Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Alhajj Ali Mohamed Shein Alihutubia Baraza la Eid El Hajj Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia Baraza la Eid El Hajj katika Viwanja vya Dole Wilaya ya Magharibi"A" Unguja iliofanyika Kitaifa katika Wilaya hiyo leo.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein amewasisitiza wananchi kuendelea kudumisha amani na utulivu na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kutoa baraka hio ambayo haina mbadala kwa wananchi wa Zanzibar.
Alhaj Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hotuba yake aliyoitoa katika Baraza la Idd El Hajj lililofanyika huko katika viwanja vya Langoni, Wilaya ya Magharibi A, Mkoa wa Mjini Magharibi ambalo lilihudhuriwa na viongozi mbali mbali pamoja na wananchi.
Katika hotuba yake hiyo Alhaj Dk. Shein alisema kuwa bila ya amani maendeleo hayawezi kupatikana na hata waumini hawatoweza kupata wasaa wa kufanya ibada kwa utulivu.
“Tunayasikia matukio mbali mbali ya kusikitisha yanayotokea katika mataifa mengine,ambako amani imekosekana yanayotendeka huko ni vurugu, udhalilishji na ukatili wa kila aina, waumini wenzetu wamo ndani ya fadhaa hawana maendeleo, hawana hata utulivu wa kufanya ibada ili waungene na wenzano kusherehekea  Sikukuu mbali mbali”, aliongeza Alhaj Dk. Shein.
Alieleza kuwa amani ni miongoni mwa baraka ambazo Mwenyezi Mungu amezitoa kwa wananchi na iwapo itachezewa kwa kujihusisha na vitendo vya uvunjifu wa sharia, itakuwa neema hiyo waliyopewa wanaikufuru na Allah atakuwa hayuko radhi.
“Tumshukuru Mola wetu kwa kutujaalia kuwa na amani katika nchi yetu, nami kila nikipata nafasi ya kuzungumza nanyi wananchi wenzetu nimekuwa nikisisitiza juu ya umuhimu wa kuendelea kudumisha amani” alisema Alhaj Dk. Shein.
Aidha, Rais Dk. Shein ameeleza kuwa kutokana na kuendelea kuwepo kwa amani na utulivu Zanzibar inaendelea kupiga hatua na kuimarika kwa uchumi wake kwa kila mwaka.
Alifahamisha kuwa hali hiyo kukua kwa uchumi inaiwezesha Serikali kupata nguvu zaidi za kuimarisha miundombinu ya uchumi na kutoa huduma mbalimmbali ambazo wananchi wanazihitaji kwa ajili ya maisha ya kila siku katika hali iliyo bora zaidi.
Rais Dk. Shein alieleza kuwa ukuaji huo wa uchumi umeiwezesha Serikali kuimarisha maslahi ya wafayakazi wa Serikali na kuinua kipato chao pamoja na kupata uwezo wa kuitekeleza mipango mbalimbali wanayoipanga.
Pamoja na hayo, Alhaj Dk. Shein alieleza kuwa ni jambo la faraja kuona kuwa hali hiyo vile vile imewawezesha baadhi ya watumishi kupata uwezo wa kifedha kwenda kutekeleza ibada ya Hijja mapema badala ya kusubiri fedha za kiinua mgongo kama ilivyozoeleka.
Aliongeza kuwa taarifa kutoka Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana zinaeleza kuwa jumla ya Watanzania 2,500 wamejitokeza mwaka huu kwa ibada ya Hijja wakiwemo 1,700 kutoka Taasisi 22 za Zanzibar zinazoshughulikia masuala ya Hijja na watu 800 kutoka Tanzania Bara.
“Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwawezesha ndugu zetu kwenda kuitekeleza ibada hio kwa hakika si kila aliyejaaliwa kupata neema hizo hudiriki kwenda kuitekeleza ibada hio kubwa” alisisitiza Alhaj Dk. Shein.
Aidha, Alhaj Dk. Shein aliwahimiza waumini wa dini ya Kiislamu kwa wale wenye uwezo wa kifedha na afya njema kuepukana na vipingamizi visivyo na msingi ambavyo vinaweza kwenda kuitekeleza ibada ya Hijja na badala yake waende kuitekeleza ibada hiyo.
Alhaj Dk. Shein pia, alisisitiza kuwa ni wajibu kuhimizana ili wale wenye uwezo wawasaidie Waislamu wengine kwenda kufanya ibada hio kwa kuzingatia miongozo ya dini iliyopo kwani watu wanaosaidia katika mambo ya kheri bila ya shaka wana ujira mkubwa mbele ya Allah.
“Ilivyokuwa leo tunasherehekea sikukuu ya Idd el Hajj, ni wajibu kuhakikisha kuwa furaha hio ipo katika familia kwa kula vizuri, kuvaa vizuri na kuendeleza furaha kwa ndugu na majirani”,alisema Alhaj Dk. Shein.
Aliwataka wananchi kujitahidi kuwalea watoto sambamba na kuwarithisha misingi ya kuheshimu, kukinai na kuthamini vilivyo vyao kwani hiyo ni misingi ya uzalendo pamoja na kuwafunza maadili mema, silka, desturi na utamaduni waliourithisha kutoka kwa wazee.
Aliongeza kuwa miongoni mwa mapenzi makubwa ambayo mzazi anawajibika kwa mtoto wake ni kuhakikisha kuwa anapata elimu ya dini na dunia kwani kumpa mtoto elimu ni haki yake ili aweze kupata ufunguo huo muhimu wa maisha yake.
Alhaj Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo kueleza kuwa Wazanzibari wote wanaungana na Watanzania wenzao katika maombolezo kama alivyotangaza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli siku tatu kuanzia juzi Jumaamosi tarehe 10, Agosti 2019 ambapobendera zote zitapepea nusu mlingoti katika maeneo yote ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Hatua hiyo imetokana na ajali ya kuanguka na kuripuka kwa lori la mafuta katika eneo la Msamvu Mkoani Morogoro na kusabisha vifo vya watu Zaidi ya 64 na majeruhi kadhaa ambapo tukio hilo limetokea wakati wananchi wakiwa katika matayarisho ya sikukuu ya Idd el Hajj tarehe 10, Agosti, 2019.
Alhaj Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwapongeza vijana wote waliofaulu kwa daraja za juu katika mitihani yao ya Kidato cha Sita mwaka 2019 kwani anaamini kwamba wale waliojitahidi na waliojiandaa vizuri ndio wengi katika waliopata matokeo bora zaidi kwani juhudi ndio shina la mafanikio huku akiwapongeza wazazi, walimu na skuli zote zilizofanya vizuri.
Sambamba na hayo, Alhaj Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuiagiza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali wazitafute sababu zilizopelekea baadhi ya skuli kuwa miongoni mwa skuli kumi za mwisho katika matokeo hayo na hatimae waandae mbinu za ufumbuzi ambazo zitaleta mafanikio hapo baadae.
Katika hotuba yake hiyo pia, Alhaj Dk. Shein aliwahakikishia wananchi wote kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imetenga fedha za kutosha, ili kuendelea kutoa huduma za afya na elimu bure kama zilivyoelezwa kwenye Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2015/2020.
Alhaj Dk. Shein alitoa wito kwa wananchi kuendelea kufanya kazi kwa bidiii ili uchumi ukue kwa kasi kubwa na hatimae iweze kutekelezwa mipango yote kwa ufanisi zaidi.
Rais Dk. Shein kwa mara nyengine tena alitumia fursa hiyo kuwakumbusha viongozi na watendaji wote wa Serikali kwamba waengeze kasi, bidii na ari katika kuyatekeleza majukumu yao ya kuwatumikia wananchi kwa ufanisi kwa kuzingatia bajeti iliyopitishwa na fedha zilizoidhinishwa kwa mwaka 2019/2020.
Miongoni mwa viongozi waliohudhuria hafla hiyo ni Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Rais Mstaafu wa Zanzibar Dk. Amani Abeid Karume na viongozi wengineo wa vyama vya siasa, serikali pamoja na Taasisi za Kijamii.
Mapema asubuhi Alhaj Dk. Shein aliungana na waumini mbalimbali wa Dini ya Kiislamu katika Sala ya Idd el Hajj pamoja na hotuba vyote vilivyofanyika katika viwanja vya Beit Al Raas ambayo vyote kwa pamoja viliongozwa na Sheikh Twaha Hussein Twaha kutoka Kianga.
Katika hotuba yake hiyo ya Idd Sheikh Twaha alieleza umuhimu wa ibada ya Hijja kwa Waumini wa Dini ya Kislamu huku akisisitiza haja ya kuimarisha amani na utulivu nchini na kuepuka kuivunja kwa maneno na hata vitendo.
Baada ya hapo Alhaj Dk. Shein alifika Ikulu ndogo ya Kibweni ambako alisalimiana na Masheikh mbalimbali wakiwemo Masheikh kutoka Wilaya ya Magharibi “A” na kutakiana kheir ya Sikukuu ya Idd El Hajj.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.