alieleza kuwa katika kuendeleza na kuimarisha shughuli za michezo na utamaduni katika skuli, Serikali itaendelea
kutilia mkazo utekelezaji wa mipango ya kuimarisha michezo na sanaa ukiwemo
Mpango wa Sport 55 na kupongeza hatua hiyo.
Akielez mipango ya
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya michezo alisema
kuwa Serikali ina mpango wa kujenga uwanja mpya utakaochukua watu 45,000 kwa
wakati mmoja huko katika mji mpya wa Fumba sambamba na imeshaamua kujenga kiwanja kimoja cha michezo
katika kila Wilaya Unguja na Pemba na tayari kiwanja kilichopo katika Wilaya ya
Kusini huko Kitogani kimeshakuwa tayari.
Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kutoa pongezi kwa Mwakilishi wa Jimbo la Uzini Mohammed Raza kwa
upendo na uzalendo wake huo wa kuendelea kuunga mkono maendeleo ya sekta mbali
mbali nchini ikiwemo sekta ya michezo na kupelekea kutoa vifaa hivyo kwa Wizara
ya Elimu vikiwemo jezi, mipira, viatu, soksi, kikombe, medali za dhahabu na
fedha, shinguard na vifaa vyenginevyo.
Pia, alitoa pongezi
kwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kwa kuendelza sekta hiyo huku akitoa
wito kwa Wizara hiyo kuangalia uwezekano
wa kuanzisha mashindano katika skuli za
msingi na Sekondari hasa mashindano kwa kutumia
‘Inter houses’.
Nae Waziri wa Elimu an
Mafunzo ya Amali Riziki Pembe Juma alimpongeza
Rais Dk. Shein kwa kuanzisha Idara ya Michezo na Utamaduni katika Wizara
hiyo hatua ambayo imepelekea kuhamasika kwa michezo na kuaza kwa vuguvugu la
michezo kama ilivyokuw kwa siku za nyuma.
Aidha, alitumia fursa
hiyo kumpongeza na kumshukuru Mwakilishi wa Jimbo la Uzini, Mohammed Raza kwa
hatua yake hiyo ya kuonesha mashirikiano makubwa kwa Serikali pamoja na Wizara
hiyo ya Elimu na kumsifu kuwa ni kionozi anaetekeleza ahadi zake kwa vitendo.
Nae Mohammed Raza
alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa ataendelea kuiunga mkono Serikali katika
kuendeleza sekta mbali mbali za maendeleo kwa kutoa misaada yake na kueleza
kuwa ahadi zake zote alizoziahidi atazitekeleza.
Aliongeza kuwa juhudi
hizo anazozichukua ni katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha
Mapinduzi ambayo imesisitiza kuimarishwa kwa michezo, hivyo akiwa kiongozi na
mkerekwetwa katika sekta hiyo ni vyema kuiendeleza na kuiimarisha sekta hiyo
hapa nchini.
Pia, aliwaeleza
wanafunzi ambao ndio walengwa wa vifaa hivyo kuwa mbali ya kucheza michezo
mbali mbali katika skuli zao pia, ni vyema wakajua historia yao sambamba na
kutambua mafanikio yaliopatikana kutokana na Mapinduzi ya Januari 12, 1964.
Sambamba na hayo, Raza
aliahidi kutoa vifaa kwa ajili ya mashindano ya netiball kwa skuli za Unguja na
Pemba huku akisisitiza ahadi yake ya kuzihudumia timu mbili za Mkoa wa Kusini na Kaskazini Pemba zitakazokuja
katika mashindano hayo hapa Unguja ambapo gharama zote za vifaa pamoja na
huduma hiyo zitafikia milioni 25.
Mapema Katibu Mkuu wa
Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Khadija Bakari alisema kuwa Wizara
imeelekeza nguvu zake katika usimamizi na utekelezaji thabiti wa shughuli zote
za elimu zikiwemo utekelezaji wa Mpango wa ‘Sport 55’ unaolenga kuimarisha
michezo katika skuli.
Aidha, aliongeza kuwa
mikakati maalumu imeandaliwa na itatekelezwa kuanzia ngazi za skuli katika
kurejesha shughuli zinzowajenga wanafunzi kuwa wakakamavu, wenye nidhamu na
maadili mema, wanaofahamu mila, silka na desturi njema za Zanzibar.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment