Waziri
wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira Mhe. George Simbachawene
amekemea watu wanaojihusisha na vitendo vya kuhujumu miundombinu ya umma na ya
watu binafsi ili kwenda kuuza kama chuma chakavu kuacha mara moja.
Pia
amezitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa kupitia Halmashauri zote nchini
zifuatilie watu binafsi, kampuni na viwanda kuhakikisha kuwa sheria na kanuni
za udhibiti wa taka hatarishi zinazingatiwa ipasavyo hali ambayo itachangia
katika udhibiti wa uchafuzi wa mazingira.
Simbachawene
amesema hayo leo ofisini kwake jijini Dodoma wakati akitoa taarifa kuhusu kanuni
za udhibiti na usimamizi wa taka hatarishi za mwaka 2019, kanuni za udhibiti na
usimamizi wa taka za kielektroniki za mwaka 2019 na kanuni za ada na tozo za
usimamizi wa mazingira za mwaka 2019.
Alisema
hatua iliyochukuliwa na Ofisi hiyo ya kufanya marekebisho katika kanuni hizi na
kuweka mfumo bora wa kisheria wa kusimamia taka hatarishi inalenga sio tu kuhakikisha
kuwa mazingira yanalindwa na kusimamiwa bali pia miundombinu ya nchi inalindwa
ipasavyo.
“Kama
tunavyofahamu, mojawapo ya taka hatarishi ni chuma chakavu, kuna baadhi ya
wafanyabiashara na watu ambao sio waaminifu wanafanya biashara hii bila kuwa na
vibali husika, lakini pia wapo ambao wana vibali lakini hawafuati masharti
yaliyowekwa chini ya vibali hivyo,” alisisitiza.
Aidha
waziri huyo aliwataka baadhi ya wanaofanya biashara hiyo huku wakikwepa kulipa
kodi stahiki kuacha udanganyifu huo kwani sasa Serikali imeweka mfumo wa
kiutawala, kisheria na kikanuni ambao sio rahisi kufanya udanganyifu huo tena
bila kugundulika.
Aliongeza
kuwa katika kuboresha usimamizi wa mazingira, Ofisi imefanya marekebisho ya
Kanuni mbalimbali pamoja na kutunga Kanuni Mpya zikiwemo za Udhibiti na Usimamizi
wa Taka Hatarishi za mwaka 2009.
Kanuni
zingine ni za Ada na Tozo za Usimamizi wa Mazingira za Mwaka 2008 na
marekebisho yake ya mwaka 2016 na 2018, pamoja na Kuandaa Kanuni mpya za
Udhibiti na Usimamizi wa Taka za Kielektroniki za Mwaka 2019.
Simbachawene
alifafanua kanuni mpya za mwaka 2019, zimeainisha aina ya shughuli za usimamizi
wa taka hatarishi ambazo zinapaswa kuwa na kibali cha Waziri mwenye dhamana ya
Mazingira akitaja shughuli zinazopaswa kuombewa kibali ndani ya nchi ni
kukusanya, kutunza, kusafirisha na kumiliki au kuendesha mtambo wa usimamizi wa
taka hatarishi.
Aidha,
shughuli za usafirishaji nje ya nchi, kuingiza au kupitisha nchini taka
hatarishi zinapaswa kuombewa kibali ambacho pia hutolewa na Waziri husika na
zimeelekeza shehena yoyote ya taka hatarishi itakayoingizwa au kupitishwa
nchini bila kufuata masharti ya Kanuni hizi, itachukuliwa kuwa ni usafirishaji
haramu wa taka hatarishi na zinapaswa kurejeshwa katika nchi zilikotoka kwa
gharama za msafirishaji.
Waziri
Simbachawene aliongeza kuwa kanuni hizi zimeweka adhabu kali zaidi kwa makosa
ya kutokuwa na kibali cha kusimamia taka hatarishi nchini zikiwemo faini
kuanzia sh. milioni tano hadi bilioni 10 au kifungo kisichozidi miaka 12 au vyote
kwa pamoja.
“Napenda kusisitiza kuwa hatua hii
iliyochukuliwa na Ofisi ya Makamu wa Rais ya kufanya marekebisho katika Kanuni
hizi na kuweka mfumo bora wa kisheria wa kusimamia taka hatarishi inalenga sio
tu kuhakikisha kuwa mazingira yanalindwa na kusimamiwa bali pia miundombinu ya
nchi inalindwa ipasavyo.
“Kama tunavyofahamu, mojawapo ya taka
hatarishi ni chuma chakavu, kuna baadhi ya wafanyabiashara na watu ambao sio
waaminifu wanafanya biashara hii bila kuwa na vibali husika, lakini pia wapo
ambao wana vibali lakini hawafuati masharti yaliyowekwa chini ya vibali hivyo.
Moja ya sharti muhimu ni kwamba kila mwenye kibali cha chuma chakavu anapaswa
kutoa taarifa ya chanzo cha chuma chakavu hicho na mahali anapokipeleka. Na
hiyo inafanyika kwa kujaza ‘tracking form’ namba 3, kutokufanya hivyo ni
kosa kubwa chini ya Kanuni hizi,” alitahadhatrisha.
No comments:
Post a Comment