Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Amuapisha Mkuu wa Kikosi cha Valantia Zanzibar Major Said Ali Juma Shamuhuna Ikulu leo.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amemuapisha Major Said Ali Juma Shamuhuna kuwa Mkuu wa Kikosi cha Valantia Zanzibar (KVZ).

Hafla ya kuapishwa kwa Major Shamuhuna, imefanyika leo Ikulu mjini Zanzibar na kuhudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamu wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd pamoja na Wakuu wa vikosi vya Ulinzi vya SMZ na SMT.

Wengine waliohudhuria hafla hiyo ni Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid, Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar Said Hassan Said, Mawaziri, Makatibu Wakuu pamoja na Naibu Kadhi wa Zanzibar Sheikh Hassan Othman Ngwali.

Viongozi wengine waliohudhuria hafla hiyo ni Mkuu wa  Mkoa wa Mjini Magharibi Ayoub Mohamed Mahmoud, Meya wa Manispaa ya Mji wa Zanzibar Khatib Abrahman Khatib, Washauri wa Rais wa Zanzibar, na viongozi wengine wa Serikali pamoja na wanafamilia.

Major Shamuhuna aliteuliwa hivi karibuni mnamo Juni 13, 2019 na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa mujibu wa uwezo aliopewa chini ya Kifungu cha 9(1) cha Sheria ya Kikosi cha Valantia Namba 5 ya mwaka 2004.

Major Said Ali Juma Shamuhuna anachukua nafasi ya aliyekuwa Mkuu wa Kikosi hicho Lt. Col. Mohamed Mwinjuma Kombo ambaye amestaafu kwa mujibu wa Sheria.

Akizungumza mara baada ya kuapishwa kwakwe, Major Shamuhuna alisema kuwa uteuzi huo alioupata kutoka kwa Rais Dk. Shein unathibitisha kwa kiasi gani Serikali inavyothamini utendaji wake wa kazi.

Aidha, Major Shamuhuna aliahidi kuwa atakiongoza kikosi hicho cha Valantia Zanzibar (KVZ) kwa kuzingatia Sheria, kanuni, taratibu, hekima na busara katika kuhakikisha mafanikio zaidi yanapatikana huku akisisitiza mashirikiano ya pamoja ndani ya Kikosi hicho.

Sambamba na hayo, Major Shamununa alieleza kuwa atahakikisha anasimamia nidhamu na utekelezaji bora wa majukumu kwa viongozi na askari wa kikosi hicho ili kufanikisha majukumu ya kila siku katika maendeleo ya Jeshi hilo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.