Na. Abraham Nyantori-MAELEZO
Wakati vikao tangulizi vya
Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) vinafikia ukingoni mwishoni mwa
wiki na kutoa nafasi kwa Marais wa SADC kukutana katika Mkutano wao wa kilele
Agost 17 na 18, wafanyabiashara wa Tanzania na ujumbe wa wafanyabiashara wa
Afrika Kusini wamekutana wakiongozwa na Marais wao Cyril Ramaphosa na Dkt. John
Magufuli.
Mkutano huo uliofanyika katika
Kituo cha Kimataifa cha Julius Nyerere, jijini Dar Es Salaam mbali na kuwakutanisha sekta binafsi, umewaleta
pamoja Mawaziri wa sekta mbalimbali nchini, taasisi za umma na binafsi za
Tanzania na Afrika Kusini, ukiwa ni jukwaa la pili kwa nchi hizo kuongea kuhusu
fursa za biashara, uwekezaji na ukuzaji wa uchumi kupitia sekta ya viwanda
Huku kila upande ukionyesha ari
ya kuongeza ushirikiano kwa mataifa haya, Rais wa Tanzania Dkt John Magufuli
ameeleza mahusiano ya kibiashara baina ya Tanzania na Afrika Kusini, ambapo
yanaonekana kukuwa kwa kasi, huku akitolea mfano miradi ya huduma na uuzaji wa
bidhaa kwenda Afrika Kusini ulikuwa toka dola za kimarekani 108.2 milioni mwaka
2017 hadi dola 437.2 milioni kwa sasa.
Rais Magufuli amesema wawekezaji
toka Afrika Kusini wamefikia 228 na kuwekeza kiasi cha dola za kimarekani 806.5
millioni na kushika nafasi ya 13 kwa ukubwa wa uwekezaji, ambapo Tanzania
katika nchi za SADC, mahusiano yake kibiashara yako juu na Afrika Kusini
ukilinganisha na nchi wanachama.
Pamoja na Tanzania kujiimarisha
katika kuboresha mihimili ya kujenga uchumi kama uboreshaji wa usafiri na
usafirishaji; bandari, viwanja vya ndege, barabara na vivutio vya utalii, Dkt
Magufuli amesema serikali yake inatambua sekta binafsi katika uwekezaji na
hivyo imeboresha sheria mbalimbali na Mamlaka zinazohudumia wawekezaji na
wafanyabiashara ili kufanikisha
Wakati Tanzania inahimiza
uwekezaji wa ujenzi wa viwanda nchini kwa wawekezaji wa nje na ndani, Rais wa
Afrika Kusini Cyril Ramaphosa anatambua hatua ambayo nchi yake imefikiwa
kiuchumi, lakini anaona ipo haja kwa bara la Afrika kuona jinsi ya kujenga
nafasi za kazi na kujenga uchumi wa mataifa hayo kwa maisha ya watu wake.
Rais Ramaphosa anasisitiza watu
wa Tanzania na Afrika Kusini kuendeleza mahusiano yao ya kihistoria kwa nchi
zao katika kustawisha uchumi,huku jicho la pili likiangalia dunia kama sehemu
ya kutegemeana.
Pamoja na kuwepo uhusiano wa
kihistoria uliotokana najitihada za Tanzania kushirikiana na nchi za Kusini mwa
Afrika katika harakati za ukombozi wa Afrika, mahusiano yamekuwa yakipanda kutoka
mahusiano ya kisiasa na kuona fursa za uwekezaji katika miradi mbalimbali na
biashara baina ya mataifa haya mawili.
No comments:
Post a Comment