Habari za Punde

Serikali ya Jamuhuri ya Watu wa China Kuendelea Kuiunga Mkono Zanzibar Katika Kuimarisha Miradi ya Maendeleo na Uhusiano.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Ali Mohamed Sein, akizungumza na Makamu Mwenyekiti wa Bunge la Watu wa Jamuhuri ya China Ikulu Zanzibar, alipofika kuonana na Rais Dk. Shein kwa mazungumzo leo.18/11/2018.Ikulu Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein ameipongeza Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maendeleo sambamba na kukuza uhusiano uliopo.

Dk. Shein amesema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokuwa na mazungumzo na Makamu Mwenyekiti wa Bunge la Jamhuri ya Watu wa China Cai Defeng, aliopo nchini Tanzania kwa ziara ya siku sita kufuatia mwaliko wa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Yustino Ndugai.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dk. Shein alitoa shukurani kwa Serikali ya Watu wa China kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzbar katika kuendeleza miradi mbali mbali ya maendeleo ambayo imekuwa chachu katika kukuza uchumi wa Zanzibar.

Rais Dk. Shein alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati yake na Jamhuri ya Watu wa China ambapo ujio wa kiongozi huyo unathibitisha ukweli huo.

Alieleza kuwa China na Zanzibar zina historia kubwa, tangu wakati wa kupigania uhuru hadi hivi leo, ambapo nchi hiyo ilikuwa ya mwanzo kuyatambua Mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya Januari 12, 1964.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Zanzibar alipongeza uhusiano na ushirikiano mzuri uliopo kati ya (CCM) na chama cha Kikomunisti cha China (CPC) chini ya uongozi wa Rais Xi Jinping wan chi hiyo.

Dk. Shein alizipongeza hatua za Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kuunga mkono jitihada za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo afya, elimu, kilimo, maji safi na salama, miundombinu, viwanda na mengineyo

Dk. Shein alipongeza juhudi kubwa zinazochukuliwa na nchi hiyo katika kutoa nafasi za masomo kwa wanafunzi kutoka Zanzibar sambamba na mashirikiano yaliopo kutoka Jimbo la Jangsu katika kuimarisha sekta ya afya.

Alipongeza azma ya Jamhuri ya Watu wa China kuendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano katika sekta mbali mbali za maendeleo zikiwemo uchumi wa bahari, uvuvi, uwekezaji pamoja na gesi asilia na mafuta.

Dk. Shein aliwakaribisha wawekezaji kutoka China kuja kuekeza Zanzibar sambamba na watalii wa nchi hiyo kuitembelea Zanzibar kutokana na vivutio kadhaa vilivyopo hapa nchini.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa uchumi wa Bahari ni miongoni mwa mambo muhimu yaliopewa kipaumbelea na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kukuza uchumi wake hasa ikizingatiwa kuwa ni mwa wanachama wa nchi zinazopakana na  bahari ya Hindi (IORA).

Pia, Rais Dk. Shein alipongeza mashirikiano yaliopo kati ya Bunge la Jamhuri ya Watu wa China na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumpongeza Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Yustino Ndugai kwa kumualika kiongozi huyo kuja kuitembelea Tanzania.

Aidha, Rais Dk. Shein alimuhamikikishia kiongozi huyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuthamini juhudi za Jamhuri ya watu wa China chini ya kiongozi wake Rais Xi Jinping kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli ataendeleza uhusiano uliopo kati ya nchini mbili hizo kwa kutambua ushirikiano wa kihistoria ambao umeanzishwa na waasisi wa Mataifa hayo.

Nae, Makamu Mwenyekiti wa Bunge la Jamhuri ya Watu wa China Cai Defeng alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Jamhuri ya Watu wa China itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo kwa lengo la kukuza uchumi na kuimarisha ustawi wa jamii.

Alimuhakikishia Dk. Shein kuwa China iko tayari kuisaidia Zanzibar katika kuendeleza uchumi wa bahari, uvuvi, utalii pamoja na sekta nyengine huku akiahidi kuimarisha sekta ya uwekezaji hapa Zanzibar kwa kuwaalika wawekezaji wa China kuja kuwekeza Zanzibar.

Aidha, kiongozi huyo alipongeza mazungumzo aliyoyafanya na viongozi wa Mabunge hapa nchini pamoja na kueleza mashirikiano mazuri yaliopo kati ya Bunge la nchi yake na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.

Sambamba na hayo, alipongeza mapokezi makubwa aliyoyapata pamoja na ukarimu wa wananachi na viongozi wa Zanzibar pamoja na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jumla.
 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.