UONGOZI wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali
za Mitaa na Idara Maalum za SMZ umetakiwa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi
juu ya matumizi ya Kamera pamoja na manufaa ya Mradi wa Mji Salama tangu
kuanzishwa kwake
Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo, Ikulu Jijini Zanzibar
alipokutana na uongozi wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na
Idara Maalum za SMZ wakati ilipowasilisha Utekelezaji wa Mpango Kazi kwa kipindi cha Julai hadi Disemba kwa mwaka
wa fedha 2019/2020.
Rais Dk. Shein alieleza kuwa Ofisi hiyo inapaswa
kutoa elimu kwa wananchi kupitia vyombo
vya habari kwa kuonesha vipindi vya matukio yanayopatikana kutokana na msaada
wa mradi wa Mji Salama kupitia CCTV zilizowekwa katika Jiji la Zanzibar hatua
ambayo itawapelekea wananchi kuuamini kuwa mradi huo unafanya kazi
ipasavyo.
Alieleza kuwa matukio hayo yakiwemo uvunjifu wa
sheria iwapo yataoneshwa katika vyombo va habari ikiwemo ZBC Televisheni wananchi
watapata kujua umuhimu na kazi za mradi huo kupitia CCTV zilizowekwa katika
maeneo yote ya Jiji la Zanzibar.
Rais Dk. Shein alisema kuwa wapo watu ambao bado hawaamini
kuwa kamera hizo za CCTV zilizowekwa katika eneo la Jiji la Zanzibar zinafanya
kazi na matukio kadhaa yanaonekana hiyo ni kutokana na kutokuwa na elimu yoyote
juu ya mradi huo.
Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa hatua hiyo pia,
itawapelekea wananchi kujua kuwa mradi huo unafanya kazi zake vyema na
unayagundua matukio kadhaa yanayofanywa katika Jiji la Zanzibar.
Alifahamisha kuwa wananchi hawaoni matukio ya kazi
za mradi huo kupitia vyombo vya habari kutokana na kutooneshwa hasa kwa yale ya
uvunjaji wa sheria na kueleza haja ya
kuoneshwa kwa wale wote wanaosimamia na wanaovunja sheria zikiwemo zie za barabarani.
Alieleza kuwa kutokana na mafanikio makubwa yaliopatikana
hapa Unguja Serikali hivi sasa imo katika mchakato wa kuuendeleza mradi huo kisiwani
Pemba hivyo, ipo haja kwa wananchi kuendelea kupewa elimu na kuelezwa mafanikio
ya mradi huo.
Aidha, Dk. aliongeza kuwa katika kuhakikisha vitendo vyote
vinavyohatarisha amani na usalama vinadhibitiwa ipasavyo Serikali imetekeleza mradi
huo ili wananchi na mali zao pamoja na wageni wanaoitembelea Zanzibar wakiwemo
watalii wanakuwa salama.
Alieleza kuwa Serikali imeamua
kuweka vifaa vya kisasa vya ulinzi kwa lengo la kuimarisha usalama katika mji wa Zanzibar kwani vifaa
hivyo vina uwezo mkubwa wa kuwabaini wahusika wa matukio mbali mbali kwa haraka
na ufanisi mkubwa.
Sambamba na hayo, Rais Dk.
Shein ameutaka uongozi wa Ofisi hiyo kuongeza juhudi katika kufanya tafiti
zinazohusiana na Ofisi hiyo kwa kuzingatia miongozo na maeneo ya Ajenda ya
Utafiti ya Zanzibar ya mwaka 2015-2020
sambamba na kuibua maeneo mapya ya utafiti ambayo hayakubainishwa katika
mpango huo.
Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alisisitiza haja kwa Ofisi hiyo kutoa elimu
kwa wananchi juu ya matokeo yanayopatikana kutoka kwa mradi huo wa Mji Salama
kupitia CCTV zilizowekwa katika Jiji la Zanzibar.
Nae Waziri wa Nchi Ofisi
ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Haji Omar Kheir
alieleza hatua
zinazoendelea kuchukuliwa katika kuhakikisha Ofisi yake inazijenga barabara za
ndani.
Mapema Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Radhia Rashid
Haroub alisoma taarifa ya Utekelezaji wa Mpango Kazi na kueleza hatua
zinazochukuliwa na Ofisi hiyo katika kuhakikisha inatoa huduma zinazopaswa kwa
wananchi.
Mradi wa huo wa Mji Salama ulizinduliwa rasmi mnamo
Oktoba 3, mwaka 2018 na Rais Dk. Shein ambapo hatua zote hizo ni kuhakikisha
Zanzibar inaendelea kuwa salama huku amani na utulivu ikiendelea kudumishwa
hapa nchini.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment