Habari za Punde

Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Autaka Uongozi Mpya wa Wazazi Kujipanga Baada ya Kupata Uongozi Mpya.

Na. Rajab Mkasab Ikulu.
Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk.Ali Mohamed Shein ameutaka Umoja wa Wazazi Tanzania kujipanga vyema baada ya kupata safu nzuri ya uongozi kuhakikisha Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinaendelea kukamata dola kwa upande wa Tanzania Bara na Zanzibar.

Makamo Mwenyekiti huyo ambaye pia, ni na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Shein aliyasema hayo, huko katika ukumbi wa Jakaya Mrisho Kikwete mjini Dodoma wakati akiufunga Mkutano Mkuu wa Umoja wa Wazazi wa Tanzania ulioenda sambamba na uchaguzi mkuu wa Umoja huo.

Dk. Shein alieleza kuwa ana matumaini makubwa kuwa Umoja huo utaiweza kazi hiyo kwa mashirikiano ya pamoja kutokana na uzoefu wao mkubwa walionao sambamba na mafanikio makubwa yaliopatikana ndani ya Umoja huo.

Aliwapongeza Wajumbe wa Umoja huo kwa kumchagua kiongozi Mchumi na kumtaka Mwenyekiti mstaafu Abdallah Majura Bulembo kupumzika kwa kuiendeleza CCM kutokana na kuwa bado nafasi yake ya Ubunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anayo.

Aidha, aliwapongeza Wajumbe hao kwa kuzingatia vyema maelezo ya Mwenyekiti wa CCM Taifa Dk. John Pombe Magufuli kwa kuwachagua na kupata viongozi bila ya kutumia hila na hilba na hatimae kuwapata viongozi walio bora.

Makamu Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumpongeza Mwenyekiti mstaafu kwa kutumia juhudi na nguvu zake kubwa sana katika kuuimarisha Umoja huo ambayo ulikuwa taabani hapo siku za nyuma.

Rais Dk. Shein alimpongeza Rais Magufuli kwa maelekezo aliyoupa Umoja huo ya kuwachagua viongozi walio bora na walioimara ili waweze kuiendeleza Umoja huo uzidi kuimarika  huku akisisitiza haja ya kuifanyia kazi hotuba yake ya ufunguzi aliyoitoa kwani ina maelekezo mengi na mambo mazito.

Aliongeza kuwa Mwenyekiti mstaafu wa Umoja huo ameweza kuifikisha mahali pazuri sana na Dk. Mndolwa Benard Edmund anapokea kijiti kutoka kwake na kuendelea kuongoza pale alipopaacha yeye.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein aliupongeza Umoja wa Wazazi wa Tanzania kwa kuwa na mitaji pamoja na miradi waliyoanzisha ukiwemo mradi wa kujenga jengo kubwa la ghorofa kumi na nne 14, kwa ajili ya kitega uchumi, mradi ambao utatumia vyanzo vya mapato ya Jumuiya ya Wazazi.

Aidha, Dk. Shein amewataka viongozi wa Umoja huo wakiwemo wale wastaafu kushirikiana na viongozi wapya  huku akiwataka viongozi hao wapya kujidhatiti katika kipindi cha miaka mitano kwa kushirikiana ili Jumuiya hiyo izidi kupata mafanikio zaidi yaliokusudiwa katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM na katika nyaraka nyengine za chama hicho ukiwemo Mpango Mkakati wa mwaka 2017-2022.

Pia, Dk. Shein aliwataka wale wote ambao wamegombania nafasi mbali mbali katika Jumuiya hiyo lakini kura zao hazikutosha wasikate tama kwani uchaguzi ni utaratibu wa kidemokrasia na huchaguliwa mtu kwa sifa zake, uwezo na viwango vyake na jinsi anavyoshirikiana na wenzake hivyo aliwataka wakusanye nguvu ili waje kugombania katika chaguzi zijazo.

Nae Mwenyekiti mpya wa Umoja huo Dk. Mndolwa Benard Edmund aliwaahidi wana Umoja huo kuwa hatowaangusha na kusisitiza kuwa aliomba nafasi hiyo ili apate kuwatumikia kwa moyo wake wote, akili na uwezo wake wote katika kuhakikisha CCM inaendela kushinda chaguzi zote zikiwemo za Serikali za mitaa za mwaka 2019.

Mwenyekiti huyo alieleza atahakikisha kuwa Umoja huo unajitegemea kutokana na uzoefu wake wa taaluma ya uchumi na kueleza kuwa atahakikisha anasimamia utawala bora na kupambana na rushwa na kuhakikisha katika kipjndi kifupi maslahi ya wafanyakazi wa Umoja huo yanasimamiwa na madeni hasa ya ndani yanakwisha.

Mapema akitangaza matokeo ya uchaguzi wa Umoja huo Jerry Slaa alimtangaza Dk. Mndolwa Benard Edmund mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti kwa kupata asilimia 68.06 za kura zote na Haidar Haji Abdallah kuwa Makamo Mwenyekiti.

Wengine waliochaguliwa katika nafasi tatu za Wajumbe wa Baraza Kuu kwa upande wa Tanzania Bara ni Lulu Abbas Mtemvu, Sudi Kassim Sudi, Stephan Hiral Ngonyani na nafasi kwa upande wa Zanzibar ni Habiba Ali Mohammed, Ali Issa Ali na Christina Joram Antoni.

Kwa upande wa nafasi za Ujumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kwa Tanzania Bara waliochaguliwa ni  Namelock Edward Sokoine, Paul Herman Kirigini na Mohamed Nassoro Ngingite na kwa upande wa Zanzibar ni Amina Ali Mohamed na Suleiman Juma Kimea na nafasi Vijana aliechaguliwa ni Omary Ajili Kalolo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.