Habari za Punde

Kikosi cha Timu ya Taifa ya Zanzibar Heroes Chapongezwa Wakati wa Hafla ya Chakula Maalum Walichoandaliwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk Shein Ikulu Jijini Zanzibar leo.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akiwapongeza Wachezaji wa Timu ya Taifa ya Zanzibar Heroes kwa kuiwakilisha  vizuri Zanzibar katika michuano ya Chalenji kwa mwaka 2019 yaliofanyika Nchini Uganda, (kulia kwa Rais) Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Balozi Seif Ali Iddi, Jaji Mkuu wa Zanzibar.Mhe Omar Othman Makungu na Waziri wa Vijana Michezo Sanaa na Utamaduni Mhe.Balozi Ali Karume, wakijumuika na Wachezaji wa Timu ya Taifa ya Zanzibar katika chakula Maalum kilichofanyika Ikulu Jijini Zanzibar. 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ametoa pongezi kwa wachezaji wa timu ya “Zanzibar Heroes” na viongozi wao kwa kuweza kuiwakilisha kwa nidhamu ya hali ya juu Zanzibar katika mashindano ya Chalenji ya mwaka 2019 na kutoa upinzani mkubwa kwa timu zote waliocheza nazo.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo Ikulu mjini Zanzibar katika hafla ya chakula cha mchana alichowaandalia wachezaji wa timu ya “Zanzibar Heroes” ambao wameshiriki mashindano ya Chalenji ya mwaka huu wa 2019 huko nchini Uganda pamoja na kuwapa zawadi ya fedha taslim.

Akisoma hotuba kwa niaba ya Rais Dk. Shein, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Ussi Haji Gavu alisema kuwa hata hivyo kwa mara hii bahati haikuwa kwa upande wa “Zanzibar Heroes” kama ilivyokuwa mwaka jana lakini timu hiyo imeendelea kuwa tishio katika mashindano hayo.

“Tumepoteza mechi mbili kwa kufungwa bao moja kwa kila mechi na tumetoka sare mechi moja,.nawapongeza wachezaji wote  mcheza kwao hutunzwa hapigwi”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa “Zanzibar Heroes” imeonesha upinzani na ufundi wa hali ya juu lakini kwenye mpira wataalamu wanasema kwamba kosa moja dogo linaweza kukugharimu “One mistake One goal”.

Rais Dk. Shein alisema kuwa wananchi wote wa Zanzibar wanahisi maumivu na machungu ya kupoteza mechi hizo kama vile wanavyohisi wao wachezaji wa “Zanzibar Heroes”.

Alitoa pongezi kwa wananchi wote wa Zanzibar kwa hamasa waliyoionesha na kwa kuiunga mkono timu hiyo wakati wote wa mashindano hadi hivi sasa “Baraza zote zilijaa washabiki na wapenzi wakiwa na simanzi wakati mlipokuwa mkicheza”,alisisitiza Rais Dk. Shein.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliwapongeza wachezaji hao kwa kuiwakilisha Zanzibar kwa heshima na nidhamu ya hali ya juu jambo ambalo limelinda sifa ya watu wa Zanzibar.

Akimnukuu Rais wa 13 wa Marekani, Marehemu Millar Fillmore ambaye alisema kuwa ‘kushindwa ikiwa bado umelinda heshima yako ni bora kuliko kupata ushindi baada ya kuvunja heshima yako’.
“Tunakupongezeni wachezaji wetu wa “Zanzibar Heroes” kwa kuendelea kutuwakilisha mkiwa na heshima kubwa na kulinda sifa njema za watu wa Zanzibar kupitia mashindano mnayotuwakilisha”,alisema Dk. Shein.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa yeye anamatumaini makubwa na ubora wa timu ya “Zanzibar Heroes” pamoja na viongozi na Mwalimu wa timu hiyo Hemed Suleiman Moroco na ndio maana kwa mara nyengine  ameamua kuwaalika Ikulu ili wafarajike na kupata chakula cha mchana pamoja.

Alieleza kuwa Serikali inathamini jithada za watu wote walioisaidia timu hiyo tangu hatua za maandalizi hadi kuiwezesha kushiriki mashindano ya mwaka huu wa 2019 huko nchini Uganda.

Akitoa nasaha zake Rais Dk. Shein alisema kuwa kila mmoja anapaswa kuendeleza umoja na kushirikiana zaidi katika kuisaidia timu ya Taifa ya Zanzibar, “Zanzibar Heroes” na timu zote zinazoshiriki katika michezo ya Kitaifa na Kimataifa.

Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuendelea kupeana moyo na kuzingatia wapi timu imejikwaa iwe kwenye maandalizi ya timu au katika mbinu za kutafuta ushindi na mambo mengine yote ambayo yatawezesha kufanya vizuri hapo baadae.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa katika kuimarisha sekta ya michezo ikiwa ni pamoja na kuimarisha miundombinu ya michezo hapa Zanzibar.

Nae Kocha Mkuu wa “Zanzibar Heroes” Hemed Suleiman Moroco alieleza kuwa Rais Dk. Shein ameonesha ujasiri na amewapa nguvu ya kuendelea kufanya vizuri zaidi na kuahidi kufanikisha ahadi yake ya kuiletea ushindi Zanzibar katika mashindano yajayo.

Alimpongeza Rais Dk. Shein kwa kuendelea kuwapa nguvu na amekuwa na mchango mkubwa katika timu hiyo tokea wakiwa kambini mpaka wakati wakiendelea na mashindano hayo na kupelekea kuwavutia watu wengi wakati wakiwa Uganda.

Kocha Moroco alitumia fursa hiyo kutoa maombi yake kwa Serikali katika kuhakikisha timu ya “Zanzibar Heroes” inapata maandalizi mazuri wakati wote na iwe ikishiriki mashindano mbali mbali ya kirafiki ya ndani na nje ya nchi.

Aidha, alisema kuwa katika maandalizi mazuri ya timu hiyo ipo haja ya kushiriki mashindano mbali mbali yakiwemo mashidano ya nchi za visiwa huku akisisitiza kuwa Zanzibar bado mpira unaendelea vyema.

Alimpongeza Rais Dk. Shein kwa kuwaandalia chakula hicho cha mchana hapo Ikulu na kueleza kuwa wanathamini jitihada  za Rais wa Zanzibar katika kuiendeleza na kuikuza sekta ya michezo hapa nchini.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.