Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk Shein Azungumza na Balozi wa Oman na Indonesia Ikulu Zanzibar.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
 Zanzibar                                                                                                             24.11.2017
---
SERIKALI ya Oman imeahidi kuendeleza ushirikiano na uhusiano wa kidugu na kihistoria uliopo kati yake na Zanzibar sambamba na kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta za maendeleo.

Balozi wa Oman nchini Tanzania Ali Abdalla Al Mahruqi aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar alipofika kwa ajili ya kujitambulisha na kufanya mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.

Katika mazungumzo hayo, Balozi huyo wa Oman alimuhakikishia Dk. Shein kuwa Oman itaimarisha zaidi uhusiano uliopo kati yake na Zanzibar na kupongeza juhudi zinazochukuliwa na pande zote mbili katika kuendeleza uhusiano na ushirikiano huku akieleza dhamira ya Serikali ya Oman kushirkiana na Zanzibar kuendeleza sekta ya elimu, afya, uvuvi, utamaduni, gesi na mafuta.

Aidha, Balozi Al Mahruqi alitumia fursa hiyo kutoa shukurani na pongezi kutoka kwa Sultan Qaboos kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wananchi wake kwa namna walivyoupokea ujumbe wa Serikali ya Oman uliofika Zanzibar kwa kutumia meli maalum ya Sultan Qaboos iitwayo “Fulk Al Salamah” iliyofika Zanzibar hivi karibuni.

 Nae Dk. Shein kwa upande wake alitoa shukurani kwa Sultan Qaboos bin Said kwa juhudi zake anazoendeleza katika kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya Oman na Zanzibar.

Dk. Shein alieleza dhamira ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuhakikisha kuwa uhusiano huo wa kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na Oman unaendelezwa kwa manufaa ya pande mbili hizo.

Aidha, Dk. Shein alitoa shukurani kwa juhudi zinazoendelezwa na Serikali ya Oman katika kuiunga mkono Zanzibar kwenye sekta ya afya, elimu, utamaduni pamoja na uhifadhi wa Mji Mkongwe huku akisisitiza uhusiano kati ya chuo kikuu cha (SUZA) na Chuo Kikuu cha Sultan Qaboos cha Oman.

Alisema kwamba hivi sasa nchi mbili hizo zina nafasi ya kushirikiana katika sekta ya mafuta na gesi asilia kutokana na Oman kupiga hatua kubwa pamoja na uzoefu na utaalamu hali ambayo itaisaidia Zanzibar kupata kujifunza kutoka kwa wataalamu wa nchi hiyo na kukuza zaidi ushirikiano na uhusiano uliopo.

Sambamba na hayo, Dk. Shein pia, alieleza haja ya Zanzibar kushirikiana na Oman katika kuimarisha sekta ya uvuvi ambapo tayari Zanzibar imeanzisha Kampuni yake ya Uvuvi na kuhitaji utaalamu na uzoefu kutokana Oman kwa kuzingatia kuwa wananchi na Serikali ya nchi hiyo zimepiga hatua hatika sekta hiyo.

Dk. Shein alitoa shukurani kwa Serikali ya Oman kwa azma yake ya kulifanyia ukarabati jengo la Beit al Ajab pamoja na kukubali kulifanyia ukarabati jengo la “People Palace”  kwani nyumba hizo historia kubwa kwa Zanzibar huku akiahidi kuzifikisha salamu za shukurani kwa wananchi kutoka kwa Sultan Qaboos kufuatia mapokezi ya ugeni uliokuja kwa meli ya  “Fulk Al Salamah”

Wakati huo huo, Rais Dk. Shein alikutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa  Indonesia nchini Tanzania Rotlan Pardede, Ikulu mjini Zanzibar ambapo Balozi huyo alieleza azma ya nchi yake kuimarisha ushirikiano na Zanzibar katika kuimarisha sekta ya elimu ambapo nchi hiyo imeahidi kutoa ufadhili kupitia progmramu maalum.

Aidha, Balozi Pardede alimueleza Dk. Shein kuwa Serikali yake itahakikisha inashirikiana na Zanzibar katika kuendeleza na kuliimarisha zao la mwani pamoja na kuimarisha sekta ya uvuvi huku akipongeza mashirikiano yaliopo katika sekta ya biashara kati ya Zanzibar na Indonesia ambapo ndani ya miaka mitatu iliyopita wafanyabiashara zaidi ya 400 walifanyabiashara nchini humo.

Balozi Pardede alitumia fursa hiyo kutoa mwaliko kwa Zanzibar katika Mkutano maalum kati ya nchi hiyo na nchi za Afrika mwezi April mwakani, mkutano ambao utajikita katika masuala ya uchumi, kilimo, mikakati ya kuimarisha viwanda na ujenzi, teknolojia, na masuala ya kifedha hatua ambayo itazidisha uhusiano kati ya nchi hiyo na Zanzibar.

Nae Dk. Shein kwa upande wake alimueleza Balozi huyo kuwa Zanzibar na Indonesia  zina historia na ushirikiano mkubwa kabla ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 ambapo yalizidi kuimarishwa kuanzia mwaka 1964 na kumuahidi kuwa Zanzibar itaendeleza uhusiano na ushirikiano huo.

Dk. Shein alitoa pongezi kwa mafanikio makubwa yaliofikiwa na nchi katika kuimarisha sekta ya kilimo hasa kilimo cha mpunga, uvuvi, utalii, biashara na sekta nyengine ambapo mbali ya mafanikio katika sekta ya kilimo pia ina uzoefu wa kulisarifu zao la mpunga kwa kulifanya vyakula mbali mbali vyenye ladha tofauti.

Dk. Shein katika mazungumzo hayo alisisitiza haja ya Serikali ya Indonesia kuiunga mkono Zanzibar katika sekta ya uvuvi kutokana na mafanikio iliyopata nchi hiyo .

Alisisitiza kuwa ni vyema ikiwa Zanzibar itaimarisha ushirikiano katika kuendeleza uvuvi wa kisasa hasa katika kufuata makubaliano ya  mkutano wa Jumuiya ya Nchi zinazopakana na Bahari ya Hindi (IORA) uliofanyika mjini Jakata Indonesia mnamo mwezi Machi mwaka huu ambapo Dk. Shein alihudhuria.

Aidha, Dk. Shein alifuirahishwa na dhamira ya Indonesia ya kutaka kushirikiana na Zanzibar katika kilimo na usarifu wa zao la mwani ambapo Balozi huyo alieleza kuwa nchi yake inajipanga kimarisha ushirikiano katika zao la mwani ambapo badala ya kuliuza kama mali ghafi litatengenezewa vitu mbali mbali tena hapahapa nchini.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza haja ya nchi hiyo kushirikiana na Zanzibar katika kuimarisha sekta ya utalii hasa ikizingatiwa kuwa nchi hiyo imepiga hatua kubwa katika sekta hiyo na kusisitiza haja kwa Wizara zinazohusiana na utalii kati ya nchi mbili hizo kuwa na mashirikiano sambamba na kuwa na uhusiano kati ya kisiwa cha kitalii cha Bali kiliopo nchini humo na Zanzibar.

Pia, Dk. Shein alieleza haja ya kuiamrisha uhuasiano kati ya vyuo vikuu vya nchi hiyo pamoja na vyuo vya Zanzibar kikiwemo chuo kikuu cha Taifa cha (SUZA), huku viongozi hao kwa pamoja wakisisitiza haja ya kutembeleana kati ya viongozi na wananchi wa nchi mbili hizo kwa lengo la kuimarisha uhusiano, utaalamu na kujifunza mambo mbali mbali.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.