Habari za Punde

Rais Dk Shein, Awapongeza Wanafunzi Waliofaulu Kidato cha Nne na Sita Zanzibar.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                                                       17.10.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewapongeza wanafunzi wa Zanzibar waliopata Daraja la kwanza wa Kidato cha Nne na Kidato cha Sita na kuwaeleza kuwa elimu haina mbadala.

Hayo aliyasema leo wakati akizungumza na wanafunzi waliofaulu Daraja la Kwanza katika mitihani ya taifa ya Kidato cha Nne Ockoba 2016 na Kidato cha Sita Mei 20017, katika hafla iliyofanyika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi, Kikwajunu mjini Zanzibar, ambapo pia, Dk. Shein aliwaandalia chakula maalum cha mchana wanafunzi hao.

Hafla hiyo imehudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali idd, Mawaziri, Manaibu Mawaziri, Makatibu wakuu na watendaji wengine wa Serikali, Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar tokea awamu yake ya Kwanza ya uongozi hadi hivi leo imekuwa ikitilia mkazo sekta ya elimu.

Alisema kuwa Serikali imechukua uwamuzi wa makusudi wa kutangaza elimu bure kwa lengo la kuwataka vijana wote wenye uwezo na wasio na uwezo waweze kusoma na kupata elimu inayohitajika huku akieleza kuwa ongezeko la wanafunzi waliofanya vizuri mwaka huu ni kubwa ikilinganishwa na miaka ya nyuma.

Aliwaeleza wanafunzi hao kuwa bado kazi ya kusoma wanayo ambayo ni kazi ngumu na kuwataka waongeze jitihada kwani hakuna kazi ngumu kama kusoma lakini akawasibitishia kuwa wataiweza licha ya ugumu uliopo.

Aidha, aliwataka wanafunzi hao kwa wale watakaopata fursa ya masomo kwa kwenda nje ya nchi wakumbuke kurudi nyumbani baada ya kumaliza masomo yao ili waje kuitumikia nchi yao “Mtu kwao ndio ngao”, alisisitiza Dk. Shein.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alitangaza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mwaka huu itatoa nafasi 15 za ufadhili wa masomo kutokana na wingi wa wanafunzi mwaka huu, kwani mwaka jana ilitoa nafasi 10 kama hizo.

Nae Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Riziki Pembe Juma aliwapongeza wanafunzi hao na kuwataka kuongeza bidii sambamba na kuachana na vishawishi vya aina zote ambavyo havitowapelekea kufikia malengo waliyojipangia.

Mapema Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Khadija Bakari Juma kwa niaba ya Wizara hiyo alitoa pongezi kwa Dk. Shein kwa kutoa mwaliko huo rasmi kwa mara nyengine tena hivyo kutimiza ahadi ya kukutana na uongozi wa Wizara pamoja na wanafunzi waliofanya vizuri na kuwapongeza pamoja na kuwashauri.

Alieleza kuwa hatua hiyo inathibitisha kwa kiasi gani Rais Dk. Shein anathamini, anajali na yupo tayari kwa dhati ya moyo na yuko tayari kulisimamia suala la utoaji wa elimu bora kwa wanafunzi wa Zanzibar na hasa walio wanyonge.

Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa wanafunzi waliohudhuria katika hafla hiyo ni 328 waliofaulu kwa kiwango cha Daraja la Kwanza kutoka katika skuli mbali mbali za Zanzibar za Serikali na Binafsi.

Aliongeza kuwa Miongoni mwa wanafunzi 240 ni wa Kidato cha Nne ambao ni sawa na asilimia 1.76 ya wanafunzi 13,647 waliofanya mtihani wa Kidato cha Nne mwaka 2016 wakiwemo wanaume 6,051 na wanawake 7,596.

Aidha, alieleza kuwa ufaulu huo ni ongezeko la wanafunzi 121 ikilinganishwa na wanafunzi 119 waliofaulu kwa kiwango cha Daraja la Kwanza Kidato cha Nne kwa mwaka 2015.

Sambamba na hayo, Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa wanafunzi 88 wa Kidato cha Sita wamefaulu kwa Kiwango cha Daraja la Kwanza ambao ni sawa na asilimia 6.2 ya wanafunzi 1,504 waliofanya mtihani wa Kidato cha Sita Mei 2017.

Kwa maelezo ya Katibu Mkuu huyo, miongoni mwao wanafunzi 744 ni wanawake na wanafunzi 760 ni wanawake ambapo ufaulu huo ni ongezeko la wanafunzi 38 ikilinganishwa na wanafunzi 50 waliofaulu Daraja la Kwanza mwaka 2016.

Pamoja na hayo, Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa mafanikio hayo yametokana na juhudi mbali mbali za uongozi wa Wizara ya Elimu, walimu, wanafunzi, wazazi na jamii kwa ujumla.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.