Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Wizara ya Kilimo Zanzibar Kuhusiana na Maendeleo ya Miradi Mbalimbali ya Wizara Hiyo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Kilimo Maliasili Mifugo na Uvuvi Zanzibar,Ikulu leo, kuhusiana na Maendeleo ya Miradi mbalimbali ya Wizara hiyo,uliofanyika katika ukumbi wa Ikulu Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  amesisitiza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuanzisha Taasisi ya Utafiti ya Uvuvi na Mazao ya Bahari ili kwenda sambamba na Sera ya uchumi wa bahari.

Hayo aliyasema leo wakati alipokutana na uongozi wa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Ikulu mjini Zanzibar ambapo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd nae alihudhuria ambapo uongozi huo ulieleza maendeleo ya miradi mbali mbali inayoendeshwa katika Wizara hiyo.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alieleza kuwa kuna umuhimu mkubwa kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuwa na Taasisi ya Utafiti ya Uvuvi na Mazao ya Bahari hasa ikizingatiwa mazingira ya Zanzibar na uchumi wake.

Alieleza kuwa ni jambo la busara kuwepo kwa Taasisi hiyo hapa Zanzibar ambayo itakuwa na umuhimu mkubwa kwa Zanzibar pamoja na wananchi wake na kuipelekea Zanzibar kutekeleza ipasavyo uchumi wa bahari kwa vitendo.

Alieleza kuwa tayari Zanzibar ni mwanachama wa Jumuiya ya Nchi zinazopakana na Bahari ya Hindi (IORA), hivyo kuna umuhimu mkubwa wa kuweka mikakati madhubuti katika kufikia malengo, makubaliano na maazimio ya Jumuiya hiyo ikiwa ni pamoja na kutekeleza kwa vitendo uchumi wa bahari.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa mbali ya uwepo wa Jumuiya hiyo ya (IORA) pia, Novemba mwaka jana 2018 alihudhuria Mkutano wa Uchumi wa Bahari uliofanyika mjini Nairobi Kenya kuanzia Novemba 26 hadi 28 ambapo mbali ya mambo mengineyo mkutano huo pia, ulijikita na masuala ya uchumi wa bahari hasa kwa nchi zilizopakana na Bahari ya Hindi.

Rais Dk. Shein pia, alieleza juhudi za makusudi zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuanzisha viwanda vya uvuvi hapa nchini, azma ya kuanzisha Chuo cha Ubaharia pamoja na kuiimarisha Kampuni yake ya  Uvuvi.

Akieleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuimarisha mradi wa kilimo cha umwagiliaji maji, Rais Dk. Shein alisema kuwa umefika wakati kwa Zanzibar kuongeza ukubwa wa eneo la kilimo cha umwagiliaji maji kwani mradi huo una umuhimu mkubwa kwa Wazanzibari hasa ikizingatiwa kuwa chakula cha wali ndio kilichopewa kipaumbele na jamii.

Alieleza kuwa matarajio ya Serikali ni kuongezeka kwa kiwango cha uzalishaji wa mpunga kutokana na mradi huo mkubwa.

Aidha, Rais Dk. Shein aliupongeza uongozi wa Wizara hiyo na kusisitiza kuwa mashirikiano katika kazi ni suala la lazima sambamba na kufanya kazi kwa kufuata maadili, sheria na kanuni za kazi ambayo yanaleta usalama mkubwa kazini.

Akisisitiza suala zima la mashirikiano kazini, Dk. Shein aliutaka uongozi wa Wizara hiyo kuendelea kuwaongoza vyema watendaji waliochini yao huku akiwaeleza malengo na madhumuni ya kuwepo kwa vyeo na utofauti uliopo kati ya kiongozi na anaeongozwa.

Dk. Shein alisisitiza umuhimu wa kufanya kazi kwa pamoja hasa ikizingatiwa kuwa kila mmoja ana majukumu yake hasa wakizingatia kuwa wanaowafanyia kazi ni wananchi.

Nae Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd alitoa pongezi kwa uongozi wa Wizara hiyo na kusisitiza haja ya kufanya kazi kwa juhudi hasa ikizingatiwa kuwa Wizara hiyo ni tegemeo kubwa kwa wananchi wa Zanzibar kutokana na kubeba mambo muhimu katika maisha yao.

Mapema Waziri wa ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, Rashid Ali Juma alieleza maendeleo ya mradi wa Usimamizi wa shughuli za Uvuvi wa Kanda ya Kusini Magharibi mwa Bahari ya Hindi (SWIOFish) ambao ni mradi wa miaka sita ulioanza Juni 22,2015 hadi Septemba 2021.

Alieleza kuwa mradi huo umetayarishwa kwa dhamira ya kuongeza faida kiuchumi, kijamii na kimazingira kwa nchi za Kusini Magharibi mwa Barahari ya Hindi (SWIO) kutokana na matumizi endelevu ya uvuvi wa bahari ambao hivi sasa unatekelezwa na nchi tatu ambazo ni Tanzania, Msumbiji na Comoro.

Pia, Waziri Juma alieleza kuwa Ujenzi wa Miundombinu ya Umwagiliaji maji unaotekelezwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia mkopo wa Benki ya Exim-Korea ambao ni miongoni mwa juhudi na mikakati ya Serikali kuleta mageuzi katika sekta ya kilimo.

Pia, alieleza kuwa mradi huo pia ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango Mkuu wa Umwagiliaji maji wa Zanzibar ambapo mkataba wake ulitiwa saini tarehe 6 Disemba 2018 baina ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya hiyo na Kampuni ya Ujenzi ya KOLON- HANSON JV kutoka Korea utakaogharimu Dola za Kimarekani milioni 64.3.

Aliongeza kuwa Mradi huo utajumuisha ujenzi wa miundombinu ya mitaro ya umwagiliaji, mabwawa manne makubwa, kuchimba visima 49 na kuweka pampu zake, ujenzi wa maeneo ya kuanikia mpunga na kukata vishamba pamoja na kuweka sawa ardhi.

Alieleza kuwa mradi huo utajenga na kuendeleza eneo litakalokuwa na jumla ya hekta 1,524 (Eka 3,810) zitakazojengwa katika mabonde saba ya umwagiliaji maji kwa Unguja na Pemba ambayo ni Cheju, Kinyasini, Kibokwa, Kilombero,Chaani, Makwararani na Mlemele.

Alisisitiza kuwa lengo kuu la mradi huo ni kuimarisha usimamizi makini wa uvuvi wa kipaumbele kuanzia ngazi ya Kikanda, Kitaifa na Kijamii.

Pamoja na hayo, Waziri huyo alieleza lengo kuu la usimamizi wa Serikali katika uchimbaji wa mchanga na usafirishaji wake ambalo ni kuhakikisha kuwa rasilimali hiyo inapatikana kikawaida kwa matumizi ya wananchi na kwa bei nafuu kwa mujibu wa kanuni na Sheria zilizopo.

Uongozi wa Wizara hiyo ulieleza kufarajika na ushauri, maelekezo wanayoyapata kutoa kwa Rais Dk. Shein ambayo yamekuwa chachu katika utendaji wa kazi zao huku wakitumia fursa hiyo kusisitiza kuwa wataendelea na ushirikiano mkubwa walio nao ili kuweza kuendelea kupata mafanikio makubwa zaidi katika Wizara hiyo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.