Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akiwapungia mkono Washiriki wa Mazoezi ya Viungo Zanzibar wakiingia katika Uwanja wa Mao Zedong kumalizia matembezi hayo na kufanya mazoezi ya Viungu katika Uwanja huo.
KUADHIMISHA Siku ya Mazoezi ya Viungo Kitaifa katika
mwezi wa Januari kila mwaka ni kielelezo muhimu katika historia ya ukombozi wa
wananchi wa Zanzibar ambao walikandamizwa kwa miongo mingi na wakoloni.
Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein
aliyasema hayo leo
huko katika uwanja wa Mao Dzedong katika Tamasha la Siku ya Mazoezi Kitaifa
baada ya kuongoza matembezi yaliyoanzia katika viwanja vya Baraza la
Wawakilishi la zamani kuelekea Mkunazini, Kariakoo, Magereza, Kilimani na
kumalizikia katika uwanja huo wa Mao.
Katika maelezo yake,
Rais Dk. Shein ambaye pia, ni muasisi wa Tamasha hilo alisema kwamba
maadhimisho hayo huwa yanaufungua mwaka mpya, tukio ambalo linashabihiana na
ufunguzi wa ukurasa mpya katika utawala wa wanyonge hapa Zanzibar.
Alieleza kuwa mazoezi hayo yanafanyika mwanzoni mwa mwezi
wa Januari ambao ndio mwezi wa heka heka na harakati za kuung’oa utawala wa
kikoloni hapa Zanzibar.
Aliongeza kuwa katika
Mapinduzi hayo matukufu ya Januari 12, 1964 wananchi hawakuwa na silaha za
kisasa kwa ajili ya mapambano, bali walikuwa na ari, uzalendo, hamu ya kujikomboa
na kuiongoza nchi yao wenyewe.
Hivyo, alisisitiza
kuwa inapoadhimishwa siku ya mazoezi ya viungo
kila mwaka katika mwezi huu wa Januari ni wajibu wa kila mmoja
kutafakari umuhimu wa maadhimisho hayo kwa mnasaba wa Mapinduzi matukufu ya
Januari 12, 1964 ambayo yaliteta ukombozi, haki na usawa kwa wananchi wote.
“Mazoezi ya viungo ni
kama chumvi katika chakula , maana chumvi ni kiungo muhimu kwenye chakula kwa
kila chakula kinachopaswa kutiwa chumvi na ndio maana waimbaji wakaisifu
chumvi”, alisisitiza Rais Dk. Shein.
Aidha, Rais Dk. Shein
alisema kuwa sekta ya michezo hapa nchini imejenga historia kubwa katika
harakati za kisiasa kuelekea Mapinduzi matukufu ya Januari 1964 ambayo yaliandaliwa
na kufanywa na Chama Cha Afro Shirazi (ASP) ambacho kilitokana na Chama cha
“African Association” na “Shirazi Association” ambapo “African Association”
kilikuwa ni matokeo ya klabu ya michezo ya vijana wa Kiafrika.
Alisema kuwa kwa
kutambua umuhimu wa michezo kwa maendeleo ya Zanzibar, Awamu zote Saba za uongozi
wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zimefanya jitihada mbali mbali za kuimarisha
sekta ya michezo, ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya michezo hasa viwanja vya
michezo.
Aidha, alisema Ilani
ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2015-2020, imeielekeza Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar, kuufanyia marekebisho makubwa uwanja wa Mao Dzedong jambo ambalo
limeshatekelezwa kwa mafanikio pamoja na kujenga viwanja vitano vya michezo
katika kila Wilaya.
Rais Dk. Shein alitoa
wito kwa Wizara ya Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na Wizara ya
Elimu na Mafunzo ya Amali, wazidi kushirikiana katika kuufanikisha utekelezaji
wa mpango maalum wa kuendeleza michezo yaani “Sport 55” ili kufikia lengo la
kuirejesha hadhi Zanzibar ya kufanya vyema katika michezo mbali mbali ya
Kitaifa na Kimataifa.
Dk. Shein aliwanasihi
wananchi wote waendelee kuithamini timu ya Taifa ya Zanzibar, “Zanzibar Heroes”
na kuipa moyo na kwa pamoja kuzingatia wapi kumefanyika kosa tangu mwanzo wa
matayarisho hadi katika mashindano yenyewe ili kuweza kutafuta mbinu na njia za
kufanya marekebisho kwa lengo la kufanya vizuri zaidi.
Aliongeza kuwa
wachezaji wa Timu hiyo ambao aliwaalika Ikulu mnamo Disemba 17, mwaka jana 2019,
katika hafla ya chakula cha mchana alichowaandalia walistahiki kupongezwa kwa
kuonesha upinzani na ufundi wa hali ya juu katika mchezo kiasi ya kwamba
waliendelea kuwa tishio kwa timu nyengine.
Alisisitiza na kutoa
wito kwa viongozi wa ZFF na BMZ waanze maandalizi ya kuiandaa timu ya “Zanzibar
Heroes” mapema kwa mfano wachezaji wajulikane na maandaliwe mapema na viongozi
watakaosimamia kamati za ushindi nao wajulikane mapema.
