Habari za Punde

Mawaziri wa Umoja wa Nchi za Mashariki na Kusini Mwa Afrika Kukutana Zanzibar.


BARAZA la Mawaziri kutoka Umoja wa Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika la Udhibiti Utakasishaji Fedha Haramu (The East and Southern Africa Anti Money Laundering Group-ESAAMLG), linatarajia kukutana 

Tanzania tarehe 08 Septemba 2017 mjini Zanzibar.
Taarifa iliyotolewa na kitengo cha mawasiliano serikalini, Wizara ya Fedha na Mipango, imesema mkutano huo umepangwa kufanyika katika hoteli ya 

Zanzibar Beach Resort Mazizini nje kidogo ya manispaa ya Zanzibar.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mkutano huo utatanguliwa na ule wa maafisa waandamizi (Makatibu wakuu), utakaoanza Septemba 2 hadi 6, mwaka huu katika ukumbi wa hoteli hiyo.

Katika mkutano huo, pamoja na masuala mbalimbali yatakayojadiliwa, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, itatumia fursa hiyo kuwasilisha taarifa ya hatua iliyofikia katika utekelezaji wa mpango wa chombo cha kimataifa kinachoshughulikia udhibiti wa utakatishaji wa fedha haramu, “The Financial Action Task Force (FATF) ulioasisiwa mwaka 2009.

Mpango huo ulizitaka nchi wanachama kufanya tathmini ya utekelezaji wa maazimio yaliyainishwa kwenye FATF, katika maeneo mbalimbali ya kisheria, kisera, miongozo ya kitaasisi zikiwemo sekta za fedha na maeneo ya ushirikiano wa kimataifa.

Lengo ni kubaini jinsi nchi wanachama zilivyojipanga katika kudhibiti suala la utakasishaji fedha haramu na ufadhili wa ugaidi (Anti-money Laundering and Combating the Financing of Terrorism).

Katika mkutano huo, mbinu na mikakati mbalimbali itakayosaidia kudhibiti utakasishaji fedha haramu na ufadhili wa ugaidi zitajadiliwa, hatua ambayo italeta matokeo chanya na kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi na kufikia maendeleo tarajiwa katika nchi wanachama ikiwemo Tanzania.

Tanzania ni miongoni mwa nchi waanzilishi wa umoja huo ulioasisiwa jijini Arusha mwaka 1999. Nchi nyengine ni Uganda, Kenya, Mauritius, Namibia, Seychelles na Swaziland ambazo zilisaini makubaliano (Memorandum of Understanding-MOU).

Hatua ambayo ilipelekea Makao Makuu ya Sekretariati ya Umoja huo wenye nchi wanachama 18, ambazo ni Angola, Botswana, Ethiopia, Kenya, Lesotho, Madagascar, Malawi, Mauritius, Msumbiji, Namibia, Rwanda, 
Afrika Kusini, Swaziland, Seychells, Tanzania, Uganda, Zambia na Zimbabwe kuwa jijini Dar es Salaam Tanzania.

Kwa sasa Tanzania ndio Mwenyekiti wa umoja huo kwa kipindi cha mwaka mmoja, baada ya kupokea uenyekiti kutoka Jamhuri ya Zimbabwe iliyomaliza muda wake mwezi huu wa Agosti 2017 ambapo Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (MB), ambae pia ni Mwenyekiti (President of the Council) atakaeongoza mkutano huo.

IMETOLEWA NA:
KITENGO CHA MAWASILIANO SERIKALINI
WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO-TANZANIA
29 AGOSTI 2017      

  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.