Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia katika viwanja vya Mzee Mgeni Fuoni Mambosasa, wakati wa hafla ya Uzinduzi wa Barabara ya Kijitoupele hadi Fuoni Mambosasa iliojengwa kwa kiwango cha lami.
RAIS wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Mapinduzi
ya Januari 12, 1964 yameleta usafiri wa uhakika wa barabara bora mjini na vijijini hapa Zanzibar.
Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo katika uzinduzi wa Barabara
ya Kijitoupele hadi Fuoni Mambosasa huko katika uwanja wa Mzee Mgeni Fuoni
Mambosasa Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini Magharibi, ikiwa ni miongoni mwa
shamra shamra za miaka 55 ya Mapinduzi.
Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alisema kuwa baada ya
Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 mipango ya maendeleo ndipo iliopoanza
ikiwa ni pamoja na kujenga barabara zilizo bora.
Rais Dk. Shein alisema kuwa kabla ya Mapinduzi hapakuwa na
barabara zenye hadhi na kiwango cha ubora kama ilivyo hivi sasa katika maeneo
yote ya Zanzibar.
Aidha, Dk. Shein alisisitiza kuwa mafanikio hayo yote
yametokana na uongozi bora wa ASP hadi
hivi leo kuwa CCM, ambapo kwa kutambua umuhimu wa miundombinu ya
barabara, ndipo imeweka kipaumbele hicho.
AlIeleza kuwa kasi ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
imeimarika zaidi, mara baada ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 tofauti na ilivyokuwa hapo kabla ya Mapinduzi hayo.
Dk. Shein aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni
Serikali ya wananchi wote wa Zanzibar na kamwe hakuna Serikali nyengine, hivyo
aliwataka wananchi kuendelea kuithamini Serikali yao na kuachana na wale
wanaoibeza.
Akieleza historia na umuhimu wa Mapinduzi, Rais Dk. Shein
alisema kuwa kabla ya kuingia wakoloni wa Kireno, Zanzibar ilikuwa
haikutawaliwa na badala yake iliongozwa na viongozi wenyeji wa kijadi wakiwemo
Masheha, Maliwali, Madiwani na wengineo.
Aliongeza kuwa kukandamizwa, kunyonywa, kunyanyaswa pamoja na
kunyimwa haki kwa Wazanzibari ikiwa ni pamoja na kunyimwa uhuru kutokana na
ushindi wa kura za ASP kila pale uchaguzi unapofanyika ndiko kulikopelekea
kufanyika kwa Mapinduzi ya Januari 12, 1964.
Katika hatua nyengine, Dk. Shein alisema Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar imedhamiria kumaliza ujenzi wa Barabara, kuanzia eneo la Fuoni
Polisi hadi Tunguu, na kubainisha kuwa utekelezaji huo utafanyika kwa awamu
mbili tofauti
“Tunatarajia pia kumalizia barabara itokayo Fuoni Mambo sasa
hadi Mwera, na nitafurahi ujenzi huo ukimalizika kabla ya muda wangu wa kuwa
madarakani kwisha”, alisema
Mapema, Katibu Mkuu
Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa,Serikali za Mitaa na Idara Maalum
za SMZ Radhia Rashid Haroub, akitowa taarifa ya kitaalamu juu ya ujenzi
huo, alisema barabara hiyo yenye urefu
wa kilomita mbili na upana wa mita saba ina uwezo wa kupitisha gari zenye uzito
wa hadi tani 20 pamoja na kuwa na mitaro ya maji ya mvua yenye urefu wa mita
1,000.
Alisema ujenzi huo
uliogharimu zaidi ya shilingi Bilioni 1.4 umetekelezwa na Serikali kupitia
Mfuko wa Barabara, ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015 - 2020,
Ibara ya 88 (c) (i) nukta ya 18.
Alieleza kuwa
uzinduzi huo unakwenda sambamba na ule wa barabara iliyoanzia Magogoni
Kwamabata hadi Nyarugusu yenye urefu wa kilomita mbili, iliyogharimu zaidi ya
shilingi Bilioni 1.1.
Aidha, alisema ni
muendelezo wa barabara iliyoanzia Nyarugusu hadi Kijitoupele yenye urefu wa
kilomita 1.65 iliyogharimu zaidi ya shilingi Bilioni moja.
"Huu ni
utekelezaji wa ahadi yako Mheshimiwa Rais iliyotutaka tukamilishe barabara hii
kwa kiwango cha lami hadi kufikia Kijitoupele, ambapo ilikamilika mwaka jana',
alisema.
Radhia alisema
kukamilika kwa ujenzi wa barabara hiyo (Nyarugusu - Kijitoupele) kwa kiasi
kikubwa imetatua tatizo la msongamano wa
magari katika barabara ya Mwanakwerekwe katika kipindi cha mvua za masika mwaka
uliopita, kwa wananchi wanaotumia barabara ya Fuoni kwenda na kurudi mjini.
Katika hatua
nyengine, Katibu Mkuu huyo alisema kwa kipindi cha miaka mitatu sasa Wizara
hiyo imefanikiwa kuzifanyia matengenezo barabara kadhaa za ndani kwa
kiwango cha lami Unguja na Pemba.
Alizitaja barabara
hizo kuwa ni pamoja na barabara ya Hospitali ya Chakechake hadi Tibirinzi,
barabara ya Misufini - Kwabiziredi, Mitiulaya, mzunguko wa nje wa Mnara wa
Mapinduzi Michenzani , barabara ya Kilimani nyumba za maendeleo pamoja na ile
ya Kikwajuni juu msikitini.
Alibainisha kuwa
barabara zote hizo; pamoja na iliyozinduliwa leo , zina jumla ya urefu wa
kilomita 8.35.
Alisema kwa sasa
barabara zinazoendelea kufanyiwa matengenezo na Wizara hiyo ni pamoja na ile ya Msingini Pemba pamoja na
barabara ya Soko kongwe kuelekea skuli ya Ngomeni.
"Taratibu za
ujenzi wa barabara ya kuelekea skuli ya Kinuni zimeshaanza kwa kutangaza zabuni
na tunatarjia kuanza ujenzi huo ndani ya mwezi wa February mwaka huu', alisema.
Nae, Waziri wa
Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara
Maalum za SMZ, Haji Omar Kheir alisema la ujenzi wa barabara za ndani
unaendelea kufanyika nchini kote, unalenga kupunguza msongamano wa magari
katika barabara kuu.
Aidha, Alisema
Wizara hiyo itaendelea kuzishughulikia barabara zote zilizoainishwa ikiwemo ya
Mtofaani - Hawaii na ile ya Fuoni
Kibondeni, ili kurahisisha huduma za
usafiri kutoka eneo moja kwenda jengine.
Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822
E-mail: abdya062@gmail.com
No comments:
Post a Comment