Habari za Punde

Uongozi wa Ofisi ya Rais Zanzibar Wapongezwa na Utendaji Kazi Wake.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, katika Mkutano wa Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo kwa kipindi cha mwezi wa Julai 2018 hadi March 2019, uliofanyika Ukumbi wa Ikulu Ndogo Kibweni Zanzibar.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein,ameupongeza uongozi wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kuendelea kuonesha taswira njema katika kutekeleza majukumu yao ya kazi.
Ameyasema hayo leo huko katika ukumbi wa Ikulu ndogo Kibweni mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi wakati ulipowasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kazi wa Ofisi hiyo kwa Kipindi cha Julai 2018 hadi Machi 2019.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuupongeza uongozi huo kwa kutekeleza vyema majukumu yao sambamba na kutekeleza vizuri taswira ya Ofisi hiyo kwa lengo la kuendelea kuwatumikia wananchi.

Aliongeza kuwa uongozi wa Ofisi hiyo inatakiwa kuendelea kuwa kioo kwa Ofisi na taasisi nyengine jambo ambalo limekuwa likitekelezwa vyema na kuweza kupata mafanikio makubwa katika utendaji wa kazi za kila siku katika Ofisi hiyo ya Rais.

Aidha, Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa uongozi wa Ofisi hiyo kwa utayarishaji na uwasilishaji mzuri wa Mpango Kazi wa Ofisi hiyo.

Rais Dk. Shein pia, aliupongeza uongozi wa Ofisi hiyo chini ya Waziri wake Issa Haji Ussi Gavu kwa kuwasilisha vyema Bajeti ya mwaka wa fedha ya Wizara hiyo kwa mwaka 2019-2020 katika Baraza la Wawakilishi na kuweza kupita kwa wakati.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alimpongeza Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee na uongozi wake wote wa Baraza la Mapinduzi kwa  kutekeleza vyema majukumu yao na kuendelea kumsaidia vizuri

Pia, Rais Dk. Shein aliwapongeza Washauri wake pamoja na Wasaidizi wake wote kwa kuendelea kumshauri na kumsaidia katika kutekeleza vyema majukumu yake ya kila siku ya kuwatumikia wananchi.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara yake ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji ya kuzifanyia ukarabati barabara zote zilizoharibika kutokana na athari za mvua za masika zinazoendelea hivi sasa Unguja na Pemba.

Pia, Rais Dk. Shein alieleza azma ya Serikali kupitia Wizara hiyo ya kuendelea na ujenzi wa barabara zote inazozijenga kwa upande wa Unguja na Pemba sambamba na kuendeleza mradi wa Huduma za Miji (ZUSP) na ujenzi wa barabara ya Mwanakwerekwe na barabara na daraja katika eneo la Kibondemzungu.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliwapongeza watendaji wenzake wa Ofisi hiyo kwa kuwasilisha vyema Mpango Kazi huo huku akiusisitiza uongozi wa Ofisi hiyo kuendelea kuijenga vizuri taswira nzuri ya Rais.

Katika maelezo yake, Dk. Mzee alisisitiza haja ya kuendeleza mashirikiano kwa viongozi na watendaji wote wa Ofisi hiyo huku wakitambua kwamba wanabeba taswira ya Rais.

Aidha, alitumia fursa hiyo kwa kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa miongozo yake anayoitoa kwa Ofisi hiyo pamoja na nyenginezo zikiwemo Wizara zote za Serikali na kuahidi kuendelea kumsaidia na kumuunga mkono.

Nao Washauri wa Rais walimpongeza Rais Dk. Shein kwa juhudi zake za kuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar sambamba na utekelezaji mzuri wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020.

Mapema, Waziri wa Ofisi hiyo, Issa Haji Ussi Gavu alieleza muhtasari wa Mpango Kazi wa Ofisi hiyoalisema kuwa uwelewa wa wananchi juu ya shughuli zinazotekelezwa na Rais  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi yameongezeka kupitia utoaji taarifa kwa njia za kisasa za mawasiliano zikiwemo mitandao ya kijamii sambamba na kupitia sinema mbali mbali Unguja na Pemba.
Alieleza kuwa Zanzibar imeendelea kushiriki katika mikutano ya kikaanda kikamilifu ambapo imekuja na tija kwa Zanzibar katika kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Waziri Gavu alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa na mahusiano mema na Wazanzibari wanaoishi nje ya nchi kupitia makongamano yanayofanyika kila mwaka ambapo pia, Ofisi hiyo imeshiriki katika Makongamano ya Wanadiaspora yakiwemo ya Watanzania wanaoishi nchini Marekani na Sweden.
Pamoja na hayo, Waziri Gavu alieleza kuwa Ofisi hiyo imeandaa Sera ya Mawasiliano na Habari ya Ofisi ambayo inatarajiwa kuimarisha utaratibu wa Mawasiliano na utoaji wa taarifa ndani na nje ya Ofisi.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.