Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
Ummy Mwalimu akizungumza na wataalam wa Afya na Maendeleo ya Jamii mkoa wa
Katavi wakati wa ziara yake mkaoni humo kujionea shughuli za Afya na Maendeleo
ya Jamii.
Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Katavi ambaye ni Mkuu wa
Wilaya ya Mpanda Mhe. Lilian Matinga akisoma taarifa ya mkoa kuhusu Sekta ya
Afya na Maendeleo ya Jamii kwa Waziri anayesimamia Sekta hizo Ummy Mwalimu wakati
wa ziara yake mkaoni humo kujionea shughuli za Afya na Maendeleo ya Jamii.
Picha zote na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini WAMJW
Na Mwandishi Wetu Katavi
Mkoa wa Katavi umeiomba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii,
Jinsia, Wazee na Watoto kuratibu ufanywaji wa tafiti mpya kuhusu hali ya mimba
na ndoa za utotoni mkoani humo ambapo kwa tafiti zilizopo una asilimia 45 ya
mimba na ndoa na mimba za utotoni.
Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Katavi ambaye ni Mkuu wa
Wilaya ya Mpanda Mhe. Lilian Matinga ameyasema hayo leo mkoani Katavi wakati wa
ziara ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy
Mwalimu alipotembelea mkoani humo kujionea shughuli za Afya na Maendeleo ya
Jamii.
Mhe. Lilian Matinga amesema kuwa tatizo la mimba na ndoa za
utotoni bado ni changamoto mkoani humo na limekuwa likichangiwa na wanajamii
kwa kuwaozesha watoto wakiwa bado shuleni.
"Niseme bado mkoani kwetu kuna tatizo la ndoa na mimba
za utotoni na ukiangalia watoto wengi wanaolewa na wazee wa miaka 50 na
zaidi" alisema Mhe. Lilian
Ameongeza kuwa Mkoani unaendeleza jitihada za Wizara katika
kuhakikisha tatizo la ndoa na mimba za utotoni linapatiwa ufumbuzi wa kudumu
kwani limekuwa likikatisha ndoto za watoto wengi wa kike kupata elimu.
Aidha ameishukuru Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuweka
msisitizo kwa jamii katika mapambano dhidi ya mimba na ndoa za utotoni nchini.
Akijibu ombi hilo Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii,
Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu amesema kuwa Wizara kwa mwaka 2020
itaratibu tafiti ya jumla kuhusu tatizo la mimba na ndoa za utotoni na
kusisitiza Maafisa Maendeleo ya Jamii kuratibu ukusanyaji wa taarifa za mimba
na ndoa za utotoni na kupata picha kamili ya mafanikio ya mapambano hayo.
" Tutashirikiana na Ofisi ya Taifa ya Takwimu kufanya
tafiti ili tujue tumefikia wapi na kwa asilimia ngapi katika kuondokana na
tatizo la ndoa na mimba za utotoni nchini" alisema Waziri Ummy.
Pia Waziri Ummy amewataka wakuu wa shule za Misingi na
Sekondari kuhakikisha wanakusanya taarifa za wanafunzi wa kike wanaoacha masomo
kwa sababu za mimba na kuolewa na kuhakikisha zinawasilishwa kwa Kamishna wa
elimu.
No comments:
Post a Comment