Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) ofisini kwake Mtumba, jijini Dodoma leo kuhusu ajira kwa vijana waliohitimu mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa “Operesheni Magufuli” na masuala mbalimbali ya kiutumishi. Kulia ni Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Dkt. Francis Michael.
Baadhi ya waandishi wa habari wakimsikiliza Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro (hayupo pichani) wakati wa mkutano uliofanyika ofisini kwake Mtumba, jijini Dodoma leo.
Na. Happiness .Shayo.23/12/2019
Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli ameelekeza vijana wote wenye elimu
ya Shahada ya Kwanza waliohitimu mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) “Operesheni
Magufuli” kupewa ajira katika
taasisi mbalimbali za serikali.
Hayo yamesemwa na Katibu
Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro
wakati wa mkutano na waandishi wa habari uliofanyika ofisini kwake eneo la
Mtumba jijini Dodoma leo.
“Serikali imekuwa ikiwajengea
vijana uadilifu, umoja, mshikamano, moyo wa kujitolea, moyo wa uzalendo,
nidhamu na ari ya kupenda kufanya kazi kwa kuwaingiza kwenye mafunzo ya Jeshi
la Kujenda Taifa, hivyo kwa kutambua mchango wao, Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli
ameagiza wapewe ajira’’ Dkt. Ndumbaro amesisitiza.
Dkt. Ndumbaro ametaja sifa
za vijana waliohitimu JKT kuwa ni lazima wawe wametumikia kwa kipindi
kisichopungua miaka miwili na kwamba wanatakiwa kuwasilisha taarifa zao
binafsi, vyeti vya elimu, taaluma na vyeti vya kuhitimu mafunzo ya JKT katika
Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kupitia barua
pepe ya ps@utumishi.go.tz.
Aidha, Dkt. Ndumbaro
ametumia fursa hiyo kuwaasa waajiri wanaowarejesha makazini watumishi wa umma
walioghushi vyeti vya elimu na taaluma kwa visingizio kwamba waliondolewa
kimakosa au waliajiriwa kabla ya tarehe 20 Mei, 2001 kwa sifa ya Elimu ya
Darasa la Saba.
“Serikali haitosita
kumchukulia hatua mwajiri yeyote atakayekiuka maelekezo halali yaliyotolewa na
Serikali kuhusiana na hatua zilizochukuliwa dhidi ya watumishi walioghushi vyeti”
Dkt. Ndumbaro amesema.
Akizungumzia suala la
udanganyifu na upendeleo katika upandishwaji vyeo, Dkt. Ndumbaro amesema kuwa
ofisi yake imebaini baadhi ya waajiri kuwasilisha taarifa za uongo Ofisi ya
Rais-Utumishi ili kuwapandisha vyeo watumishi kwa lengo la kuwanufaisha baadhi
yao bila kuwa na vigezo vilivyowekwa kwa mujibu wa Sheria na Kanuni
zinazosimamia Utumishi wa Umma.
“Ofisi yangu itaendelea
kuwachukulia hatua stahiki waajiri watakaobainika kufanya udanganyifu kwa
madhumuni ya kuipotosha Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na
Utawala Bora ili iweze kutoa vibali vya kuwapandisha vyeo watumishi
isivyostahili” Dkt. Ndumbaro amefafanua.
Dkt. Ndumbaro amehitimisha
mkutano huo kwa kuwataka Maafisa Utumishi nchini kufanya kazi kwa weledi kwa
kufuata Sheria, Kanuni na Taratibu za Utumishi wa Umma badala ya kuwa chanzo cha
kero na matatizo ya kiutumishi.
Mkutano kati ya Katibu Mkuu,
Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro na
waandishi wa habari ulikuwa na lengo la kuuhabarisha umma juu ya masuala
mbalimbali ya kiutumishi.
No comments:
Post a Comment