Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akimsikiliza  mgeni wake Balozi wa Jamhuri ya Korea Nchini Tanzania Mhe.CHO Taeick wakati wa mazungumzo yao yaliyofanyika leo katika ukumbi wa Ikulu Mjini Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameipongeza Jamhuri ya Korea kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar na kusisitiza haja ya kuwepo ushirikiano katika sekta ya utalii baina ya pande mbili hizo.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Jamhuri ya Korea nchini Tanzania CHO Taeick.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa Zanzibar imeweza kuimarika katika sekta ya utalii kutokana na vivutio kadhaa vilivyopo sambamba na mikakati madhubuti iliyowekwa hivyo, ni jambo la busara iwapo watalii kutoka Jamhuri ya Korea watakuja kwa wingi kuitembelea Zanzibar.

Aliongeza kuwa katika kuhakikisha uhusiano na ushirkiano unaimarika zaidi kati ya pande mbili hizo hasa katika sekta ya utalii ipo haja ya kuwepo mashirikiano kati ya Zanzibar na kisiwa cha Cheju kiliopo Jamhuri ya Korea ambacho ni maarufu duniani katika sekta ya utalii.

Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza kwamba katika kuhakikisha mafanikio zaidi yanapatikana kwenye mashirikiano katika sekta ya utalii ipo haja ya kuanzisha safari za ndege kati ya Zanzibar na Jamhuri ya Korea kupitia Shirika la ndege la Korea.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuipongeza Jamhuri ya Korea kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo.

Rais Dk. Shein alisema kuwa Jamhuri ya Korea imekuwa mshirika mwema wa maendeleo ya Zanzibar kwani imekuwa ikionesha juhudi zake na kuwa bega kwa bega na Zanzibar katika kuimarisha miradi hiyo ya maendeleo.

Alieleza kuwa mbali ya Jamhuri ya Korea kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika sekta hizo za maendeleo pia, alieleza haja ya kutoa mashirikiano kwa kuisaidia Zanzibar katika kutoa mafunzo kwa mafundi wa Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC) Televisheni.

Alieleza haja ya kupatiwa mafunzo hayo ni kutokana na Shirika hilo kuanza kuwa na upungufu wa wataalamu hao ambao ndio rasilimali muhimu katika kuendesha Shirika hilo kutokana na wakati uliopo kutokana na wataalamu hao wengi  kufika muda wao wa kustaafu kazi.

Alisisitiza kwamba kuwepo kwa mitambo mipya pamoja na vifaa kadhaa vilivyonunuliwa na Serikali hivi karibuni kwa ajili ya kuendesha kituo hicho cha televisheni itakuwa ni jambo la busara ikienda sambamba na uwepo wa mafundi wataalamu katika Shirika hilo.

Rais Dk. Shein alisema kwamba miongoni mwa sekta ambazo Jamhuri ya Korea imekuwa ikiiunga mkono Zanzibar katika kuziimarisha hapa nchini ni pamoja na sekta ya kilimo, hasa kilimo cha mpunga wa umwagiliaji maji.

Rais Dk. Shein alisema kuwa tokea Jamhuri ya Korea kuanza ushirikiano na uhusiano wa Kidiplomasia kati yake na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar mnamo mwaka 1992, imeweza kuisaidia kwa kiasi kikubwa Zanzibar katika kuendeleza sekta za maendeleo ikiwemo kilimo, elimu, uvuvi na nyenginezo.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa Jamhuri ya Korea imeweza kusaidia katika ujenzi wa skuli ya kisasa ya Sekondari ya Kwarara ambayo pia, ina studio ya matangazo pamoja na vifaa mbali mbali vya habari kwa ajili ya mafunzo na utoaji elimu kwa wananchi.

Aliongeza kuwa Jamhuri ya Korea pia, imeweza kusaidia uanzishaji wa Kituo cha kutotolea vifaranga vya samaki wakiemo kaa na majongoo ya baharini kilichopo Beit el Ras ikiwa ni jitihada za kuhakikisha sekta ya uvuvi na ufugaji vinaimarika sambamba na kupanua soko la ajira kwa vijana.

Rais Dk. Shein pia, aliipongeza Jamhuri ya Korea kwa kuendelea kuwa mshirika mzuri wa maendeleo ya Zanzibar kwa kuweza kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika mikakati yake ya kupambana na umasikini pamoja na kutekeleza Dira ya Maendeleo ya Zanzibar ya 2020.

Nae Balozi Balozi wa Jamhuri ya Korea nchini Tanzania CHO Taeick  aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein kwa kuendeleza uhusiano na ushirikiano wa kidugu kati ya pande mbili hizo.

Balozi huyo wa Jamhuri ya Korea alizipongeza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kuendelea kuviweka vizuri vivutio vya kitalii sambamba na mazingira ya Zanzibar ili yaweze kuwavutia wageni wanaokuja kuitembelea Zanzibar.

Alieleza kuwa ni jambo la faraja iwapo mashirikiano yataimarishwa zaidi kati ya pande mbili hizo hasa katika sekta ya utalii kwani Zanzibar ina vivutio vingi vya kitalii na watu wa Korea wanapenda kuja kuviona.

Balozi huyo alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Jamhuri ya Korea iko tayari kuiunga mkono Zanzibar katika kuhakikisha Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC) Televisheni linapata mafundi wataalamu kwa ajili ya kuliendesha Shirika hilo ili liendeleze ubora wake.

“Jamhuri ya Korea iko tayari kushirikiana na Zanzibar katika kuwapata mafunzi wataalamu kwani kuna methali isemayo samaki mkunje angali mbichi na pia, kuna nyengine isemayo mbuyu ulianza kama mchicha hivyo ni vyema vijana wakapata mafunzo ili waje kuwa wataalamu wa Shirika hilo”,alisisitiza Balozi CHO Taeick

Aidha, Balozi CHO Taeick alimueleza Rais Dk. Shein kwamba Jamhuri ya Korea itahakikisha miradi yote iliyoahidi inatekelezwa vyema tena kwa wakati ukiwemo mradi wa kilimo cha mpunga wa umwagiliaji maji.

Sambamba na hayo, Balozi CHO Taeick alimueleza Rais Dk. Shein kwamba mashirika ya Jamhuri ya Korea likiwemo Shirika la Maendeleo la Jamhuri ya Korea (KOICA) litaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo.

Pia, Balozi huyo alieleza kuwa kupitia programu ya Kijamii ya Jamhuri ya Korea (SAMAUL)  imewawezesha wananchi wa kijiji cha Cheju na Kibokwa kunufaika na mradi wa skuli ya awali, mafunzo ya amali yakiwemo kilimo cha mpunga, mboga na ufugaji.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.