Habari za Punde

KMKM yaingia mkataba wa Ujenzi wa Nyumba ya Makaazi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kisiwani Pemba

Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Nd. Shaaban Seif  Mohamed wa kwanza Kushoto pamoja  na CDR- Hamadi Masoud Khamis  wa Kikosi cha Kuzuia Magendo Zanzibar {KMKM} wakitia saini Mkataba wa ujenzi wa Nyumba ya Makaazi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Kisiwani Pemba hafla iliyofanyika Vuga Mjini Zanzibar.
Picha na – OMPR – ZNZ.

Na Othman Khamis, OMPR
Wizara ya Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar leo imetiliana saini Mkataba na Kikosi cha Kuzuia Magendo Zanzibar {KMKM} juu ya Ujenzi wa Nyumba ya Makaazi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kisiwani Pemba.
Ujenzi wa Nyumba hiyo itakayojengwa sambamba  na zile za Wafanyakazi wa Mheshimisha Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar utafanyika katika eneo la Kijiji cha Pagali kiliopo Magharibi ya Mji wa Chake Chake Pemba.
Kwa upande wa Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Saini hiyo imetiwa na Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Nd. Shaaban Seif  Mohamed wakati ule wa Kikosi cha Kuzuia Magendo Zanzibar imetiwa na CDR- Hamadi Masoud Khamis hafla iliyofanyika Vuga Mjini Zanzibar.
Akizungumza mara baada ya utiaji saini hiyo Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Nd. Shaaban Seif  Mohamed  alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeamua kujenga Nyumba  ya Makaazi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ili kumjengea mazingira mazuri ya uwajibikaji anapokuwa Kisiwani Pemba.
Alisema  Ujenzi huo licha ya kukabidhiwa Kikosi cha KMKM  katika muelekeo wa kuzijengea heshima Taasisi za Serikali  mbele ya Umma lakini pia zinastahiki kupewa kazi hiyo kutokana na uwajibikaji wao mkubwa kubwa unaofahamika.
Naye kwa upande wake  CDR – Hamadi Masoud Khamis aliishukuru  Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa kukiamini Kikosi hicho kukabidhiwa jukumu hilo licha ya kazi nyengine ya ulinzi kilichokabidhiwa na Taifa.
Kamanda Hamad  kwa niaba ya Mkuu wa KMKM na Wapiganaji wa Kikosi hicho aliahidi kwamba kazi waliyokabidhiwa watahakikisha wanaitekeleza na kuimamilisha katika kuzingatia muda waliopangiwa.
Ujenzi wa Nyumba ya Makaazi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Pagali Chake chake Pemba unatarajiwa kugharimu jumla ya Shilingi za Kitanzania Bilioni Moja, Mia Sita na Sitini na Nne, Laki Moja, Thamanini na Tisa, Mia Saba na Thamanini na Tisa { 1,664,189,789/-}.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.