Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Azungumza na Uongozi wa Wizara ya Afya Zanzibar.


 
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Afya Zanzibar, wakati akipokea taarifa ya Utekelezaji wa Mpango Kazi kwa mwezi wa Julai hadi Disemba 2019 /2020, uliofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar na (kulia kwa Rais) Katibu Mkuu Jiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Abdulhamid Yahya Mzee, Waziri wa Afya Zanzibar Mhe. Hamad Rashid Mohammed. 
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuna umuhimu wa kutizama upya sheria zinazosimamia mwenendo wa usalama wa chakula nchini, ili kuondokana na malalamiko mbali mbali ya wafanyabiashara.

Dk. Shein ametowa ufafanuzi huo, wakati akipokea taarifa ya utekelezaji wa mpango kazi ya Wizara ya Afya, kwa kipindi cha kuanzia Julai hadi Disemba, 2019, hafla iliyofanyika Ikulu mjini hapa.

Alisema kuna umuhimu kwa Uongozi wa Wizara hiyo kuziangalia upya sheria zinazosimamia usalama wa chakula, hususan katika suala zima la ukaguzi wa bidhaa zinazotoka na kuingia nchini,    kwa kigezo cha kuwepo malalamiko kutoka kwa wafanyabaishara juu ya tozo wanayolipa kugharamia   ukaguzi huo.

Alisema wafanyabishara wamekuwa wakilalamikia gharama hizo, kwa kigezo kuwa dhima ya kuthibitisha ubora wa bidhaa  uko mikononi kwa Serikali badala ya wao kubebeshwa mzigo huo.

Alisema  pamoja na sheria zilizopo kuwa na uwiano katika nchi nne za Afrika Mashariki, kuna umuhimu wa kuzipitia upya kwa kuzingatia kuwa Serikali ndio yenye dhima katika kufanya utafiti na kupata matokeo.

Dk. Shein alieleza wafanyabiashara wamekuwa wakilalamikia kuwepo kwa utitiri wa taasisi za uchunguzi, jambo linaloongeza urasimu.

Alieleza kuwa mbali na taasisi hizo kuongozwa  na sheria yake kila moja, kuna umuhimu wa viongozi kukaa pamoja ili kuwa na mfumo maalum wa utoaji wa tozo moja.

Alisema Serikali haiwezi kupuuza malalamiko ya wafanyabiashara hao na kubainisha kuwa itafanya juhudi za kuzitafutia ufumbuzi changamoto hizo ili kuondokana na  malalamiko.

Aidha,   aliitaka Wizara hiyo kujikita katika suala la kusomesha na kuwaendeleza  wafanyakazi wake katika nyanja tofauti, ikiwemo za Injinia na nyengine zenye upungufu ili waweze kufanyakazi kwa ufanisi.

Alisema kuna umuhimu wa kuwa na program maalum ya mafunzo , itakayotoa fursa kwa wafanyakazi kusoma ndani na nje ya nchi, hatua aliyobainisha itaiwezesha Wizara kuwa na wataalamu wa kutosha katika kipindi kifupi.

Sambamba na hilo Dk. Shein alisisitiza umuhimu wa kufanya tafiti mbali mbali , ikiwa ni hatua muafaka katika kuzipatia ufumbuzi changamoto mbali mbali zinazojitokeza.

Rais Dk. Shein aliutaka uongozi wa Wizara hiyo kuhakikisha huduma zote za Maabara zinafanyika ndani ya Hospitali za Serikali badala ya kufanyika taasisi zanje, kwa kigezo kuwa Serikali imekuwa ikitenga kiwango kikubwa cha fedha na kubainisha kuwa huduma za maabara ndio msingi wa matibabu.

Aliushauri uongozi wa Wizara hiyo kuendleea kuviimarisha vituo vya Afya , hususan vile vilioko vijijini kisiwani Pemba kwa kuvipatia nyenzo, vifaa tiba na dawa, ili wagonjwa wasikimbilie hospitali ya Abdalla Mzee.

Aidha, aliipongeza Wizara hiyo kwa juhudi kubwa inazoendelea kuchukuwa katika kukabiliana na ugonjwa wa malaria, sambamba na kupunguza kiwango cha maambukizi ya virusi vya ukimwi kutoka asilimia 0.6 hadi kufikia asilimia 0.4.

Vile vile aliipongeza Wizara hiyo kwa kuandaa mpango mzuri wa taarifa yake, pamoja na hatua mbali mbali ilizozichukuwa kuimarisha huduma za Afya hapa nchini.

Nae, Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliupongeza uongozi wa Wizara ya Afya kwa kuandaa vyema taarifa hiyo ya utekelezaji.

Aidha, aumeutaka uongozi huo kufanya juhudi kukiimarisha kitengo cha mifupa katika Hospitali Kuu ya Mnazi mmoja, ikizingatiwa mahitaji makubwa yaliopo kutokana na kuwepo ongezeko kubwa la ajali za barabarani hapa nchini.

Mapema, Waziri wa Wizara Afya Hamad Rashid Mohamed akiwasilisha muhtasari wa utekelezaji wa mpango kazi wa Wizara hiyo, alisema katika kipindi hicho Wizara ilipanga kutumia zaidi ya shilingi Bilioni 57.8 , kati yake shilingi Bilioni 47.8 kwa ajili ya Idara na taasisi zilizozomo ndani ya Wizara hiyo na shilingi Bilioni 9.9 kwa ajili ya Hospitali ya Mnazimmoja.

Alisema Wizara ilipanga kukusanya zaidi ya shilingi Bilioni 4.6 kutoka vyanzo mbali mbali vya mapato ili kuchangia mfuko mkuu wa Serikali.

Alisema katika kipindi hicho Wizara hiyo imefanikiwa kutekeleza shughuli mbali mbali kwa mafanikio makubwa ikiwemo ununuzi wa dawa (shilingi bilioni nane), hivyo kuwezesha upatikanaji wa dawa muhimu katika vituo vya Afya na Hospitali kwa asilimia 90.

Aidha, alisema katika kipindi hicho gharama za usafirishaji wa wagonjwa nje ya nchi zilipungua kutoka shilingi 341,292,993 hadi  kufikia shilingi 32,186,488 .

Waziri Rashid alisema  Wizara ilifanikiwa kuajiri wafanyakazi 479, ikiwemo madaktari , wauguzi, fundi sanifu maabara na wataalamu wengine.

Alisema kupatikana kwa mashine ya CT Scan mpya katika Hospital ya Mnazimmoja kutapunguza mrundikano wa wagonjwa wanaosubiri huduma hiyo.

Kuhusiana na uimarishaji wa  miundombinu na majengo, Waziri huyo alisema  ujenzi wa Bohari kuu kisiwani Pemba unaendelea vizuri na unategemewa kukamilika ifikapo mwezi April, mwaka huu.

Alisema miongoni mwa changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji wa mpango huo ni pamoja na  mabadailiko ya ushuru kutoka Mamlaka ya Kukusaya ushuru Tanzania (TRA), ambayo kwa kiasi kikubwa umeathiri usafirishaji wa dawa muhimu kutoka MSD kwenda Bohari ya Dawa (CMS).

Nae, Mshauri wa Waziri katika Wizara hiyo, Dr. Mohamed Saleh Jidawi, alipongeza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, chini ya uongozi wa Rais Dk. Ali Mohamed Shein katika kuimarisha huduma za afya nchini.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.