STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 5.01.2018
RAIS wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema kuwa miongoni
mwa malengo ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 ni kufanya hali za maisha
ya Wazanzibari kuwa bora na ujenzi wa soko la Tibirinzi ni miongoni mwa malengo
hayo na sio kichocheo cha kubaguana kwa vyama, dini, jinsia au mahala mtu
anapotokea.
Dk. Shein
amesisitiza kuwa jengo hilo jipya la soko ni ukombozi kwa wakulima,
wafanyabiashara, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali pamoja na wananchi wote kwa
jumla kwa kuweza kuongeza kipato chao
ili maisha yao yaweze kuwa bora.
Rais Dk.
Shein aliyasema hayo leo mara baada ya kulizindua soko jipya la Tibirinzi Chake
Chake Pemba.
Dk. Shein
alisema kuwa soko hilo si vyema likahusishwa na masuala ya kisiasa kwani ni soko
la watu wote wa vyama vyote, dini zote na jinsia zote huku akiwataka
wafanyabiashara watakaolitumia soko hilo kuleta bidhaa zenye ubora
zitakazolingana na hadhi ya soko hilo.
Alisema kuwa ujenzi wa soko hilo ni
katika hatua za kutafsiri Mapinduzi ya mwaka 1964 kwa vitendo kwa kuwaletea
wananchi maendeleo zaidi bila ya ubaguzi.
Alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatekeleza
Sera mbali mbali zikiwemo zinazolenga kuinua kipato cha wananchi na kupunguza
umasikini…
Sambamba na hayo, Dk. Shein
alisisitiza haja ya kulitunza na kulienzi soko hilo ikiwa ni pamoja na
kudumisha usafi wa soko hilo kwani usafi ni jambo la lazima na halina mbadala.
Dk. Shein alitumia fursa hiyo
kueleza mafanikio sambamba na azma ya Mapinduzi Matukufu ya Januri 12, 1964
ambayo yamewakomboa wananchi wa Zanzibar na kukata minyororo ya chuki na
udhalimu sambamba na kunyanyaswa.
Alieleza madhumuni makubwa ya
Mapinduzi ya Zanzibar ni kuwa huru na hatua ambayo imepekea kupanga mambo bila
ya kuingiliwa na mtu na kuweza kuongoza nchi sambamba na kuandaa mipango ya
muda mrefu na muda mfupi na wakati.
Alieleza kuwa Zanzibar imepata maendeleo
makubwa katika kukuza uchumi wake ndani ya kipindi cha miaka 54 huku akieleza
kuwa mabadiliko makubwa ya kiuchumi,
sera ya serikali maisha ya watu ambayo yote hayo ni maendeleo.
“Leo naambiwa ndege zinazokuja
Pemba hivi sasa hazitoshi, meli hazitoshi watu wanasafiri kila leo hayo yote ni
maendeleo na kukua kwa uchumi.. jengo hilo ni lazima tulipe heshima yake”
Alisema Dk. Shein.
Nae Waziri wa Kilimo, Maliasili,
Mifugo na Uvuvi Hamad Rashid Mohammed alieleza kuwa kuna kila sababu ya
kumuenzi na kumuombea dua Rais Dk. Shein kwa maendeleo makubwa sambamba na
juhudi anazozichukua katika kuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar.
Waziri Rashid alisema kuwa maendeleo
yanayoonekana na kwa mara ya kwanza katika historia wafanyakazi wameweza
kulipwa mshahara mara mbilili wanaopata, kuzalisha mpunga tani 39 elfu, kuwepo
na mchele kutoka Zanzibar pamoja na maendeleo mengineyo ikiwemo kuimarika kwa
miundombinu.
Aliongeza kuwa Rais Dk. Shein kuwa
Zanzibar imebaki salama kutokana na hekima yake na hakuna mpasuko na kumekuwa
na amani kubwa kwani huwezi kupata maendeleo kama hakuna amani ya nchi.
Alieleza kuwa Dk. Shein ni kiongozi
anaetaka kila mmoja kutoa maamuzi na kumshirikisha kufanya hivyo na ndicho
kilichomfanya Dk. Shein kuweza kuwatumikia watu tena bila ya ubaguzi.
“Kina mzee Karume wasingeweza
kupindua nchi kama wasingekuwa na nia nzuri… Mwenyezi Mungu peke yake ndie
anaechagua kiongozi.. kwani katika mazingira haya nani angelijua kuwa Hamad
Rashid angekuwa Waziri wa Kilimo…unapomkuta kiongozi anajenga fitna kwa watu
anajenga fitna kwa watu, unapomkuta kiongozi anajenga makundi hata salamu
alaykum haitikiii ni kweli huyu mtu wa peponi?”,aliuliza Hamad Rashid.
Waziri Rashid aliwataka baadhi ya wananchi
kisiwani humo kuwacha siasa na badala yake washughulikie mambo ya msingi na
yenye kuleta maendeleo huku akieleza kuwa Serikali inalengo la kujenga masoko
makubwa mawili huko Malindi mjini Zanzibar na soko jengine litajengwa huko
kiswani Pemba.
Mapema Katibu Mkuu wa Wizara ya
Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Joseph Abdalla Meza alieleza kuwa soko hilo
ni kati ya masoko manne yaliojengwa Zanzibar kupitia Programu ya Miundombinu ya
Masoko, Uongezaji Thamani na Huduma za Kifedha Vijijini (MIVAP) inayogharamiwa
na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya
Kilimo (IFAD) na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Aliongeza kuwa program hiyo
inasimamiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na
Uvuvi kwa Zanzibar na kueleza kuwa ujenzi wa soko hilo ulianza mwezi wa Aprili
2016 ambapo wazabuni 12 waliomba kufanya kazi hiyo na baada ya tathmini Kampuni
ya ZECCON LIMITED ya Zanzibar ndiyo iliyoibuka mshindi na kupata tenda hiyo na
kuingia mkataba wa ujenzi kwa gharama za TZS Milioni 972.2 ambapo kati ya hizo
milioni 48.6 zimetolewa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Alisema akuwa soko hilo lina
vibaraza 76 vitakavyokabidhiwa kwa wafanyabiashara ambapo soko hilo lina chumba
cha baridi kwa ajili ya kuhifadhia samaki na chumba maalum kilichotengwa
kuwekewa mtambo wa kutengenezea barafu ambao utawasaidia wavuvi kutumia barafu
hizo wakati wakiwa baharini.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment