Habari za Punde

Maadhimisho ya Siku ya Watu Wenye Ulemavu Duniani Yaadhimisha Katika Kijiji cha Uzini Zanzibar.

Sehemu ya Maandamano ya Walemavu yaliofanyika Uzini, wilaya ya Kati, mkoa wa Kusini Unguja wakati wa maadhimisho ya siku ya walemavu duniani
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipata maelezo ya kikundi cha Walemavu kutoka Mwembe Makumbi kinachojishughulisha na kutengeneza viatu vya ngozi wakati alipotembelea maonyesho ya walemavu katika uwanja wa Skuli ya Uzini wakati wa maadhimisho ya siku ya walemavu duniani ambayo kitaifa yalifanyika mkoa wa Kusini,Unguja.
Makamu wa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akihutubia wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Watu Wenye Ulemavu Duniani, yaliadhimishwa katika viwanja vya Skuli ya Uzini Wilaya ya Kazi Unguja.  
Sehemu ya Watu wenye ulemavu wakimsikiliza kwa makini Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipokuwa akihutubia kwenye kilele cha siku ya kimataifa ya maadhimisho ya watu wenye ulemavu yaliofanyika kwenye viwanja vya skuli ya Uzini, wilaya ya Kati mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akikabidhi kiti maalum cha kutembelea walemavu (Wheel Chair) kwa   Bi. Hidaya Shaib Muombwa ambacho kilipokelewa na ndugu yake kwa niaba wakati wa kilele cha maadhimisho ya siku ya walemavu duniani katika viwanja vya Skuli ya Uzini, mkoa wa Kusini Unguja
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akimkabidhi mafuta maalum ya ngozi Bw. Hussein Ussi Ali wakati wa kilele cha maadhimisho ya siku ya walemavu duniani katika viwanja vya Skuli ya Uzini, mkoa wa Kusini Unguja. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)







Na. Mwandishi OMR.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ameitaka jamii kuhakikisha kuwa watu wenye ulemavu  hawaachwi nyuma kwenye nyanja zote za maendeleo.

Makamu wa Rais ameyasema hayo leo wakati wa maadhimisho ya Siku ya Watu wenye ulemavu duniani iliyofanyika mkoa wa Kusini, Unguja, Zanzibar.

Akihutubia mamia ya watu wenye ulemavu na wasio na ulemavu kwenye kwenye viwanja vya Skuli ya Uzini, Makamu wa Rais alisema tumejumuika leo hapa  kuungana na wenzetu duniani kote  kuadhimisha kilele cha siku ya Kimataifa ya Watu wenye Ulemavu Duniani ambayo imebeba kauli mbiu isemayo 
 “Mabadiliko kuelekea jamii Jumuishi na Maendeleo Endelevu kwa wote”
Ujumbe huu unalenga kuhakikisha kuwa watu wenye ulemavu wanajumuishwa katika mipango yote ya maendeleo ili kuweza kufikia malengo endelevu ya dunia ifikapo mwaka 2030 pia inakwenda sambamba na Dira ya Maendeleo ya Zanzibar ya 2020; Ilani ya Chama Tawala na mpango wa kukuza Uchumi na kupunguza Umasikini Zanzibar (MKUZA III) ambapo maswala ya watu wenye ulemavu yamezingatiwa.

Tanzania iliridhia mkataba wa kimataifa wa haki za watu wenye ulemavu ambao umeweka misingi madhubuti  wa utekelezaji wa masuala mbali mbali kwa ajili ya watu wenye ulemavu, ikiwemo; Usawa, Ushirikishwaji kikamilifu katika mipango ya hifadhi ya jamii na kupunguza umasikini na kuwapatia huduma pamoja na kufanya kazi na taasisi zinazoshughulikia masuala ya watu wenye ulemavu, alisema Makamu wa Rais.

Kwa upande wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar itaendelea kuweka mipango thabiti na mathubuti yenye kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata haki za kisiasa, kiuchumi, kijamii na fursa sawa kama wengine na kuahikisha watu wenye ulemavu wanashiriki kikamilifu katika ngazi mbali mbaliza uongozi za kitaifa.

Makamu wa Rais alitoa rai kwa kusema “kuanzia leo kila mmoja miongoni mwetu awe askari wa mwenzie katika kuhakikisha kuwa tunalinda haki na usawa wa watu wenye ulemavu”.

Makamu wa Rais aliwaasa wanafamilia kutoficha  maovu wanayofanyiwa watu wenye ulemavu, alisema Serikali kwa nguvu zote inakemea vitendo  vya ubakaji na udhalilishaji kwa watu wenye ulemavu kwani si vitendo vya kiungwana hata kidogo na kuvitaka vyombo vya ulinzi na usalama kuwashughulikia kikamilifu wahalifu hawa na wakithibitika wafikishwe kwenye vyombo vya sheria ikiwemo mahakama na kutoa adhabu kali dhidi ya wale watakaobainika.

Mwisho, Makamu wa Rais alisema Serikali kwa kushirikiana na Wadau wengine wa Maendeleo  pamoja na wananchi itaendelea kuhakikisha kuwa ‘digital technology’ inakuwa rafiki kwa walemavu hususan katika kuwawezesha kupata elimu, vitendea kazi katika maendeo yao pamoja na kuhakikisha wanafikia kirahisi huduma zote za kijamii.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.