RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la MapinduziDk.
Ali Mohamed Shein kesho anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika Kilele cha Maadhimisho
ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi), ambapo kwa upande wa Zanzibar maadhimisho
hayo yatafanyika Mkoa wa Kusini Unguja.
Katika maadhimisho
hayo yanayotarajiwa kufanyika katika eneo la Tunguu,Wilaya ya Kati Unguja
ambapo baadae Rais atawahutubia wananchi katika ukumbi wa Dk. Ali Mohamed Shein
uliopo katika Kampasi ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), baada ya kupokea
maandamano ya wafanyakazi wa sekta za umma na binafsi.
Aidha, salamu mbali
mbali zitatolewa zikiwemo kutoka Shirika la Kazi Duniani (ILO), Jumuiya ya
Waajiri Zanzibar (ZANEMA), salamu za Waziri, risala ya wafanyakazi, Rais atatoa
zawadi kwa wafanyakazi bora na hatimae kuwahutubia
wafanyakazi.
Kauli mbiu ya mwaka
huu katika maadhimisho hayo inasema “Kuimarika kwa Uchumi wa Taifa, kuendane na
Kuongezeka kwa Maslahi ya Wafanyakazi”.
Kila ifikapo Mei Mosi
ya Kila mwaka, Zanzibar huungana na nchi nyengine duniani katika kuadhimisha
Siku ya Wafanyakazi Duniani ambapo hapo mwaka jana maadhimisho hayo yalifanyika
huko Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba.
Katika uongozi wa Rais
Dk. Shein wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba aliielekeza Wizara
yenye dhamana ya masuala ya kazi na Shirikisho la Vyama Huru vya Wafanyakazi
(ZATUC) kuwa maadhimisho ya Mei Mosi yafanyike kwa utaratibu wa mzunguko ili
kila Mkoa wa Zanzibar upate fursa hiyo.
Katika hotuba zake
mbali mbali anazozitoa Rais Dk. Shein amekuwa akisisitiza kuwa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea na utaratibu wake wa kuzilinda haki za
wafanyakazi na kuimarisha maslahi ya wafanyakazi hatua kwa hatua.
Katika hotuba yake ya
Mei Mosi mwaka jana, Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar ya Awamu ya Saba itaendelea kuhakikisha kwamba maslahi ya wafanyakazi
katika sekta ya umma na binafsi yanazidi kuimarika siku hadi siku kadri hali ya
uchumi wa Zanzibar itakavyoruhusu.
Aliongeza kuwa dhamira
ya Serikali ni kuona kuwa maslahi ya kila mwananchi wa Zanzibar katika sekta
yoyote ile anayoifanyia kazi yanaimarika bila ya kujali aina ya muajiri.
Katika hotuba ya
kuzindua Baraza la Nane la Wawakilishi aliyoitoa tarehe 11 Novemba mwaka 2010
Dk. Shein alieleza bayana mtazamo wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya
Saba kuhusu wafanyakazi na kusema “Rasilimali moja kubwa ya nchi ni wafanyakazi
ambapo ndio msingi wa kujenga uchumi na maendeleo yote ya nchi”.
Aidha, katika kutilia
mkazo suala la umuhimu wa kushirikiana na vyama vya wafanyakazi alisema kuwa
“Maslahi bora ya wafanyakazi popote ni ajenda yetu na tutahakikisha
mashirikiano na chombo chao ‘Shirikisho la vyama huru vya wafanyakazi’ na
kukuza mahusiano mema”.
Kama inavyofahamika
kuwa wafanyakazi ni muhimu katika maendeleo ya Taifa lolote lile kwani ni
rasilimali inayotegemewa katika kuzalisha mali na kunyanyua uchumi wa nchi.
Kwa kutambua hilo
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikichukua hatua mbali mbali kujenga
mazingira mazuri kwa wafanyakazi ili waweze kuzalisha zaidi na kuongeza pato la
Taifa.
Siku hii ya Mei Mosi
inatokana na historia ya maandamano yaliyotokea Chicago nchini Marekani mnamo
mwaka 1886 ambapo zaidi ya wafanyakazi 300,000 waliandamana wakidai haki zao za
msingi.
Jumuiya za Kitaifa zilipendekeza
kwamba siku ya tarehe 01 Mei ya kila mwaka iwe ni siku ya mapumziko kwa ajili
ya kuwakumbuka wafanyakazi walioumia na waliofariki zama hizo na Tanzania
inaungana na Jumuiya hizo kufanya siku hiyo kuwa ni siku ya kufanya maadhimisho
hayo pamoja na kuwa ni siku ya mapumziko.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment