Habari za Punde

Wanadiaspora Watakiwa Wasiwe Miongoni Mwa Kundi la Wachache Wanaodharau Nchi Zao Kwa Maendeleo Yanayofikiwa na Nchi Nyengine.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akizungumza na Viongozi mbali mbali na Wanadiaspora katika Kongamano la Tano la Diaspora Tanzania lililofanyika leo katika ukuimbi wa Uwanja wa Tibirinzi Chake chake Mkoa wa Kusini Pemba.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amewataka Diaspora kutambua kuwa wana jukumu lililosawa la kuijenga Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mujibu wa nafasi na uwezo walionao, ikiwa kwa kiuchumi au kielimu.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika ufunguzi wa Kongamano la tano la Diaspora linalofanyika huko katika viwanja vya kufurahishia watoto Tibirinzi Chake Chake Pemba.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein aliwataka wanadiaspora katu wasiwe miongoni mwa kundi la wachache wanaodharau nchi zao kwa maendeleo yaliyofikiwa na nchi nyengine.

Alisema kuwa maendeleo ya kweli hayaji kwa kutupiana lawama na hayaji kwa misingi ya utashi bali maendeleo ya kweli yanahitaji bidii na maarifa katika utetekelezaji wa majukumu yao, umoja na mshikamano pamoja na matumizi mazuri ya rasilimali zilizopo.

Aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekamilisha Sera ya Diaspora ambayo ilizinduliwa rasmi tarehe 09 Mei, 2018 kwa lengo la kuhakikisha mipango ya maendeleo.

Pamoja na mambo mengine Rais Dk. Shein alieleza kuwa Sera inaeleza na kufafanua mipango ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuwashirikisha Wanadiaspora katika fursa za kijamii na kiuchumi zilizopo kwa Wanadiaspora na namna bora ya kuzitumia fursa hizo.

Hivyo, Dk. Shein aliiagiza Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Uratibu wa Wazanzibari Wanaoishi Nchi za Nje iliopo katika Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kuhakikisha kwamba kopi ya Sera hiyo inawekwa katika Tovuti ya Idara kwa haraka iwezekanavyo ili Wanadiaspora wengi zaidi wapate kuisoma na kuifahamu.

Pamoja na hayo, alimuagiza Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyeiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Haji Gavu kuunda Jukwaa rasmi la Diaspora la Zanzibar ambalo kabla ya Kongamano la Diaspora Jukwaa hilo likae kwa kupanga taratibu za Kongamano.

“Kila kiumbe kina mapenzi ya nyumbani, na mara nyingi hata wadudu mbali mbali kama nyuki, huwa tayari kujitoa muhanga kwa ajili ya kutetea nyumbani kwao, nyumbani ni nyumbani, anayependa kwao ndie mzalendo halisi”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa hivi sasa suala la kuwashirikisha Wanadiasora katika kuimarisha maendeleo ya nchi zao za asili limepewa umhimu wa pekee na nchi mbali mbali duniani pamoja na Mashirikiano ya Kimataifa.

Alisema kuwa tarehe 5 Julai, 2006 akiwa Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alialikwa kuhudhuria mkutano wa  “Inteletuals From Africa and Diaspora” kwa niaba ya Rais Jakaya Kikwete huko Salvador, Bahia nchini Brazil ambapo mkutano huo ulieleza umuhimu wa Wanadiaspora kuchangia maendeleo ya nchi zao.

Alieleza kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeamua kuandaa mikakati mbali mbali ya kuwashirikisha Wanadiaspora katika kupanga na kutekeleza mipango ya maendeleo, ambapo Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2010-2015 ilianza kuweka mikakati maalum juu ya ushiriki wa Wanadisapora katika kuijenga nchi yao.

Dk. Shein aliahidi kwamba atahakikisha Kongamano hilo linaandaliwa kila mwaka ili kuweza kukutana na Wanadiaspora hasa katika kipindi hichi cha baina ya mwezi wa Juni na Septemba, huku akieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuweka bajeti maalum kila mwaka juu ya Kongamano hilo.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliwahakikishia Wanadiaspora kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inawakaribisha kuja kuekeza Zanzibar na kuwahakikishia kuwa suala la ardhi wasiwe na wasi wasi kwani wahusika wapo akiwemo Waziri anaeshughulikia Ardhi pamoja na Mkurugenzi wa ZIPA.

Pia, Dk. Shein aliwasihi Wanadiaspora  kuendelea kuwa Mabalozi wazuri wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika nchi wanazoishi na kuendelea kuwa mfano wa tabia njema ili kuendeleza sifa ya ukarimu, urafiki na usalama ambayo raia wa Tanzania wamejijengea na inatambulika katika mataifa yote duniani.

Aliwataka kuendelea kuishi kwa kuzingatia misingi ya urafiki, udugu na sheria ya nchi hizo wanazoishi huku wakiwa na mapenzi makubwa baina yao pamoja na nchi yao ya asili pamoja na kuimarisha Jumuiya zao ili ziendelee kuwa daraja la kuwaunganisha kati yao na wale waliopo nyumbani pamoja na taasisi zinazogusa maslahi yao.

Pamoja na hayo aliwataka kuendeleza kwa ari na kasi utamaduni wa kuja kutembelea nyumbani kila baada ya muda jambo ambalo ni muhimu na linaimarisha mapenzi huku akiwasisitiza wanapokuja nyumbani wafanye jitihada za kuja na watoto wao.

Nao Wanadiaspora walimpongeza Rais Dk. Shein kwa kukubali kushirikiana nao katika Kongamano hilo sambamba na kuwa karibu na Wanadiaspora huku akiwa mshiriki mkubwa wa maendeleo yao.

Pia, walieleza azma yao ya kujikusanya ili kuweka nguvu kwa pamoja badala ya kufanya kazi kwa mtu mmoja mmoja kwa lengo la kuweza kutoa msaada mkubwa zaidi.

Katika hafla hiyo, Dk. Shein pia, aligawa Sera kwa Wanadiaspora waliofika katika Kongamano hilo huku akitumia fursa hiyo kueleza mipango ya Serikali ya Kujenga miji mipya ya kisasa pamoja na kuuongeza mji wa Zanzibar kwa kufukia bahari katika eneo la Gulioni na kueleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuanzisha vyuo vikuu vipya viwili ambacho kimoja kitajengwa katika eneo la Fumba.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.