Habari za Punde

HESLB yakusanya TZS 94.01 bilioni kati ya Julai – Desemba, 2018.*Ni kutoka kwa wanufaika zaidi 198,659 * Yasisitiza kuwasaka wanufaika na waajiri wanaokiuka sheria. * Yajiunga rasmi na mfumo GePG.

Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Abdul-Razaq Badru (wa pili kushoto), Mwakilishi wa Wizara ya Fedha, Basil Baligumya (kushoto) na wawakilishi wa benki za CRDB (Goodluck Nkini), NMB (Taina Kikoti) na TPB (Deo Kwiyukwa) wakishiriki katika uzinduzi malipo ya mikopo ya elimu ya juu kupitia Mfumo wa Serikali wa Ukusanyaji Mapato (GePG). hafla hiyo imefanyika jijini Dar es salaam leo, Jumanne, Jan. 15, 2019 (Picha na HESLB).
  • Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Abdul-Razaq Badru (katikati) akiongea jijini Dar es salaam leo, Jumanne, jJn. 15, 2019 wakati wa uzinduzi malipo ya mikopo ya elimu ya juu kupitia Mfumo wa Serikali wa Ukusanyaji Mapato (GePG). Kulia ni Mwakilishi wa Wizara ya Fedha, Kitengo cha GePG Basil Baligumya na kueshoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Urejeshaji Mikopo wa HESLB Ignatus Oscar (Picha na HESLB).

Na Mwandishi Wetu, 15, 2019
Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imekusanya jumla ya TZS 94.01 bilioni kutoka kwa wadaiwa wa mikopo ya elimu ya juu katika kipindi cha Julai – Desemba, 2018 na kuvuka lengo lake la kukusanyaTZS 71.4 bilioni katika kipindi hicho.

Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Abdul-Razaq Badru amesema leo jijini Dar es salaam kuwa makusanyo hayo yametoka kwa jumla ya wanufaika zaidi 198,659 ambao wamejiari au kuajiriwa katika sekta binafsi na umma.

Wanufaika waliobainika na kuanza kulipa kati ya Julai – Disemba 2018

“Katika kipindi hicho cha Julai – Desemba pia tumefanikiwa kuwabaini wanufaika wapya zaidi 12,600 ambao walikua hawajaanza kurejesha mikopo yao na sasa wameanza na hivyo kufanya wateja wanaorejesha kufikia198,656 hivi sasa,” amesema Badru wakati akiongea na wanahabari katika ofisi za HESLB na kuongeza:

“Makusanyo haya ya TZS 94.01 bilioni ni sawa na ongezeko la asilimia 8.7 ikilinganishwa na TZS 85.88 bilionizilizokusanywa katika kipindi kama hicho mwaka uliopita yaani, Julai – Disemba, 2017,” amesema.

Badru alikua akieleza hali ya ukusanyaji wa mikopo katika kipindi cha nusu mwaka wa fedha wa 2018/2019unaomalizika baadae mwezi Juni mwaka huu.

“Malengo yetu kwa mwaka mzima ni kukusanya TZS 150 bilioni, hivyo kwa kukusanya TZS 94.01 bilioni hadi Desemba, 2018, tunaona tunakwenda vizuri na tutavuka hata lengo letu … tunawashukuru wateja wetu wanaorejesha na waajiri wanaotuunga mkono kwa kufuata masharti ya sheria,” amesema Badru.

Kwa mujibu wa sheria iliyoanzisha HESLB, waajiri wanapaswa kukata asilimia 15 ya mshahara ghafi (basic salary) wa mnufaika na kuwasilisha makato hayo kwa HESLB ndani ya siku 14 baada ya tarehe ya mwisho wa mwezi wa makato.

Kujiunga na GePG
Katika mkutano huo, HESLB pia ilitangaza rasmi kujiunga na Mfumo wa Serikali wa Ukusanyaji Mapato yaani (Government e-Payment Gateway - GePG) na kusisitiza kuwa kuanzia sasa, malipo yote kwenda HESLB yatapokelewa kwa mfumo huo unaofuatwa na taasisi mbalimbali za Serikali.

“Mwajiri au mnufaika anachotakiwa kufanya ni kunakiri ‘Namba ya Kumbukumbu’ Control Number) iliyopo kwenye ankara (Loan Statements) zao na kufanya malipo kwa njia ya benki au simu,” amesema Badru na kufafanua kuwa namba hizo na maelezo ya kina yapo kwenye tovuti yetu (www.heslb.go.tz).
Akizungumza katika mkutano huo, mwakilishi wa Wizara ya Fedha ambao ndiyo wasimamizi wa GePG, Basil Baligumya alisema uamuzi wa Serikali kukusanya malipo yake kupitia GePG unalenga kumpa mlipaji urahisi wa kulipa, kuongeza mapato na hivyo kutoa huduma bora kwa wananchi.
Kwa upande wao, wawakilishi wa benki za CRDB, NMB na TPB ambao walihudhuria mkutano huo waliipongeza serikali kwa kuanzisha mfumo wa GePG na HESLB kwa kujiunga kwa wakati na kuahidi kutoa ushirikiano ili kuwawezesha wateja wa HESLB kulipa kwa urahisi.
Namba za simu kwa wateja wenye maswali
“Ninachopenda kusisitiza ni kuwa kuanzia sasa, hakuna malipo yoyote yatakayopokelewa bila kufuata mfumo huu na wateja wetu wenye maswali wanaweza kutupigia kwa namba 0659 748 536; 0621 870 172; 0620 714 421; na 0621 870 173),” amesema.

HESLB ni taasisi ya Serikali iliyoanzishwa mwaka 2005 ili kutekeleza majukumu makuu mawili. Mosi, kutoa mikopo ya elimu ya juu kwa wanafunzi wa kitanzania ambao ni wahitaji na pili kukusanya fedha za mikopo iliyoiva kutoka kwa wanufaika waliokopeshwa na Serikali tangu mwaka 1994/1995.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.