Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Balozi Seif Ali Iddi akihutubia wakati mkutano na Uongozi wa Benki ya Dunia kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika miradi ya Maendeleo mara baada ya tafrija ya pamoja na Uongozi huo.iliofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Sea Cliff Kama Zanzibar.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mh. Mohamed Aboud Mohamed akishukuru ushirikiano uliopo kati ya SMT,SMZ na Benki ya Dunia uliosaidia kuzikomboa Kaya Maskini Nchini.
Mkurugenzi Mkuu wa Mfukowa Maendeleo ya Jamii Tanzania {TASAF} Nd. Ladislaus Mwamanga akisisitiza nia ya Tasaf kuendelea kuzisaidia Kaya Maskini Nchini.
Mkurugenzi na Mkuu wa Mtandao wa Masuala ya Kijamii na Ajira wa Benki ya Dunia Bwana Michal Rutkowski akitoa salamu kwenye tafrija hiyo na kupongeza miradi ya Tasaf jinsi inavyotekelezwa vyema Visiwani Zanzibar.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliyevaa Suti na Miwani akiwa katika tafrija ya pamoja na Ujumbe wa Viongozi wa Benki ya Dunia na Tasaf Tanzania ukiwa Zanzibar kukagua Miradi ya maendeleo ya Jamii inayosimamiwa na Tasaf hapo Hoteli ya Sea Cliff Kama.
Balozi Seif kati kati waliokaa vitini akiwa katika picha ya pamoja na Uongozi wa Benki ya Dunia, Tasaf Tanzania pamoja na Tasaf Zanzibar mara baada ya kumaliza Tafrija hapo Sea Cliff Hoteli Kama,Kulia ya Balozi Seif ni Mkurugenzi wa Benki ya Dunia wa masuala ya Kijamii Bw. Michal Rutkowski, Waziri Mohamed Aboud, Mshauri Mkuu wa WB Bibi Margaret Grosh, kushoto ya Balozi Seif ni Mkurugenzi wa Tasaf Tanzania Nd. Ladislaus Mwamanga, Mkurugenzi wa Masuala ya Kijamii wa WB Bw. Steen Jorgensen na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Pili Mh. Mihayo Juma N’hunga.
Picha na – OMPR – ZNZ.
Na.Othman Khamis OMPR.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ameiomba Benki ya Dunia {World Bank - WB} kuendelea kuiunga mkono Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika harakati zake inazozichukuwa za kuimarisha ustawi wa Wananchi wake hasa wale wa kipato cha chini.
Alisema ustawi wa Jamii unapaswa kujengewa mazingira bora na ya kudumu yatakayowezesha kupatikana kwa nguvu za pamoja ambazo hupatikana kwa mjumuisho wa Serikali Kuu kwa kushirikiana na Wadau wa Maendeleo waliopo Nchini na wale wa nje.
Balozi Seif Ali Iddi alitoa ombi hilo katika Tafrija Maalum iliyoandaliwa kwa ajili ya Ujumbe wa Benki ya Dunia {WB} uliofanya ziara ya Siku Tatu Zanzibar kukagua Miradi ya Maendeleo iliyochini ya Mfuko wa TASAF inayopata msukumo kutoka Benki ya Dunia iliyofanyika Hoteli ya Sea Cliff iliyopo Kama nje kidogo ya Kaskazini ya Mji wa Zanzibar.
Alisema Benki ya Dunia imekuwa Mshirika mkubwa wa Zanzibar katika kuunga mkono miradi ya Kiuchumi na Kijamii inayoanzishwa na Serikali na hata Taasisi za Kiraia jambo ambalo aliuhakikishia Ujumbe wa Taasisi hiyo ya Kimataifa ya Fedha kwamba Miradi inayofadhili itasimamiwa kwa lengo la kufanikiwa vyema.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema miradi yote iliyoanzishwa na Wananchi katika maeneo mbali mbali ya Visiwa vya Unguja na Pemba kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Tanzania {TASAF} na kupata msukumo wa Benki ya Dunia umeleta ukombozi kwa Wananchi waliowengi Nchini.
Alisema hatua hiyo ya mafanikio makubwa yaliyoleta ustawi wa maisha yao katika kujipatia Kipato cha uhakika imekua chachu kwa baadhi ya Vijiji vyengine Nchini kushawishika na kuuomba Uongozi wa Tasaf kuwaingiza katika Programu za Miradi hiyo muhimu.
Balozi Seif alisema awamu ya kwanza ya Miaka Mitano ya Miradi ya Tasaf iliyoanza Mwaka 2000 ikiwa na jumla ya Miradi ya Kiuchumi na Maendeleo 75 Unguja na Pemba imegharimu jumla ya shilingi Bilioni Tatu na kushirikisha Wananchi Laki 135,798.
Alisema mafanikio ya Miradi hiyo imewezesha kuongezeka kwa Miradi ya Tasaf katika Awamu ya Pili iliyoanza Mwaka 2005 hadi 2013 kwa gharama za shilingi Bilioni 12.9 kwa kushirikisha Wananchi Laki 471,346 Unguja na Pemba.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliueleza Ujumbe huo wa Benki ya Dunia kwamba Serikali Kuu katika kuwajengea uwezeshaji Kiuchumi Wananchi wake hasa wale walioko katika mazingira magumu umelenga kuwapunguzia ukali wa Maisha.
Alisema hatua hiyo imepelekea awamu ya Tatu ya Tasaf kuwafaidisha Wananchi hao wanaoishi katika mazingira magumu ambapo Shehia 233 zimeingizwa katika mpango huo kwa kuzihusisha Kaya Maskini 45,881, kati ya hizo Kaya 33,532 hupokea fedha kila baada ya kipindi cha miezi Mitatu.
Balozi Seif alifafanua kwamba mpango huo tayari umeshaanza kuleta mafanikio makubwa kwa Familia za Kaya Maskini kwa vile hali ya upatianaji wa chakula inaanza kuridhisha sambamba na Watoto wa Kaya hizo kuendelea na masomo yao ya Msingi na Sekondari bila ya vikwazo hasa katika upatikanajiwa sare za skuli.
Mapema Mkurugenzi Mkuu wa Mfukowa Maendeleo ya Jamii Tanzania {TASAF} Nd. Ladislaus Mwamanga alisema kazi kubwa inayofanywa na Wananchi wa Zanzibar kwenye miradi ya Maendeleo kupitia programu zinazosimamiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Tanzania {Tasaf} imeleta mafanikio makubwa.
Nd. Mwamanga alisema Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Mfuko huo itaendelea kuongeza nguvu mara dufu katika kuona kundi kubwa la Wananchi walio na kipato duni hasa Vijijini wanaongezewa nguvu za uwezeshaji ili kuondokana na mazingira magumu.
Akitoa salamu kwa niaba ya Ujumbe wa Viongozi hao wa Benki ya Dunia Mkurugenzi na Mkuu wa Mtandao wa Masuala ya Kijamii na Ajira wa Benki ya Dunia Bwana Michal Rutkowski alisema Taasisi hiyo ya Kimataifa ya Fedha haina sababu ya kusua sua katika kuongeza nguvu kwenye miradi ya Tasaf inayoendelea vizuri katika utekelezaji wake.
Bwana Michal alisema Uongozi wa juu wa Benki ya Dunia {World Bank} umefurahishwa na jitihada kubwa zinazochukuliwa na Wananchi walio wengi Visiwani Zanzibar katika utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo ya Jamii inayosimamiwa na Mfuko wa Tasaf Tanzania.
Akimkaribisha mgeni rasmi katika tafrija hiyo Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mh. Mohamed Aboud Mohamed alisema ushirikiano wa karibu uliopo kati ya Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Benki ya Dunia umesaidia kupunguza umaskini kwa baadhi ya Kaya Nchini Tanzania.
Waziri Aboud alisema ushirikiano huo unaendelea kuwa kigezo tosha kinachotoa majibu ya uwepo wa utulivu wa kimaisha kwa Baadhi ya Familia za Kaya hizo jambo ambalo limeleta faraja zaidi kwa watoto wao katika kushiriki vyema masomo yao.
Hii ni mara ya pili kwa Mkurugenzi ambae pia ni Mkuu wa Mtandao wa Masuala ya Kijamii na Ajira wa Benki ya Dunia Bwana Michal Rutkowski na Maafisa wake kutembelea miradi ya maendeleo ya Kijamii inayosimamiwa na Mfuko wa Tasaf Nchini Tanzania.
Ziara ya kwanza ya Bwana Michal na ujumbe wake hapa Tanzania ilifanyika Tarehe 8 Novemba Mwaka 2017 ambapo pamoja na mambo mengine ujumbe huo uliridhika na mafanikio makubwa ya Wananchi katika kuendelesha miradi yao ya Maendeleo.
No comments:
Post a Comment