Rais Dk. Shein alitoa
wito kwa Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais, Idara ya Watu wenye Ulemavu, Wizara
ya Elimu na Mafunzo ya Amali na Wizara ya Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo
wapange mkakati maalum wa kuwashirikisha Watu wenye Ulemavu katika michezo
mbali mbali ambayo wanaimudu kutokana na hali zao za viwiliwili.
Rais Dk. Shein ameutoa
wito huo kutokana na kuona kwamba katika jitihada za kukuza sekta ya michezo,
bado hawajashirikishwa ipasavyo Watu wenye Ulemavu.
Hivyo, alisisitiza kwamba
itakuwa ni jambo la busara na la kupendeza iwapo vijana wenye ulemavu
watatayarishwa vizuri katika michezo wanaoimudu na kushirikishwa kuicheza
katika Tamasha la Elimu bila Mapilipo au katika shamrashamra za maandhimisho ya
Sherehe za Mapinduzi.
Mapema Waziri wa Nchi
Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais Mohamed Aboud alieleza azma ya Tamasha hilo na
kusisitiza umuhimu wake katika kukuza umoja, ushirikiano na mshikamano sambamba
na kuhuisha afya kwa wafanyaji wa mazoezi.
Nae Kamishna wa
Michezo Zanzibar, Sharifa Khamis alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Rais Dk.
Shein kwa kuendelea kuliunga mkono Tamasha hilo sambamba na kuendelea
kuiimarisha sekta ya michezo hapa nchini.
Nao wafanyamazoezi ya
viungo katika risala yao iliyosomwa na Sihaba Mohamed walieleza jinsi
walivyofarajika na uongozi wa Rais Dk. Shein na kumpongeza kwa dhati kwa
kuijenga Zanzibar katika kipindi cha uongozi wake wa miaka 10 na kumuomba
Mwenyezi Mungu amjaalie amalize salama muda wake wa Urais kwa uzima na afya.
Walieleza kuwa ni
dhahiri kwamba Rais Dk. Shein ameitumikia Zanzibar ipasavyo na kwa moyo wake
wote katika uhakikisha kwamba anailetea maendeleo katika nyanja ya kiuchumi,
kisiasa na kijamii hali ambayo kila mmoja anaiona.
Aidha, walieleza kuwa
wao wanamazoezi amewawekea kumbukumbu ya kujivunia tangu alipolitangaza tamasha
hilo kuwa la Kimataifa mwaka 2014 walipomualika kuwa Mgeni Rasmi kwenye Bonanza
lao la lililofanyika huko katika uwanja wa Amaan mjini Unguja.
“Tunamuomba Mwenyezi
Mungu aendelee kukupa imani ya kuitumikia nchi yetu na tunakuomba hata pale
utakapopumzika basi ibaki akilini mwako kuwa Tamasha hili bado ni lako na
uendelee kujumuika nasi mwaka hadi mwaka”, walieleza wanamazoezi hao.
Rais Dk. Shein
aliungana na wanamazoezi hao kwa kumshukuru kwa dhati Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Dk. John Joseph Pombe Magufuli kwa kumteua Amina Talib
ambaye ni Katibu wa (ZABESA), kuwa Kamishna wa Tume ya Haki za Binaadamu na
Utawala Bora.
Alisisitiza haja kwa
Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale pamoja na Wizara ya Vijana,
Utamaduni, Sanaa na Michezo kushierikiana pamoja kulitumia Tamasha la Utalii la
Zanzibar ili kuingiza michezo ya riadha, kuogelea na resi za baiskeli ambayo
anaamini kwamba watalii wataifurahia sana.
Wanamazoezi hao
waliiomba Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Maendeleo ya Wanawake na Watoto kwa
kushirikiana na Chama cha Mazoezi Zanzibar (ZABESA) kuandaa mpango wa kuwapatia
taaluma ya ujasiriamali na mikopo ili waweze kujikwamua kimaisha.
Kwa maelezo ya
wanamazoezi hao, ujumbe wa mwaka huu wa 2020 wa Tamasha hilo unalenga kwenye umuhimu
wa mazoezi lakini pia, mikusanyiko yao hiyo iwaletee maendeleo kwa maana ya
kwamba walenge pia, kujikwamua kiuchumi.
Sambamba na hayo,
wanamazoezi hao walimpongeza Rais Dk. Shein kwa kuendelea kuilinda na kuitunza
amani na utulivu wa nchi sambamba na kuwaletea maendeleo makubwa ambayo leo hii
wananchi wanajivunia.
Pia, walitumia fursa hiyo
kulishukuru Shirika la Bandari Zanzibar kwa kuendelea kuwasaidia kufanikisha Tamasha
hilo na kumpongeza Mkurugenzi wa Shirika hilo kwa kuwasidia kutokana na kuelewa
umuhimu wa mazoezi na kuwapongeza wanamazoezi wa Unguja, Pemba na Tanzania Bara
pamoja na wananchi wote kwa ushiriki wao.
Katika Tamasha hilo,
Rais Dk. Shein alitoa vyeti maalum kwa washiriki wa Tamasha hilo kutoka Unguja,
Pemba na Tanzania Bara ambapo mapema wanamazoezi hao walipita mbele ya jukwa
kuu alilokaa Rais huku wakionesha umahiri wao wa mazoezi.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment