Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Uongozi wa Wizara ya Ujenzi Mawasiliano na Usafirishaji Ikulu Jijini Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Ujenzi Mawasiliano na Usafirishaji Zanzibar,wakati wa mkutano wa kuwasilisha taarifa za utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo kwa mwezi wa Julai hadi Disemba 2019 /2020, uliofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar, (kulia kwa Rais) Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi.Dkt. Abdulhamid Yahya Mzee na Waziri wa Ujenzi Mawasiliano na Usafirishaji Zanzibar. Mhe.Dr. Sira Ubwa.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameutaka uongozi wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji kuongeza kasi katika kuitumikia Wizara hiyo kutokana na huduma inazozitoa kuwa muhimu kwa wananchi.

Hayo aliyasema leo, Ikulu Jijini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji wakati ilipowasilisha Utekelezaji wa Mpango Kazi  kwa kipindi cha Julai hadi Disemba kwa mwaka wa fedha 2019/2020.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein aliipongeza Wizara hiyo na kuutaka uongozi huo kuendela na kasi ya kufanya kazi vyema ili mafanikio zaidi yaweze kupatikana kwani wananchi waliowengi wanategemea huduma zake. 

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza madhumuni ya Mkonga wa Taifa hasa Serikalini na kueleza umhimu wa Wizara hiyo kuhakikisha kuwa kwa upande wa taasisi za Serikali Zaidi inachojali ni kutoa huduma zaidi kuliko kufanya biashara.

Pia, Rais Dk. Shein alieleza haja kwa uongozi wa Wizara hiyo kuwwaekewa mazingira mazuri zaidi wafanyakazi wake ikiwemo kuwatunza na kuwapa stahiki zao hasa kwa wale wanaofanya kazi za barabara na baharini.

Kwa upande mwengine Rais Dk. Shein alieleza kuwa wapo wale ambao hawana nia nzuri na Wizara hiyo hivyo, ni vyema uongozi ukawaelewa na kutowawacha  wakaendelea kuharibu na badala yake wawachukulie hatua za kisheria.

Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kukaa pamoja kwa Taasisi za Serikali wakati wa maandalizi ya miradi ili kuepuka athari zinazoweza kutokea hapo baadae.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza umuhimu wa kuwepo kwa Wakala wa Serikali wa Karakana Kuu ya Vyombo vya Moto Zanzibar ya  kisasa itakayotoa huduma bora kutokana na uwepo wa wataalamu sambamba na vifaa vinavyokwenda na wakati uliopo.

Dk. Shein pia, alisisitiza haja ya kufuatwa sheria za barabarani hasa ikizingatiwa kuwa baadhi ya madereva hawafuati sheria za barabarani na kuwataka askari Polisi kufanya wajibu wao kwa kuwakamata na kuwapeleka mahakamani.

Akitoa wito wa kupambana na muhali kwa wale wanaovunja sheria zikiwemo za barabarani, Rais Dk. Shein alisema haja ya kufuatwa sheria na kuondokana na muhali kwani huo ndio unaopelekea watu walio wengi kuvunja sheria.

Rais Dk. Shein aliipongeza Wizara hiyo kwa juhudi inazozichukua katika kufuatia miradi ya barabara hasa kisiwani Pemba na kuusifu uongozi wa Wizara hiyo pamoja na watendaji wa Wizara hiyo kwa ufuatiliaji wao huo.

Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliupongeza uwasilishaji na utayarishaji wa taarifa hiyo na kueleza kuwa Wizara hiyo imekusanya vyanzo vingi vya mapato ukiwemo uwanja wa ndege na bandarini hivyo ni lazima watendaji wa wafanyakazi wake wasiwe wa kubahatisha.

Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alieleza kuwa maeneo hayo ni ya kiuchumi hivyo masuala ya ulinzi na usalama ni vyema yafanyiwe kazi kwa azma ya kukuza uchumi wa nchi. 

Nae Waziri wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji Sira Ubwa Mamboya alisema kuwa kwa kipindi cha robo mbili (Julai-Disemba 2019) Wizara hiyo imefanikiwa kukamilisha sehemu ya ujenzi wa barabara mbali mbali Unguja na Pemba kwa kiwango cha lami ikiwemo barabara ya Ole-Kengeja yenye urefu wa kilomita 35.

Alieleza kuwa ujenzi wa barabara hiyo unaendelea na kwa sasa jumla ya kilomita 22.5 zimeshawekwa lami na kazi ya usafishaji kwa barabara yote umekamilika na ujenzi wa barabara hiyo unaendelea kwa hatua mbali mbali za kifusi.

Aliongeza kuwa kati ya kilomita 33.8 za barabara ya Bububu-Mahonda- Mkokotoni, ni kilomita 31 tu zimekamilika kwa kiwango cha lami ambazo zimo kwenye mradi wa ADB na tayari barabara hii imezinduliwa rasmi tarehe 10 Januari 2020, matayarisho ya ujenzi kwa kilomita 2.8 zilizobakia kutoka KwaNyanya hadi Bububu Polisi yameanza.

Kadhalika, alisema kuwa barabara ya kutoka Matemwe hadi Muyuni (Km7.5) nayo imekamilika kwa kiwango cha lami na barabara ya Koani-Jumbi imeshawekwa lami kilomita moja kati ya kilomita 6.3 na kazi ya ujenzi inaendelea.

Alisema kuwa Barabara ya Jozani-Charawe-Ukongoroni yenye urefu wa kilomita 23 kazi ya ujenzi imeanza rasmi ambapo jumla ya kilomita 7 zimekamilika kwa kiwango cha kifusi na matayarisho ya kuweka lami yameanza.

Vile vile, ujenzi wa barabara kutoka Fuoni Polisi hadi Kibonde Mzungu yenye urefu wa Kilomita 1.2 inaendelea kwa hatua mbali mbali za kifusi na mategemeo ni kumalizika mwishoni mwa mwezi huu wa Machi 2020.

Aidha, alieleza kuwa ni matarajio ya Wizara hiyo kuwa jengo la abiria katika uwanja wa ndege wa Abeid Amani Karume litakamilika katika muda uliopangwa hasa ikizingatiwa kuwa Serikali imetenga fedha zake za ndani ili kukamilisha ujenzi huo..

Alisema kuwa Wizara kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege imefanikiwa kuimarisha huduma katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume (AAKIA) kwa kuimarisha ulinzi na usalama wa uwanja kwa kuzifanyia matengenezo mashine za X-ray nane (8) za ukaguzi pamoja na kuliimarisha eneo la mizigo na abiria.

Pia, Waziri huyo alieleza kuwa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege imeanza ujenzi wa uwanja mdogo wa Ndege wa Kigunda (Nungwi) kwa kujenga maegesho ya Ndege, barabara ya kutulia na kurukia ndege pamoja na barabara ya kupitia ndege kwa kiwango cha kifusi na sasa kiwanja hicho kimeanza kazi kwa majaribio.

Pamoja na hayo, Waziri Mamboya alieleza jinsi Wizara kupitia Shirika la Meli inavyoendelea kuzifanyia matengenezo meli zake ili ziweze kuendelea kutoa huduma kama kawaida.

Mapema Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Mustafa Aboud Jumbe akisoma taarifa ya Utekelezaji wa Mpango Kazi alieleza jinsi Wizara hiyo inavyotekeleza miradi mbali mbali ikiwemo ya barabara na hatua Unguja na Pemba.     

Nao viongozi wa Wizara hiyo waliupongeza na kuusifu uongozi wa Rais Dk. Shein ambao umesaidia kwa kiasi kikubwa kuimarika kwa huduma za mawasiliano hapa Zanzibar.

Walieleza kuwa mawasiliano yameweza kusaidia kwa kiasi kikubwa katika kuimarisha sekta za maendeleo ikiwemo utalii sambamba na hatua kubwa zilizofikiwa katika mradi wa “Mji Salama” ambapo matumizi ya Kamera za CCTV zimekuwa zikifanya kazi vizuri katika kuwatambua wahalifu.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.